Header Ads

ARCADO NTAGAZWA ANA KESI YA KUJIBU


Na Happiness Katabazi
 
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imemuona aliyekuwa waziri wa zamani ambaye kwa sasa ni Kada wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Arcado Ntagazwa kwa kosa moja tu la kujipatia kofia,fulana zenye jumla ya thamani ya shilingi milioni 74.9 kwa njia ya udanganyifu  ana kesi ya kujibu.
 
Uamuzi huo ulitolewa jana Hakimu Mkazi Geni Dudu ,ambaye alisema kesi hiyo ilikuja jana kwaajili ya kutoa uamuzi wa kumuona Ntagazwa na wenzake wana kesi ya kujibu au la na kwamba upande wa jamhuri katika kesi hiyo ili kuthibitisha kesi yao waliweza kuleta jumla ya mashahidi wa tano.
 
Hakimu Dudu alisema baada ya kupitia vielelezo na ushahidi uliotolewa na mashahidi watano wa upande wa jamhuri,mahakama yake imefikia uamuzi wa kuona upande wa jamhuri umeweza kuthibitisha kesi yake na hivyo kwa kauli moja mahakama yake inamuona Ntagazwa na washitakiwa wengine akiwemo mtoto wake wana kesi ya kujibu na kwamba anaiarisha kesi hiyo hadi Agosti 2 na 5 mwaka huu, itakapokuja kwaajili washitakiwa hao kuanza kujitetea.
 
Kwa upande wake Ntagazwa ambaye ni pia ni Mwanasheria kitaaluma alieleza kuwa anakusudia kuleta mashahidi wawili wakati atakapoanza kujitetea.
 Mbali na Ntagazwa washtakiwa wengine ni Senetor Mirelya (60) na Webhale Ntagazwa ambaye ni mtoto wa Ntagazwa ambao wanatetewa na wakili wa kujitegemea Alex Mgongolwa.
 
Aprili 23 mwaka jana, ilidaiwa mahakamani hapo na Wakili wa Serikali Ladslaus Komanya mbele ya Hakimu Mkazi Liad Shamshama alidai kuwa Oktoba 22 mwaka 2009 huko Msasani Mikoroshini washtakiwa hao kwania ovu walijipatia fulana 5000 na kofia 5000 zenye jumla ya thamani ya Shilingi milioni 74.9 toka kwa Noel Sevele kwa makubaliano kuwa wangemlipa Sevele kiasi hicho cha fedha katika kipindi cha mwezi mmoja tangu walipochukua vifaa hivyo lakini hata hivyo walishindwa kumlipa na washtakiwa walikana shtaka na kwamba upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika. 
 
Ntagazwa ambaye kwa sasa ni Kada wa Chadema , kabla ya kujiunga na chama hicho miaka minne iliyopita, akitokea chama cha Mapinduzi (CCM).Akiwa mwanachama wa CCM, aliwahi kuteuliwa na rais wa Serikali ya awamu ya pili na ya tatu, Ally Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa kushika nyadhifa za uwaziri katika wizara mbalimbali hadi ilipofika mwanzoni mwa mwaka 2006, Rais Jakaya Kikwete alipounda baraza lake jipya la mawaziri na kuamuacha nje ya baraza hilo. 
 
Ntagazwa ambaye aliwahi kuwa mbunge wa muda mrefu wa Jimbo la Mhambwe kwa tiketi ya CCM, hadi sasa nakumbukwa kwa msemo wake mmoja maarufu aliowahi kuutoa bungeni akiwa Waziri Nchi ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Mazingira alisema ‘Ipo siku wajukuu zetu watafukua makaburi yetu wachunguze ubongo wetu kama tulikuwa na akili timamu’. Ntagazwa alitoa msemo huo kutokana na kutoridhishwa na baadhi ya maamuzi yaliyokuwa yakifanywa na baadhi ya watendaji waliopewa dhamana.
  
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Julai 31 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.