Header Ads

SIRI ZAANIKWA KESI YA JENGO LINALOKARIBIA IKULU




Na Happiness Katabazi

SHAHIDI wa  tatu katika kesi ya matumizi mabaya ya madaraka katika ujenzi wa jengo la ghorofa 18, lililo karibu na Ikulu, Saimon Maembe ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa Manispaa ya Ilala iliwanyima kibali washtakiwa katika kesi hiyo cha kuongeza idadi ya ghorofa kwenye juu.

Kesi hiyo inawakabili vigogo wawili wa Wakala wa Majengo (TBA) ambao ni aliyekuwa Ofisa Mtendaji Mkuu wa TBA, Makumba  Togolai Kimweri na Msanifu Mkuu wa TBA, Richard John Maliyaga.

Washtakiwa hao wanadaiwa kutumia madaraka yao vibaya kwa kutoa kibali cha kupanua jengo hilo kwa kuongeza ghorofa tatu zaidi kutoka 15 hadi 18, bila idhini ya mamlaka husika na bila kufuata Sheria za mipango miji.

Jengo hilo linalomilikiwa kwa ubia kati ya kampuni ya Royalle Orchard Inn na TBA, liko katikati ya Jiji la Dar es Salaam, katika mtaaa wa Chimara,  kitalu namba 45 na 46, karibu na Taasisi ya Saratani Ocean Road, katika  Manispaa ya Ilala.

Akitoa ushahidi wake jana Mchunguzi  wa kesi hiyo toka  Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), alidai wakati anafanya uchunguzi wake aligundua kuwa  Manispaa ya Ilala ilikataa maombi ya washtakiwa hao  kujenga ghorofa 15.

Maembe alidai   licha ya kuwa Wizara ya Ujenzi kutoa waraka kwa TBA ikielekeza kuwa ni lazima ishirikishwe katika mchakato wa uendelezaji wa viwanja vinavyomilikiwa na TBA kwa niaba ya Serikali, hata hivyo washtakiwa hao hawakuishirikisha wizara hiyo katika mradi huo.

Maembe aliyekuwa akiongozwa na  Mwendesha Mashtaka wa Takukuru, Leonard Swai, kutoa ushahidi wake alieleza kuwa alianza kufanya uchunguzi wa ujenzi wa jengo hilo   baada ya  Rais Jakaya Kikwete  na Waziri Mkuu Mizengo Pinda kutoa maelekezo kwa  Takukuru, na kwamba alikabidhiwa jukumu hilo na Kaimu Mkurugenzi wa Takukuru.

Alidai  wakati akifanya uchunguzi wake  alikwenda TBA ambako alipata nyaraka mbalimbali za mradi huo kama vile tangazo la zabuni ya ubia wa ujenzi wa jengo hilo, maombi ya wazabuni na taarifa ya tathmini ya zabuni hiyo.

Alizitaja nyaraka nyingine kuwa ni mihtasari ya vikao na uamuzi wa Bodi ya Zabuni ya TBA, mkataba wa ujenzi wa jengo hilo na vibali vya ujenzi, na kwamba kampuni ya Royalle Orchard Inn ndio ilishinda zabuni hiyo na kwamba  nilibaini kuwa vibali vya ujenzi vilitolewa na TBA, jambo ambalo lilimshangaza nikuona   kuwa vibali vya ujenzi vilitolewa na TBA wenyewe, kwa sababu haikuwa kawaida kwani kuna mamlaka zinazohusika na vibali vya ujenzi.

Maembe alidai kuwa katika  makubaliano ya ubia kati ya TBA na kampuni hiyo, walikuabaliana kujenga jengo kwa ajili ya makazi na biashara na kwamba jengo litakuwa ni la ghorofa 15.
Alidai kuwa kibali cha kwanza kilikuwa ni cha ujenzi wa ghorofa 15 na cha pili kikiwa ni cha upanuzi wa mradi kutoka ghorofa 15 hadi 18 na kwamba vyote vilitolewa na kusainiwa na mshtakiwa wa pili, Maliyaga.

Shahidi huyo alidai kuwa baadaye alikwenda Manispaa ya Ilala ambayo kwa mujibu wa Sheria namba  8 ya Mipango Miji ya mwaka 2007 ndio yenye mamlaka ya kutoa vibali, ili kuona kama walihusika kutoa vibali vya ujenzi huo.

“Kiongozi wa Idara ya Mipango Miji alieleza kuwa waliwahi (washtakiwa) kupeleka maombi ya kibali cha  kujenga ghorofa 15 lakini wakayakataa, kwa sababu hayakuendena na ramani ya mchoro wa eneo husika.”

Maembe alidai   baadaye alikwenda Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambayo ndio yenye uamuzi wa mwisho ya matumizi ya ardhi, na kwamba katika Idara ya Mipango Miji alipata ramani ya eneo husika ya mwaka 2000.
“Maelekezo ya ramani yalikuwa wazi, kwanza ni kuwa matumizi ya ardhi katika eneo husika ni makazi tu na mbili  majengo katika eneo hilo ni ya ghorofa tatu hadi sita. Kwa hiyo niligundua kuwa kilichofanyika katika ujenzi huo kilikuwa kinyume cha sheria.”, alidai shahidi huyo.

Hata hivyo alidai kuwa alipowauliza wizara kama waliwahi kutoa mabadiliko ya matumizi ya ardhi katika eneo husika, walikataa kuwa hawajawahi kupata mnaombi kama hayo.

Katika ushahidi wake shahidi huyo alidai kuwa wakati akichambua nyaraka alizozikusanya, alipata waraka kutoka Wizara ya Ujenzi, ambako TBA iko chini yake, ukiielekeza TBA kuishirikisha katika mchakato wa uendelezaji wa miradi ya viwanja inavyovimiliki.

Hata hivyo shahidi huyo alidai kuwa alipokwenda Wizara ya Ujenzi kuona jinsi walivyoshirikishwa, Katibu Mkuu wa wizara hiyo alisema TBA haikuwahi kuwashirikisha katika mradi huo.
Pia shahidi huyo alidai kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Manunuzi ya Umma, taasisi yoyote ya umma inapotaka kuingia katika ubia na sekta binafsi katia mradi, lazima ifanye upembuzi yakinifu, ili kubaini changamoto, gharama, faida, wadau na namna ya kutatua changamoto za mradi na kwamba hata hivyo TBA haikufanya upembuzi yakinifu katika mradi huo na kwamba.

Alisisitiza licha ya ukiukwaji huo wa sheria katika ujenzi huo, washatakiwa walikuwa na ufahamu wa taratibu zilizopaswa kufuatwa kwani kulikuwa na dokezo kutoka mshatakiwa wa pili kwenda kwa mshtakiwa wa kwanza.
Katika dokezo hilo lililosomwa mahakamani hapo mshtakiwa wa pili alikuwa akieleza kuwa amefanya mawasiliano na Manispaa ya Ilala, lakini imesisitiza kuwa eneo hilo ni la makazi na linahitajika ghorofa tatu hadi sita tu.
Alidai kuwa baada ya uchunguzi huo aliwahoji washtakiwa kutokana na tuhuma hizo ambapo walikiri, katika maelezo yao ya onyo, ambayo aliomba mahakama iyapokee kama kielelezo cha ushahidi.

Hata hivyo upande wa utetezi ukiongozwa na Wakili Majura Magafu, ulipinga kupokewa kwa maelezo hayo na Hakimu Sundi Fimbo aliamuru kesi hiyo ya msingi isimame ili kuendesha kesi ndogo (Trial within a trial) kuona uhalali wa maelezo hayo ya onyo ya washtakiwa na hakimu huyo akaiarisha kesi hiyo hiyo hadi Septemba 5 mwaka huu, itakapokuja kwaajili ya mahakama kuanza kuisikiliza kesi hiyo ndogo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Agosti 29 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.