Header Ads

KORTI KUU YAMPA MUDA JEETU

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu ya Tanzania imeridhia ombi la upande wa walalamikaji katika kesi ya Kikatiba iliyofunguliwa na mfanyabiashara maarufu Jeetu Patel na wenzake watatu dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali la kutaka mahakama hiyo iwapatie siku 10 za kuleta nyaraka nyingine na hati ya kiapo kipya.


Uamuzi huo ulitolewa jana na jopo la majaji watatu waliokuwa wakiongozwa na Jaji Kiongozi, Fakhi Jundu, ikiwa ni saa chache baada ya jopo la mawakili wa utetezi, linaloongozwa na Mabere Marando, kuwasilisha ombi hilo la kuomba waongezewe muda kwani wakati wakipitia jalada la kesi waliyoifungua mahakamani hapo wamebaini kuwa walisahau kuambatanisha nyaraka muhimu ambazo zitapaswa kutumika katika kesi hiyo na kwamba watawasilisha kiapo kipya.

Akitoa uamuzi huo, Jaji Kiongozi Jundu, alisema anakubaliana na ombi hilo na kuutaka upande wa walalamikaji kuwasilisha nyaraka na hati ya kiapo kipya Agosti 14 na upande wa wadaiwa kujibu Septemba 10 na upande wa mlalamikaji kama utakuwa na majibu, wajibu Septemba 24 na kuahirisha kesi hiyo hadi Septemba.

Kwa upande wake, Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface, anamwakilishi mshtakiwa wa kwanza na wa tatu; na wakili wa mdaiwa wa pili Reginald Mengi, Michael Ngaro, aliaambia mahakama kuwa kesi hiyo jana ilikuja kwa ajili ya kutajwa kwa mara ya kwanza, hivyo wakaomba wapewe muda wa kujibu madai hayo na kwamba wana mpango wa kuwasilisha pingamizi kuhusu kesi hiyo.

Mapema Juni 4 mwaka huu, Jeetu na wenzake walifungua kesi hiyo ya Kikatiba Na.30 wakiomba mahakama hiyo itafsri sahihi ya ibara 13 (4,5 na 6 (b) cha Katiba ambacho kinatamka watu wote ni sawa mbele ya sheria na pia itafsiri ibara 13 (6) (b) inayosema mtu yeyote asichukuliwe ana hatia hadi pale mahakama itakapomkuta na hatia.

Kwa mujibu wa hati ya madai, walalamikaji hao wanadai kuwa wamefikia uamuzi huo wa kuiomba mahakama itoe tafsiri ya ibara hizo kwa kuwa wanaamini ibara hizo za Katiba zimevunjwa na Mengi ambaye alitumia vyombo vya habari kuwahukumu kwa kuwaita wao ni ‘Mafisadi Papa’ wakati Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu inayosikiliza kesi zao haijatoa hukumu

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Agosti 7,2009

No comments:

Powered by Blogger.