Header Ads

SERIKALI-UPELELEZI KESI YA LIYUMBA WAKAMILIKA

Na Happiness Katabazi

BAADA ya vuta ni kufute baina ya upande wa utetezi na upande wa mashitaka katika kesi matumizi mabaya na kuisababishia serikali hasara ya Sh bilioni 221 inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala, Amatus Liyumba, jana upande wa mashitaka uliiambia Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika.


Wakili Kiongozi wa Serikali Justus Mulokozi mbele ya Hakimu Mkazi Eva Nkya, alidai kuwa upelelezi umekamilika hivyo unaiomba mahakama hiyo ipange tarehe ya nyingine kwaajili ya kuja kumsomea maelezo ya awali mshitakiwa.

Baada ya wakili Mulokozi kuwasilisha ombi hili, Wakili wa mshitakiwa, Majura Magafu anayesaidiana na Hudson Ndusyepo aliinuka na kutoa madai kuwa upande wa utetezi jana ulikuwa unatarajia upande wa mashitaka ungewa tayari umeishajiandaa hata kwakuwapatia nakala ya maelezo ya awali.

Magafu aliyekuwa akizungumza kwa sauti ya ukali alinukuu kifungu cha 225(4),(5) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai kama ilivyofanyiwa mapitio 2002,kwamba kifungu hicho kinatamka bayana ndani ya siku 60 zinapotimia aidha kesi isikilizwe au ifutwe nakuongeza kuwa kinachoshangaza ni kwamba upande wa mashitaka umekuja kuomba airosho jingine kupitia mlango wa nyuma.

“Sisi upande wa utetezi ni rai yetu kwamba matakwa ya kifungu hicho hayajatimizwa na upande wa mashitaka kwakuwa kesi hii ilifunguliwa Mei 28 mwaka huu, hadi leo(jana) siku 60 ziliisha juzi na hakuna hati ya kuomba kuongezewa muda…hivyo tulitarajia leo wenzetu wangemsomea mteja wetu maelezo ya awali lakini wameshindwa kufanya hivyo.

“Mheshimiwa hakimu sheria za nchi zimetungwa kwaajili ya watu wote wapate haki na taratibu zilizoainishwa kwenye sheria hizo zifuatwe sasa zisipofuatwa ni ukiukwaji wa Katiba ya nchi pia kwani katiba inasema kila mtu ana haki ya kusilizwa…hivyo mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni mjeta wetu yupo mahabusu kwasababu ambazo serikali inazijua na sisi upande wa utetezi tunazijua, basi tunaomba mahakama imwachie.” alidai Magafu.

Akijibu hoja hizo Wakili Kiongozi Mulokozi, alijibu kwa kifupi kwamba kifungu hicho cha 225 kilichotumiwa na wakili Magafu upande wa mashitaka unakijua vizuri mno na kwamba hawakuona haja ya jana kuja ombi la kuongezewa muda kwasababu hakukuwa na amri yoyote iliyotolewa na mahakama iliyokuwa ikitaka kesi hiyo ianze kusikilizwa jana.

Aidha Magafu aliinuka tena na kumtaka Mulokozi ajibu hoja yake ya kutaka kesi hiyo ifutwe na si vinginevyo.Hata hivyo Hakimu Nkya alisema baada ya kusikiliza hoja za pande mbili alisema kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya kutajwa na kuona kama upelelezi kama umekamilika na kuongeza kuwa hata hivyo kesi hiyo ni miongoni mwa kesi zilizopelekwa kwa Jaji Mkuu Agustino Ramadhani ili ziweze kupangiwa jopo la mahakimu wa kuisikiliza hivyo hadi sasa hana taarifa yoyote hivyo akaairisha kesi hiyo hadi Agosti 11 mwaka huu, mshitakiwa atakapokuja kusomewa maelezo ya awali.


Mei 28 mwaka huu, Mulokozi alidai mahakamani hapo kuwa Liyumba anakabiliwa na makosa mawili ya jinai katika kesi hiyo Na.105/2009 kwa matumuzi mabaya ya ofisi ya umma ambapo anadaiwa kuwa kati ya mwaka 2001-2006 akiwa mwajiriwa wa serikali, aliidhinisha ujenzi wa minara pacha, bila idhini ya Bodi ya Wakurugenzi wa Benki Kuu.

Aidha, anadaiwa kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221 kwa uamuzi wake wa kuidhinisha ujenzi wa minara hiyo pacha kosa linaloangukia kwenye shitaka la kwanza.

Liyumba alisomewa mashitaka mapya baada ya Hakimu Mkazi Walirwande Lema, aliyekuwa akisikiliza kesi namba 27/2009 iliyokuwa ikimkabili mshitakiwa huyo na Meneja Miradi wa BoT, Deogratius Kweka, kuwaachia huru baada ya kubaini hati ya mashitaka ilikuwa ina makosa kisheria.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima,Julai 29,2009

No comments:

Powered by Blogger.