Header Ads

MADEREVA WAGOMA,ABIRIA WASOTA DAR

*Wapinga mwenzao kufungwa miaka 30

Na Happiness Katabazi

MAELFU ya abiria waliokuwa wakisafiri kutoka jijini Dar es Salaam kwenda mikoa mbalimbali na nchi jirani, jana walikwama kuondoka katika Kituo Kikuu cha Mabasi Ubungo, baada ya madereva wa mabasi yanayofanya safari hizo kugoma kutoa huduma.


Madereva hao walifikia uamuzi wa kugoma ili kuishinikiza serikali iingilie kati maamuzi ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Tabora, kumfunga miaka 30 jela dereva mwenzao wa basi la Mohamed Trans, aliyesababisha ajali iliyopoteza maisha ya zaidi ya abiria 20.

Mgomo huo wa aina yake ambao haujawahi kutokea nchini kwa miaka ya karibuni, ulianza majira ya saa 12:00 asubuhi ambapo magari yanayokweda mikoa ya Kanda ya Ziwa na Nyanda za Juu Kusini, yalitakiwa kuondoka na kusababisha usumbufu mkubwa kwa abiria waliowahi tiketi tangu asubuhi kwa ajili ya safari.

Tanzania Daima ilishuhudia kundi la madereva wakiwa wamebeba mabango makubwa yaliyosomeka; ‘Kama, dereva miaka 30, Chenge kaua kuku?’, ‘Madereva hatutendewi haki’, ‘Tochi laki tano, rushwa milioni mbili’ na ujumbe mwingine.

Madereva hao pia wanalalamikia vitendo cha askari wa usalama barabarani (trafiki) kuwasimamisha ghafla maeneo ya porini na kuwaomba rushwa.

Walidai kuwa, kumekuwepo na tabia ya askari hao, wanaotanda katika barabara ya Pwani hadi Iringa, kuwasimamisha mara kwa mara na kuwatoza faini ya kati ya sh 20,000 hadi 100,000.

Madereva hao, pia wameilalamikia Mamlaka ya Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (SUMATRA), kwa kupanga ratiba ya magari hayo, isiyoendana na umbali halisi wa vituo.

Tukio hilo lilisababisha msongamano mkubwa wa abiria katika kituo hicho, ambao walilazimika kukaa chini wakisubiri hatma ya safari zao, huku askari polisi na wale wa kuzuia fujo (FFU) wakiimarisha ulinzi.

Wakati wote wa mgomo huo, abiria hawakuweza kumpata mtu wa kumuuliza au kumdai nauli, kwani viongozi wa Jeshi la Polisi na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, walifika eneo hilo, majira ya saa 1:30 asubuhi na kuanza kikao na madereva hao ili kutafuta suluhu.

Viongozi waliofika kwenye eneo hilo ni Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Evance Balama aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa, William Lukuvi, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Jordan Rugimbana na Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova.

Baada ya kuwasili, viongozi hao waliitisha mkutano wa dharura na madereva, ambao waliwaeleza madai yao.

Katika mkutano huo, madereva walifikia muafaka wa kuunda kamati maalum itakayoshirikiana na serikali kushughulikia malalamiko yao haraka iwekekanavyo.

“Malalamiko yenu tumeyasikia na tutayafikisha sehemu husika, nikitoka hapa naenda kuzungumza na IGP Said Mwema na tuone jinsi gani ya kuyatatua… ninawaomba mrejee kwenye mabasi muanze safari za kwenda mikoani,” alisema Kamanda Kova.

Katika kuonyesha kuwa serikali haikubaliani na madai ya madereva hao, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Rugimbana alisema kuwa kama kila dereva akiamua kufanya analotaka kamwe hawatafika na si rahisi kupinga hukumu ya mahakama kwa njia ya mgomo.

“Kama kila dereva akaamua kufanya analowaza, kamwe hatutafika na huwezi kupinga hukumu iliyotolewa na mahakama kwa mgomo, kuna utaratibu wa kisheria,’’ alisema Rugimbana.

Aidha, Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Balama, aliwaambia waandishi wa habari kuwa serikali haiwezi kutatua madai ya madereva hao kwa siku moja, hivyo aliwataka wawe na uvumilivu.

Baada ya makubaliano hayo, madereva hao walisitisha mgomo, na ilipofika majira ya saa 4:16 asubuhi, mabasi yalianza safari zao za mikoani na nchi jirani.
Hata hivyo, baadhi ya abiria waliozungumza na Tanzania Daima, walisema kuwa waliathirika kwa kiwango kikubwa kwani wapo waliotaka kufika mapema sehemu walizotakiwa kwa ajili ya shughuli mbalimbali, zikiwemo za kikazi na mambo ya kifamilia.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Agosti 15,2009

No comments:

Powered by Blogger.