Header Ads

HEKO JWTZ,POLISI KUDHIBITI VURUGU MTWARA





Na Happiness Katabazi

BILA woga wala kumung’unya maneno  napenda kutoa  pongezi  zangu za dhati kwa vyombo vya ulinzi na usalama yaani Jeshi la Ulinzi la Watanzania (JWTZ), chini ya  Jenerali Davis Mwamunyange, Jeshi la Polisi na chini ya Inspekta Jenerali(IGP), Said Mwema na serikali kwa ujumla wake kwa kuweza kuwadhibiti wale wahuni  ambao ni baadhi ya wakazi wa Mtwara ambapo kwa makusudi wiki hii waliamua kuanzisha vurugu kubwa mkoani hapo kwa kisingizio kuwa hawataki bomba la gesi lisije Dar es Salaam.

Maana bila vyombo hivyo kuingia kazini ni wazi machafuko makubwa yangeendelea kutokea na kusababisha  madhara makubwa mkoani hapo.Tena napenda kuvitia moyo vyombo hivyo kuwa viendelee kutimiza wajibu wake bila kuwaonea haya wahuni ambao wana kila dalili za kutumiwa na watu wenye hulka za kinyang’au kwa maslahi yao binafsi ili mwisho wa siku waone Taifa letu nalo likitumbukia katika vita, jambo ambalo wahuni hao ambao wamekamatwa na hao manyang’au wanaowatuma kufanya hivyo hawatafanikiwa.

Hivyo basi vyombo hivyo vya dola vilikuwa sahihi kabisa katika kufanya oparesheni yake kule Mtwara  hadi vimefanikiwa kumaliza ghasia hizo na washiriki wa ghasia hizo wameweza kukamatwa na hivi kinachosubiriwa ni ofisi ya Mkurugunzi wa Mshitaka(DPP),Dk.Eliezer Feleshi na waendesha mashitaka wake kuwafungulia kesi wale wote waliokamatwa wakishiriki uhalifu huo.  

Tanzania itaendelea kuwa ni nchi ya mshikamano na amani yake ni mfano wa kuigwa ulimwenguni licha ya hivi sasa kumeanza kuibuka baadhi ya matukio yasiyopendeza yanayoashiria uvunjifu wa amani lakini,kwakuwa vyombo vya unzi na usalama vipo imara wahusika wanakamatwa na kisha kufikishwa mahakamani na kwa wale wafuasi 53 wa Sheikh Issa Ponda , Machi 21 mwaka huu, Mahakama ya Hakimu Mkazi iliwafunga jela mwaka mmoja baada ya kuwakuta na hatia ya kufanya mkusanyiko haramu, kukaidi amri ya jeshi la polisi.

Na Mei 9 mwaka huu, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu pia ilimhukumu kifungo cha mwaka mmoja nje ,Sheikh Ponda baada ya kumtia hatiani kwa kosa la kuingia kwa jinai katika kiwanja cha Chang’ombe Markas.

Sasa na nyie wahuni wa Mtwara mnaofanya vurugu mjifunze katika hukumu hizo mbili wale vihelehele waliokuwa wakiandamana wakitaka kwenda kwa ofisini kwa DPP-Dk.Feleshi ili wamshinikize aondoe hati yake ya kumfungia dhamana Ponda, walikamatwa na kufikishwa mahakamani na wakafungwa gerezani mwaka mmoja na hivi sasa wamesambazwa katika magereza kadhaa hapa nchini, na huyo Ponda waliyokuwa wakimpigania yeye kafungwa kifungo cha nje.

Sasa na nyie wahalifu mliofanya uhalifu Mtwara nawasii sana mjifunze kutokana na hukumu hizo, kuwa kama kuna mtu anawatuma kufanya uhalifu huo basi mkae mkijua mtu huyo anawatoa kafara nyie kwani mtaoshughulikiwa moja kwa moja ni nyie na mtakaopata madhara makubwa ya kisheria ni nyie.

Na vurugu za madai ya kidini katika mkoa wa Dar es Salaam, baada wahusika kukamatwa na kufikishwa mahakamani, zimetulia, Dar es Salaam, hivi sasa ipo shwari na  nchi inazidi kusonga mbele.Hivyo kule Mtwara napo mamlaka husika inatakiwa itumie sheria kuwashikisha adabu wavunjivu wote wa sheria.

Wiki hii Tanzania ilijikuta ikiandika historia mbaya katika sura ya dunia kwasababu ya ghasia kubwa zilizotokea mkoani Mtwara na kusababisha mtu mmoja kupoteza maisha na wengine,kujeruhiwa na baadhi ya wakazi wa eneo hilo makazi yao na sehemu zao za kufanyia biashara kuaribiwa.

Chanzo cha vurugu hizo zinaelezwa kuwa baadhi ya wakazi wa eneo hilo la Kigoma Mjini kumaliza kusikiliza hotuba ya Wizara ya Nishati na Madini iliyowasilishwa na waziri wa wizara hiyo Profesa Sospitha Muhongo.

Na baadhi ya wakazi wa Mtwara wamekuwa wakikataa gesi iliyogundulika Mtwara, isiletwe Dar es Salaam.
Itakumbukwa kuwa Januari mwaka huu, wananchi wa Mtwara walipozusha ghasia ,niliandika makala na niliiweka kwenye ukurasa wangu wa facebook ambayo dhima ya makala yangu ilikuwa ikimshauri Mkurugenzi wa Mashitaka(DPP),Dk.Eliezer Feleshi awafikishe mahakamani wale wote walioshiriki kwenye vurugu za Januari mwaka huu huko Mtwara kwa kisingizo wanazuia bomba la Gesi lisijengwe kutoka Mtwara kuja Dar es Salaam.

Kuna usemi usemao ‘Vita haina macho’.Sasa vurugu zile zilizotokea wiki hii Mtwara naweza kuzifananisha na vita baaida ya wananchi hao ambao kwa makusudi waliamua kujichukulia sheria mkononi na kuanza kufanya uhalifu na kujibishana jeshi la polisi kwa kisingizio kuwa bomba la gesi lisijengwe kutoka Mtwara kuja Dar es Salaam.
Na matokeo ya kitendo hicho cha kujichukulia sheria mkono kilichofanywa na baadhi ya wananchi wa Mtwara ndicho mwisho wa siku kilichopelekea Jeshi la Polisi kuingia kazini kama  kifungu cha 20, 21(2) vya Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya mwaka 2002 inavyoanisha wazi majukumu ya jeshi hilo.

Ambapo kifungu cha 20 kinampa polisi mamlaka wakati akifanya jukumu lake la ukamataji wa mwarifu/waharifu kuvunja eneo lolote na kuingia kumkamata mwarifu huyo kwa lengo la ku.Wakati kifungu cha 21(1) kinamruhusu ofisa wa polisi kutumia nguvu wakati akikamata waharifu.

Kwa mtiririko huo ndiyo maana nimelazimika kutumia msemo huo kuwa ‘Vita haina macho’ kwani vurugu za Mtwara zilipoanza kufanywa na baadhi ya wakazi wa Mtwara  ambao nao wahuni hao walikuwa na silaha za jadi mkononi zilisababisha Jeshi la Polisi kuingia kazini na kuanza kuwashughulikia wale wote waliokuwa wakifanya vurugu  hizo na mwisho wa siku hata wale ambao hakushiriki katika vurugu hizo kwa njia moja ama nyingine wameathiriwa na vurugu hizo na wengine wakijikuta wamepoteza mahali pa kuishi.

Lakini Binafsi nimekuwa nijikijiuliza kuwa mbona kila kukicha tunasikia kwenye vyombo vya habari vikitoa nafasi kubwa ya kusikika habari za wale wahuni wanaofanya vurugu Mtwara lakini hatuoni vyombo hivyo vya habari vikitoa nafasi kwa wakazi wengine wa Mtwara ambao hawawaungi mkono wahuni hao?

Je ina maana ni wakazi wote wa Mtwara wanataka bomba la gesi lisijengwe kuja Dar es Salaam kwa niia ya vurugu kama zile? Kule Mtwara kuna waandishi wenzetu lakini mbona hatusikii waandishi wenzetu hao wakienda kuwahoji wakazi wa Mtwara ambao wanapingana na wenzao kwa kuwasilisha madai yao kwa njia ya vurugu?

Wakati umefika sasa kwa waandishi wenzetu wa Mtwara kutuletea habari toka kwa wananchi wengine ambao hawaungi mkono kudai dai hilo kwa njia ya vurugu.Kwani kwa kushindwa kufanya hivyo,jamii italazimika kuamini wakazi wote wa Mtwara nao wanaunga mkono wahalifu hao.

Maana binafsi sikubaliani kuwa ni wakazi wote wa Mtwara wanawaunga mkono wenzao wale wanaodai kiwanda cha gesi kijengwe Mtwara kwa njia ya vurugu.  

Sote tunafahamu kuwa Tanzania ni nchi inayoongozwa kwa kufuata utawala wa sheria, na inamruhusu mtu yoyote yule ambaye anaona haki yake imeporwa au kuvunjwa aende mahakamani kuidai.

Sasa hawa waliofanya vurugu Mtwara walikuwa wanapaswa kwenda kudai dai hilo kwa njia ya amani na kama wangeshindwa wangechangisha fedha wakamweka wakili ,akafungua kesi ya madai ya kupinga bomba hilo lisijengwe kuja Dar es Salaam, kwaniaba yao,kuliko uhuni walioufanya.

Licha kuna watu wamekuwa wakidai kuwa wananchi hao hawajapewa elimu ya kutosha, mi binafsi sikubaliani na hilo kwani elimu imetolewa ila tu hawa waliofanya vurugu tayari wana ajenda yao mbaya mioyoni na akili mwao.

Kwani hata kama hoja ni kwamba hawajapewa elimu ya kutosha, ni kwanini siku Waziri wa Nishati Profesa Mhongo alipomaliza kusoma bajeti yake,wakaanzisha vurugu?Tena kama ya bajeti kusomwa siku mbili nyuma walisambaza vipeperushi vya kufanya vurugu siku hiyo.

Tuwaulize wahalifu wale hivi siku hiyo Waziri Mhongo aliingia mkataba na wahalifu wale wa kuwapatia elimu ya gesi akiwa bungeni wahalifu wale ?

Tunachokifahamu sisi waziri huyo alikuwa akienda kusoma bajeti ya wizara inayohusu nchi nzima siyo wakazi wa Mtwara.Kwahiyo nasisitiza kuwa wale waliofanya vurugu Mtwara ni wahuni na ni wahalifu kama walivyowahalifu wengine, na sheria za nchi zipo ,na ziwashughulikie kikamilifu ili wasiweze kurudia kufanya uhalifu huo ambao umesababisha watu kupoteza maisha, makazi ya watu kuaribiwa.

Nafahamu watu watailamu jeshi la polisi ,lakini tunapaswa tujiulize kwanza hivi kama wale wahalifu wasingezusha vurugu siku ile, jeshi la polisi na JWTZ lingeingia mtaani kukabiliana na wahalifu wale?Jibu ni jepesi tu ,JWTZ na Polisi wasingepoteza muda na nguvu zao kuingia mtaani mjini Mtwara na kupambana na wahalifu wale ambao tayari wameishaipaka matope nchi.

Kwa kitendo kile walivyokifanya ,hata kama walichokuwa wakikidai ni sahihi, wakae wakijua wamevunja sheria za nchi, na watafikishwa mahakamani kwa makosa ambayo yatakuwa yameandaliwa na waendesha mashitaka wetu na hapo ndipo itakapokuwa imeanza safari yao ya utumwa baina ya wahalifu hao  na Mahakama na mahabusu.

Kwa watu wanaofikiri sawa sawa ,inawawia vigumu kuamini hawa wananchi ni wao wenyewe ndiyo wanaojituma kufanya uhalifu huo ule kwa kisingizio cha dai hilo.

Kwani hawa wananchi kwa muda mrefu walikuwa wakilalamika kucheleweshea malipo yao ya mauzo ya Korosho lakini hata siku moja hatujawahi kuwaona wakifanya uhalifu wa haina ile.

Na kama kweli dai lao ni hilo ni la kukataa bomba la gesi lisije Dar es Salaam, dai ambalo na fahamu haliwezi kutekelezekwa kwasababu ni dai lisilo na tija ,ni kwanini wahalifu hao wakimbilie kuchoma nyumba za viongozi ,mahakama, ofisi za CCM,na nyumba ya Mwandishi wa Habari ?

Naviomba vyombo vya dola ikiwemo Polisi, JWTZ na Idara ya Usalama wa Taifa, ifanye kazi yake ya uchunguzi ili kujua kama kweli wahalifu hao wanadai hilo kweli? Nani anawapa jeuri na morali wahalifu  hao kufanya uhalifu ule bila woga tena kwa njia haramu?

Huenda kuna kikundi cha wadhalimu kipo nyuma ya hawa wahalifu kina watuhumia wahalifu hawa kufanya uhalifu huo kwa kisingizio cha kukataa bomba hilo lisije Dar es Salaam,wakati wakifahamu wazi hao wahalifu wanachokikataza hawana mamlaka nacho.

Naamini dola likiamua kufanyakazi yake kikamilifu huko Mtwara,inauwezo wa kubaini kilichopo nyuma ya pazia ya chanzo cha vurugu hizo na itawadhibiti na dai hilo litakuwa ndoto kwa wahalifu hao.

Kwani mifano ya dola kusambaratisha vikundi vya wahalifu hao hao ni mingi sana na wala si yakutafuta.Mfano vyombo vya ulinzi na usalama vilivyofanikiwa kuwasambaratisha wale baadhi ya waumini wa dini ya Kiislamu Mkoani Dar es Salaam, mwaka jana na Machi mwaka huu ,waliokuwa wakiendesha maandamano haramu kwa kisingizio cha kutetea uislamu, kutokomeza ujambazi katika mikoa ya Kigoma, Kagera na Arusha, vurugu za Msikiti wa  Mwembe Chai, ujambazi wa kutisha katikati ya jiji la Dar es Salaam, kati ya miaka ya 2006 muda mfupi tu tangu Rais Jakaya Kikwete Desemba 21 mwaka 2005, alipoapishwa kushika madaraka ya urais.

Narudia tena bado ninaimani kubwa na vyombo vya ulinzi na usalama kuwa vikiamua kufanya kazi vinafanyakazi yake kikamilifu na ndiyo maana hata leo hii nimejitokeza kuvipongeza kwa kuweza kurejesha amani mkoani Mtwara ambayo ilitoweka kwa siku mbili kwaajili ya vurugu baina ya wahalifu wale na vyombo vya dola.

Niitimishe makala yangu kwa kuvipongeza vyombo kwa kufanya oparesheni hiyo ambayo imezaa matunda na kukata ngebe za hao wahalifu ambao ambao kama ya kupata mkong’oto wa wana usalama walijitapa kuwa wapo tayari kufa kwaajili ya kuipigania gesi.

Lakini cha kushangaza wahalifu hao waliokuwa wakijitapa kuwa hawaogopi dola, leo hii wamefya mkia kwa kuhofia oparesheni hiyo.

Nimejiuliza kuwa hivi mpiganaji gani ambaye ameapa kufa kwaaiili ya kuipigania gesi asalimu amri baada ya polisi kuwatembezea mkong’oto?

Shujaa au mpiganaji yoyote huwa aogopi polisi wala bunduki.Sasa iweje hawa waliojitapa kutoliogopa dola na kuamua kujichukulia sheria mkononi leo hii wameona JWTZ na Polisi wamekalia kooni wameshusha silaha chini? Ni wazi hawa ni watu waoga kwani kama siyo waoga wangejitokeza kupambana na askari hao ili tuwajue kuwa nao ni mahodari na wapo tayari kwa lolote.

Tanzania ni nchi inayooendelea hivyo binafsi sioni kama ni muda mwafaka kwa sisi wananchi hususasini wakazi wa Mtwara kuanza kujiingiza kwenye vurugu badala ya kushiriki kwenye shughuli za kujiletea maendeleo na taifa letu.

Wanahabari na wananchi wengine wote wapenda amani na tunaoheshimu utawala wa tuukatae uhuni unaofanywa na wahalifu wale wanaofanya vitendo vya uvunjifu wa amani kwa kisingizio cha kuzuia bomba la gesi lisijengwe kuja Dar es Salaam,kwani una hatarisha amani na wanaoteseka ni watoto na wanawake na miundombinu yetu inaaribika ambayo imejengwa kwa kodi zetu.

Pia napenda kutoa raia kwa wale wananchi wote ambao wamechoka kuishi hapa Tanzania katika nchi yenye amani, basi ni wakati mwafaka kwa watu hao wapenda vurugu kwenye kuamia katika nchi zenye vita ili wakaishi huko kwenye nchi zenye vita wafurahi zaidi ,kuliko kuishi hapa nchi na kuanza kutuletea vurugu ambazo zinahatarisha amani yetu ambazo sisi wengine hatutaki vita jamani.

Mwisho nimalizie kwa kuvipongeza vyombo ya dola yaani Polisi na JWTZ kwa kuweza kuwadhibiti wahalifu wale walioleta vurugu kule Mtwara.Na itafute chanzo cha vurugu hizo kwani hii ni mara ya pili sasa wahuni wale wanazusha vuru hizo kwa kisingizo hicho na mara ya kwanza vurugu ambazo zilisababisha pia watu kupoteza maisha ni Januari mwaka huu.

Mungu ibariki Tanzania,Mungu Ibariki Afrika
Chanzo: www.katabazihappy.blogspot.com
Facebook:happy katabazi  , Mei 26 mwaka 2013.
  
0716 774494



No comments:

Powered by Blogger.