Header Ads

MENEJA BENKI YA CRDB JELA MIAKA MITANO KWA WIZI



Na Happiness Katabazi,Mwanza

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Mwanza, imemhukumu kifungo cha miaka mitano jela Meneja wa Benki ya CRDB,wa matawi ya Nyanza na Bugando mkoani Mwanza, Daniel Peter Waijaha, pamoja na mteja wa benki hiyo, Dismas Mohamed Ndaliko  baada ya kuwakuta na hatia  wa kosa la wizi wa jumla ya  Sh Milioni 140 mali ya benki hiyo.

Hukumu hiyo ilitolewa na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mwanza,  Anjelo Rumisha ambaye alikuwa akisikiliza kesi hiyo ya jinai Na.76 ya mwaka 2011.Ambapo mbali na adhabu hiyo pia hakimu huyo amemtaka meneja huyo azirejeshe fedha hizo alizoziiba katika Tawi la Nyanza.

Hakimu Rumisha alisema baada ya kumtia hatiani meneja huyo pia Meneja wa Business Banking, Stephano Harry Mboma, ambaye alikuwa mshatakiwa wa pili katika kesi hiyo amemuachia huru  baada ya kuona hana hatia katika mashitaka dhidi yake.



Kwa upande wake Ndaliko (mteja) ambaye alikuwa mshtakiwa wa tatu katika kesi hiyo alihukumiwa adhabu hiyo kwa kosa la kujaribu kumsaidia meneja huyo kuepukana na adhabu kwa kufuta ushahidi wa kosa hilo.
Wakati meneja huyo na mteja wakihukumiwa adhabu hiyo, Meneja wa Business Banking, Stephano Harry Mboma, ambaye alikuwa mshatakiwa wa pili katika kesi hiyo ameachiwa huru baada ya kuonekana kuwa hana hatia katika mashtaka yote yaliyokuwa yakimkabili.

Hukumu hiyo ilitolewa na Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mwanza, Jumatatu ya Juma hili, Anjelo Rumisha, aliyekuwa akisikiliza kesi hiyo.
Hata hivyo licha ya kuwatia hatiani washtakiwa hao kwa mashtaka hayo, na kuwahukumu adhabu hiyo, Hakimu Rumisha aliwaachia huru katika mashtaka mengine yote yaliyokuwa yakiwakabili.

Upande wa mashtaka  uliokuwa ukiongozwa na Wakili wa Serikali Mwandamizi, David Kakwaya haukuridhika na uamuzi huo wa washtakiwa hao kuachiwa huru katika mashtaka mengine, na tayari umewasilisha taarifa ya kusudio la kukata rufaa.

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, washtakiwa wote kwa pamoja  walikuwa wakikabiliwa na jumla ya mashtaka matano, lakini ni mashtaka mawili tu ndio yalikuwa yakiwahusu washtakiwa wote watatu, ambayo ni kula njama kutenda kosa na kughushi.

Katika shtaka la kwanza washtakiwa wote walikuwa wakidaiwa kuwa katika tarehe tofautitofauti katika miezi isiyofahamika, mwaka 2010, walikula njama kutenda kosa la kughushi nyaraka.

Shtaka la pili lilikuwa ni la wizi likiwahusu mshtakiwa wa kwanza Meneja Waijaha na mshtakiwa wa pili, Mboma. Walidaiwa kuwa katika  tarehe na miezi isiyofahamika mwaka 2010, kwa pamoja waliiba Sh 107.8 milioni katika benki hiyo tawi la Nyanza.

Shtaka la tatu ambalo pia ni wizi lilikuwa likiwahusu mshtakiwa wa  kwanza, Waijaha na wa tatu, Ndaliko (mteja). Walidaiwa kuwa Desemba 4, 2010, katika benki hiyo tawi la Bugando, waliiba Sh32.15 milioni mali ya benki hiyo.

Katika shtaka la nne la kughushi, washtakiwa wote walikuwa wakidaiwa kuwa kati ya Desemba 4, 2010, katika tawi la Bugando, kwa pamoja walitengeneza nyaraka za uwongo za kuchukulia pesa benki kwa lengo la kufanya udanganyifu.

Ilidaiwa kuwa lengo la nyaraka hizo za uwongo lilikuwa ni mteja mmoja aitwaye New Ana  Filling Station, mmiliki wa akaunti namba 01J1016800800, alichukua pesa kiasi cha Sh 140 miloni katika tawi hilo, jambo ambalo halikiuwa kweli.

Mshtakiwa wa tatu (Ndaliko) pia alikuwa pia akikabiliwa na shtaka mbadala la kusaidia kutendeka kwa kosa la wizi.
Alidaiwa kuwa kati ya  Desemba 4, 2010,  na kwa siku nyingine baadaye , akijua kuwa mshtakiwa wa kwanza aliiba pesa jumla ya Sh140 milioni mali ya CRDB, alimsaidia kufuta ushahidi ili kumwezesha kuepuka adhabu.
Shtaka la tano ni la kuwasilisha nyaraka za uwongo, lililokuwa likimkabili mshtakiwa wa kwanza peke yake (Meneja Waijaha).

Ilidaiwa kuwa Desemba 4, 2010 katika tawi la CRDB Bugando Mwanza, akijua na kwa udanganyifu, alitoa risiti ya benki ya kuchukulia pesa kwa lengo la kuonesha kuwa ilisainiwa na mteja, New Ama Filling Station na akaunti namba 01J1016800800, jambao ambalo si kweli.

Kwa mujibu wa maelezo ya awali ya kesi waliyosomewa washtakiwa hao, wizi huo ulibainika baada ya Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Ndani kumwagiza mkaguzi wa ndani kufanya ukaguzi wa kushtukiza katika tawi la Nyanza.

Uamuzi huo wa Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Ndani kuamuru kufanyika kwa ukaguzi wa kushtukiza katika tawi hilo ulitokana na taarifa zilizopatikana kuwa kulikuwa na tofauti kubwa ya ulali wa pesa katika tawi hilo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Mei 30 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.