Header Ads

MAHAKAMA YA RUFAA KUMSIKILIZA SHEIKH FARID JUNI 10



Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Rufani nchini, Juni 10 mwaka huu, inatarajia kuanza kusikiliza ombi lililowasilishwa  na viongozi wa Jumuiya ya Uhamsho  na Miadhara iliyokatwa na kiongozi wa jumuiya hiyo  Sheikh Farid Hadi Ahmed na wenzake tisa dhidi ya Mkurugenzi wa Mashitaka  wa Zanzibar.

Ombi hilo ambalo limepewa Na. 1/2013, Sheikh Farid na wenzake wanaiomba Mahakama hiyo, itoa amri ya kuifuta rufaa iliyowasilishwa na DPP, Aprili 15, ya mwaka huu, kwa sababu hadi sasa hakuna  rufaa iliyokuwa imefunguliwa mahakamani ya kupinga amri ambazo zilitolewa na mahakama.
Kwa mujibu wa ratiba za vikao vya Mahakama ya Rufani, maombi hayo yanatarajiwa kusikilizwa na Jopo la Majaji watatu January Msoffe, Salum Massati na William Mandia.

Mbali ya Sheikh Farid, waombaji wengine ni Mselem Ali Mselem,  Mussa Juma Mussa, Azan Khalid, Suleiman Juma Suleiman, Khamis Ali Suleiman, Hassan Bakar Suleiman, Ghalib Ahmada Juma,Abdallah Said na Fikirini Fikirini.

Sheikh Farid na wenzake waliwasilisha maombi hayo chini ya hati ya dharura na wameonyesha tangu Oktoba 25, mwaka 2012  hadi leo wanaishi gerezani  na kwamba kama maombi hayo yatacheleshwa  kusikilizwa hivyo kama yakicheleweshwa kusikilizwa yatasababisha waendelee kusota gerezani kwa muda mrefu na hivyo kuwaletea madhara na usumbufu.

Sheikh Farid anadai  taarifa ya kukata rufaa ya DPP haihusiani na uamuzi ulitolewa Machi 11, mwaka 2013 ambao mdaiwa (DPP), anaupinga.

Na kwamba katika maombi ya DPP hayajaambatanishwa na kiapo cha mwapaji  ambapo mwapaji ni wakili wa Sheikh Farid , Abdallah Juma Mohammed, ambaye anadai kuwa Oktoba 25, mwaka 2012 waombaji walishitakiwa kwa makosa manne chini ya sheria ya Usalama wa Taifa na Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002.

Wanadai kuwa , mashitaka dhidi yao  walisomewa mbele ya Msajili wa Mahakama Kuu ya Zanzibar siku hiyo, lakini hawakupewa nafasi ya kujibu kwasababu msajili hana mamlaka ya kusikiliza mashitaka hayo.
 
Wakili Abdallah anadai waombaji waliomba kudhaminiwa mbele ya msajili ambapo Wakili wa Serikali alipinga  maombi hayo kwa msingi wa kuwa kuna hati ya DPP wa Zanzibar chini ya Sheria ya Usalama wa Taifa kwamba usalama wa nchi ungetetereka hivyo mahakama isiwape dhamana.
 
Wakili huyo anadai  Msajili aliwanyima dhamana  wateja wake  na kuwaamuru warudi rumande hadi Novemba 8, mwaka 2012, kesi ilipokuja kwaajili ya utajwa.
 
Kwa mujibu wa wakili huyo, waombaji hawakuridhika na uamuzi na kuwasilisha maombi ya marejeo ya uamuzi Mahakama Kuu ya Zanzibar lakini mlalamikiwa aliwasilisha pingamizi la awali akiomba mahakama itupilie mbali maombi hayo.

Anadai baada ya  Jaji Abraham Mwampashi wa Mahakama Kuu  kusikiliza maombi ya marejeo na pingamizi la awali la DPP, Machi 11, mwaka huu, alitoa uamuzui wa kutupilia mbali pingamizi na kufuta mwenendo mzima uliokuwa chini ya msajili na uamuzi wa maombi ya dhamana.

Wakili huyo anadai kuwa  Machi 12, mwaka huu,DPP   aliwasilisha taarifa ya kukata rufani kupinga uamuzi wa Jaji Mwampashi kutupilia mbali pingamizi lake la awali na kuwasilisha sababu za kukata rufani.

Hata hivyo, wakili huyo anadai kuwa uamuzi wa Mahakama Kuu wa Machi 11, mwaka 2013, hauwezi kupingwa kwa njia ya rufani wala ya marejeo mbele ya Mahakama ya Rufani.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Mei 22 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.