Header Ads

MAHAKAMA YAAMURU ROBERT KISENA WA SIMON GROUP AKAMATWE






Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imetoa amri ya kutaka mshitakiwa wa nne katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la UDA,Idd Simba, Mkurugenzi  Mtendaji wa Kampuni ya Simon Group Limited,Robert Simon  Kisena akamatwe na kufikishwa mahakamani kwaajili ya kuja kukabiliana na kesi inayomkabili.

Amri hiyo ilitolewa jana  na Hakimu Mkuu Mfawidhi wa mahakama hiyo Elvin Mugeta baada ya kuridhia ombi la wakili wa serikali Awamu Mbagwa na mawakili wa utetezi Alex Mgongolwa na Romani  Lamwai ambao walitaka Kisena ambaye ni mshitakiwa wa nne katika kesi hiyo akamatwe na akifikishwe mahakamani hapo ili kesi iweze kuendelea.

Wakili wa Serikali Mbagwa alianza kwa kuikumbusha mahakama hiyo kuwa kesi hiyo jana ilikuja kwaajili ya upande wa jamhuri kuwasomea maelezo ya awali washitakiwa lakini upande wa jamhuri hautaweza kuwasomea maelezo hayo kwasababu mshitakiwa wanne(Kisena),bado hajakamatwa na kwamba hawezi kuwasomea maelezo ya awali washitakiwa watatu  wakati mshitakiwa wanne hayupo kwani kufanya hivyo ni kusumbua muda wa mahakama .

“Sisi upande wa jamhuri tulikuwa tayari kwaajili ya kuwasomea maelezo ya awali wa washitakiwa lakini kwasababu mshitakiwa wa wanne hayupo mahakamani na taarifa tulizonazo bado hajakamatwa tunashindwa leo (jana)kuwasomea maelezo hayo…hivyo tunaomba mahakama hii itoe amri ya Kisena akamatwe na haweze kufikishwa mahakamani ili aje kukabiliana na kesi inayomkabili”alidai wakili Mbagwa.

Kwa upande wao mawakili wa utetezi Mgongolwa na Masumbuko nao walidai wanaunga mkono hoja hiyo ya wakili wa jamhuri ya kutaka Kisena akamatwe na kwamba kesi hiyo iarishwe kwa hairisho la muda mfupi kwani wanaamini serikali inamkono mrefu na ainayafahamu haya makazi ya Kisena na kwamba  hadi kufikia jana ilikuwa ni siku 25 tangu kesi hiyo ilipofunguliwa upya mahakamani na Kisena akaunganishwa katika kesi hiyo lakini cha kushangaza hadi leo Kisena hajakamatwa na kufikishwa mahakamani.

“Kesi hii ina watesa wateja wetu kwani hadi sasa hawafahamu makosa yanayowakabili kwa kina, hawapati ajira sehemu nyingine kwasababu ya kesi hii…hivyo na sisi mawakili wa utetezi tunaunga mkono kuwa Kisena akamatwe aletwe mahakamani ili kesi hii iweze kuendelea na kwamba Kisena ni mtu anayetafutwa sana na serikali na hata Aprili 30 mwaka huu, kesi hii ilipofunguliwa rasmi Kisena pia hakuwepo mahakamani na hivyo hakuweza kusomewa mashitaka yake ambapo siku hiyo kesi hiyo iliarishwa hadi leo lakini pia leo Kisena hajafika mahakamani”alidai wakili Masumbuko.

Akitoa amri ya mahakama, hakimu Mugeta alisema amesikiliza maombi ya mawakili wa pande zote mbili na kwamba mahakama yake inatoa amri ya Kisena akamatwe na afikishwe mahakamani na akaiarisha kesi hiyo hadi Juni 4 mwaka huu ambapo Simba na wenzake wataendelea kuwa nje kwa dhamana.
Aprili 30 mwaka huu, upande wa jamhuri uliifuta kesi ya awali  ya matumuzi mabaya ya madaraka iliyokuwa ikimkabili Simba na wenzake wawili na kisha kufungua kesi mpya yenye mashitaka sita yakiwemo mashitaka ya rushwa na uhujumu uchumi  na kisha kumuunganisha Kisena katika kesi hiyo ambapo katika kesi ya awali iliyofutwa Kisena alikuwa ni shahidi wa upande wa jamhuri na hivyo kufanya kesi hiyo ya makosa ya rushwa, uhujumu uchumi kuwa na jumla ya washitakiwa wa nne hivi sasa.   

Ilidai siku hiyo ya Aprili 30 kuwa washitakiwa wanne na wakili Mwandamizi wa Serikali Oswalid Tibabyekomya  wanakabiliwa na makosa ya rushwa,uhujumu uchumi,matumizi mabaya ya madaraka na kulisababishia shirika hilo hasara ya Sh. Bilioni 8.4. Na kwamba Tibabyekomya alieleza kuwa baada ya kuyachambua makosa hayo wamebaini kuwa yanaangukia katika Sheria ya Uhujumu Uchumi

Mbali na Idd Simba ambaye ni mshtakiwa wa kwanza na Kisena ambaye ni mshtakiwa wa nne, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ya Uhujumu Uchumi namba 3 ya mwaka 2013, ni Salimu Mwaking’inda na Victor Alfred Milanzi.Mwaking’inda, ambaye ni mshtakiwa wa pili katika kesi hiyo alikuwa Mkurugenzi wa UDA na Milanzi ambaye ni mshtakiwa wa tatu, alikuwa ni Meneja Mkuu wa UDA.

Washtakiwa hao walisomewa mashtaka hayo mapya  katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na walisomewa mashtaka hayo na Wakili wa Serikali Awamu Mbagwa. Hata hivyo Kisena hakuwapo  mahakamani wakati wenzake wakisomewa mashtaka.

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka waliyosomewa jana, shtaka la kwanza la kula njama linawahusu Simba na Milanzi na Kisena.

Washtakiwa hao wanadaiwa kuwa kati ya Septemba 2009 na Januari 2010, jijini Dar es Salaam, kwa pamoja walikula njama za kutenda kosa la vitendo vya rushwa, kinyume cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa.

Kwa mujibu wa hati hiyo ya mashtaka, shtaka la pili la vitendo vya rushwa linamhusu Kisena peke yake, hata hivyo shtaka hilo halikusomwa kutokana na mshtakiwa huyo kutokuwapo mahakamani.

Shtaka la tatu ni la vitendo vya rushwa ambalo linawahusu Simba na Milanzi. Wakili Mbagwa alidai kuwa kati ya Septemba 2009 na Januari 2010, walikubali kupokea Sh320 milinoni kutoka kwa Kisena ushawishi wa kuiuzia Simon Group hisa za UDA ambazo zilikuwa bado hazijagawiwa.Katika shtaka la nne ambalo ni la matumizi mabaya ya madaraka, linawahusu Simba , Mwaking’inda na Milanzi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Mei 21 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.