Header Ads

PONDA AFUNGWA MWAKA MMOJA






 Na Happiness Katabazi
 
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imemhukumu kifungo cha nje cha mwaka mmoja   Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Sheikh Ponda Issa Ponda aliyekuwa akikabiliwa na kesi ya uchochezi na wizi wa malighafi zenye thamani ya Sh.milioni 59  baada ya kumkuta na hatia katika kosa moja la kuingia kwa jinai katika kiwanja cha Chang’ombe Markazi.

Sambamba na hilo, mahakama hiyo imewaachiria huru washitakiwa wengine 49 baada ya kuwaona hawana hatia katika makosa matano yote waliyokuwa wakishitakiwa nao kwasababu upande wa jamhuri umeshindwa kuleta ushahidi wa kuishawishi mahakama iwaone wanahatia  na kwamba akasema upelelezi uliofanywa na jeshi la polisi katika kesi hiyo ni dhahifu na kwamba mahakama haiwezi kumfunga mtu kwa ushahidi wa hisia tu.

Akisoma hukumu hiyo kuanzia jana saa 3:36-5:56 asubuhi alisema upande wa jamhuri ulikuwa ukiwakilishwa na Wakili Mwanadamizi wa Serikali Tumaini Kweka  katika kuthibitisha kesi yake walileta jumla ya mashahidi 16 na upande utetezi uliokuwa ukiwakilishwa na mawakili wa kujitegemea Nassor Juma, Njama ambapo alisema washitakiwa hao walikuwa wakikabili na kosa la kula njama, kuingia kwa nguvu, kuzuia kwa nguvu, wizi wa   malighafi zenye thamani ya Sh.milioni 59 na uchohezi ambalo kosa hilo la uchochezi lilikuwa likimkabili Ponda na mshitakiwa wa tano tu (Mukadamu Abdalah).

Hakimu Nongwa alisema baada ya kupitia ushahidi wa pande zote amebaini kuwa jamhuri limeshindwa kuthibitisha kosa la kwanza ambalo ni la kula njama kwani kosa hilo kwa mujibu wa hati ya mashitaka limeshindwa kueleza kuwa washitakiwa hao walikula njama kutenda kosa gani na kwasababu hiyo kosa la kula njama, kosa la tano la kula njama kutenda kosa la uchochezi nalo limeshindwa kuthibitika jamhuri imeshindwa kuleta ushahidi unaonyesha Ponda na Mkadamu walimshawishi nani kutenda kosa hilo na hivyo anakubaliana na hoja za mawakili wa utetezi kuwa kosa hilo limeshindwa kuthibitishwa.

Akilichambua kosa la pili ambalo ni la kuingia kwa jinai katika kiwanja cha Markazi ,hakimu Nongwa alisema kwa mujibu wa ushahidi wa upande wa jamhuri unaonyesha washitakiwa waliingia katika kiwanja ila hawakuweza kuwatambua washitakiwa hao  licha  Ponda katika utetezi wake alieleza mahakama kuwa walianza ujenzi wa msikiti wa muda katika eneo hilo Oktoba 12 mwaka jana ana alikiri yeye na wenzake ambao hawakutambuliwa mahakamani walishiri kujenga msikiti wa muda.

“Mahakama hii imeona Ponda amepatiakana na hatia katika kosa hili la kuingia kwa jinai katika kiwanja cha Markazi kwani kifungu cha 85 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002 ,ambayo inasema kuingia kwa jinai ni kwa mshitakiwa aingie kwenye kiwanja kwa kuhusisha idadi kubwa ya watu, kuingia kwa nguvu au kwa nguvu lakini kwa ushahidi uliotelewa umethibitisha Ponda aliingia katika kiwanja hicho na kwasababu hiyo mahakama hii inamuona ana hatia katika kosa hilo la pili la kuingia kwa jinai Ponda peke yake”alisema Hakimu Nongwa.

Kuhusu  kosa la kuzuia kwa nguvu , hakimu alisema pia jamhuri imeshindwa kulithibitisha na kwamba hakuna ushahidi unaonyesha washitakiwa walionza kujenga msikiti ule wa muda Oktoba 12  ndiyo walewale waliokamatwa Oktoba 14 mwaka jana  nakwamba hakuna ushahidi unaonyesha ujenzi wa msikiti ule wa muda ulileta hali ya uvunjifu wa amani na kwamba Ponda na hao wenzake ambao hawajatambuliwa walitumia malighafi za kampuni ya Agritanza kujengea msikiti ule.

Hakimu Nongwa kuhusu kosa la wizi ,pia upande wa jamhuri umeshindwa kulithibitisha kwamba msikiti ule wa muda ulijengwa na malighafi za kampuni ya Agritanza na kwamba hakuna ushahidi ulioletwa ukaonyesha malighafi za ujenzi wanazotuhumiwa washitakiwa kujengea msikiti wa muda katika kiwanja cha Markas za kampuni ya Agritanza zilikuwa na thamani ya Sh.milioni 59 na kwamba hakuna ushahidi ulioletwa unaonyesha msikiti wa muda ulijengwa kwa malighafi za kampuni ya Agritanza.

“Mahakama hii imeona ushahidi ulioletwa na upande wa jamhuri ambao upelelezi ulifanywa na jeshi la polisi ni dhahifu na ndiyo maana mahakama yake imewachiria huru washitakiwa 49 katika makosa manne yaliyokuwa yakiwakabiri kwasababu yameshindwa kuthibitishwa na ninawashauri mawakili wa serikali muwe makini katika uandaaji wa hati zenu za mashitaka”alisema Hakimu Nongwa.

Wakili Kweka aliomba mahakama itoe adhabu kali kwa Ponda ili iwe fundisho kwa wengine. Kwa upande wa wakili wa Ponda, Njama aliomba mahakama impatie mteja wake adhabu ndogo kwani hiyo ni mara yake ya kwanza kukutwa na hatia na kwamba amekaa gerezani muda mrefu toka Oktoba 18 mwaka jana hadi jana kwani Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP), Dk.Eliezer Feleshi alimfungia dhamana Ponda na Mukadamu.

Hakimu Nongwa baada ya kusikiliza hoja za mawakili hao  alisema mshitakiwa anayepatikana na hatia katika kosa hilo la kuingia kwa jinai kwa mujibu wa kifungu cha 35 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya mwaka 2002 , mtu huyo atatakiwa afungwe jela miaka miwili, au faini au vyote viwili.

“Lakini kwa mazingira ya kesi hii mahakama hii imeamua kutumia kifungu cha 25(g) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu  na kwamba mahakama hii imeona Ponda amekaa gerezani muda mrefu na kwamba ni mara yake ya kwanza kutiwa hatiani hivyo  mahakama yake inamfunga kifungo cha nje cha mwaka mmoja, awe ni mtunza amani na mwenye tabia nje kwa kipindi chote hicho.

Hata hivyo hakimu Nongwa alisema inawezekana Ponda alitenda kosa hilo kwa nia njema,ila Ponda alivunja sheria katika kudai haki yake hivyo na kwamba Ponda akumbuke hakuna aliyejua ya sheria akaamuru askari wampeleke Ponda kujaza fomu za masharti hayo ya kuakisha atakuwa ni mtunza amani na mwenye tabia njema, ambapo Ponda alikwenda kujaza fomu hizo na kisha kuachiliwa huru.

Baada ya Ponda kuachiliwa huru wafuasi wake waliokuwa wametanda nje ya uzio wa mahakama hiyo na ndani, walilipuka kwa shangwe.Hata hivyo ulinzi ulikuwa umeimalishwa kwa farasi ,mbwa lakini hata hivyo hakuwepo na uvunjifu wowote wa amani.

Akizungumza na waandishi wa Habari Ponda alisema kilichofikiwa na mahakama ni haki yake na pia alikuwa na haki ya kuwa nje na pia imeonyesha jinsi vyombo vya dola vinavyoweza kupambikizia watu kesi na kwamba anapata fursa ya kushiriki katika masuala ya kijamii.

Oktoba 18 mwaka jana, ndiyo walifikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza wakikabiliwa na makosa hayo matano.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Mei 10 mwaka 2013.

No comments:

Powered by Blogger.