Header Ads

SERIKALI YAFUFUA KESI ILIYOFUTWA DHIDI YA 'MADILU'

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa mashtaka umemfungulia kesi mpya ya unyang’anyi wa kutumia silaha mtuhumiwa Ezekiel Matitu maarufu kwa jina la ‘Madilu” anayekabiliwa na kesi tano za kuwapora na kuwajeruhi wanawake wanaokodi teksi jijini Dar es Salaam.

Mwendesha mashtaka wa polisi, Kasoro Alfred, mbele ya hakimu Hadija Msongo wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu alidai kuwa wameamua kumfungilia kesi hiyo ambayo awali ilifutwa mwaka jana mahakamani hapo, chini ya kifungu cha 225 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ambacho kilitaka upelelezi wa kesi kukamilika ndani ya siku 60 tangu kesi ilipofikishwa mahakamani, kwa sababu polisi wamekamilisha upelelezi.

“Wakati kesi hii imefutwa polisi walitumia muda huo kukamilisha upelelezi na kwa sababu upelelezi umekamilika ndiyo maana leo tumeifungua upya kesi hii ambayo awali iliondolewa mahakamani hapa kwa sababu upelelezi ulikuwa haujakamilika kwa muda wa sheria unavyotaka” alisema Kasoro.

Alfred alidai kuwa Machi 8 mwaka jana saa nane mchana Mikocheni eneo la Rose Garden , mshtakiwa aliiba simu aina ya Nokia ,cheni ya dhahabu, fedha taslimu sh 700,000 na dola tano, vitu vyote hivyo vikiwa na thamani ya sh 984,000 mali ya Stumali Mzirai ambaye ni Mfanyakazi wa Hoteli ya New Afrika.

Kasoro aliiambia mahakama kwamba upelelezi umekamilika na kuomba apangiwe tarehe ya mshtakiwa kusomewa maelezo yake ya awali ambapo hakimu alitoa sharti la dhamana kwa kumtaka mshtakiwa kuwa na wadhamini wawili watakaotoa sh milioni moja na kuirisha kesi hiyo hadi Januri 26 mwaka huu, atakaposomewa maelezo ya awali.

Mshtakiwa alishindwa kutimiza masharti ya dhamana lakini hata kama angetimiza bado angeendelea kusota rumande kutokana na kesi nyingine zinazomkabili ikiwemo ya kumpora na kumjeruhi Balili Kasongo mahakamini hapo.

Alhamisi iliyopita shahidi huyo, F 2486 D/C Pius, katika kesi ya kumpora Balii Kasongo ,alidai mbele ya Hakimu Henzron Mwankenja kuwa mshtakiwa huyo ni mzoefu wa kufanya uhalifu huo kwa sababu anakabiliwa na kesi 11 za aina hiyo na kwamba kesi saba zimeondolewa mahakamani kutokana na mshtakiwa na washirika wake kuwapigia simu za vitisho wanawake hao waliowatendea uhalifu na kuwataka wasifike mahakamani kutoa ushahidi vinginevyo watawafanyia unyama wa kutisha,” alidai shahidi huyo.

Shahidi wa kwanza katika kesi hiyo, Balili Kasongo, ambaye aliporwa vitu mbalimbali vyenye thamani ya sh 1,140,000 alidai Januari mwaka jana, alipotoka Extelecom kuchukua dola 2,000 alizokuwa ametumiwa na ndugu yake, alikodi teksi ambayo ilikuwa imeegeshwa jirani na kutaka impeleke Ubungo.Alidai baada ya kufika Magomeni, dereva teksi alimweleza kuwa anaingia Sheli kuweka gari, lakini ghafla alimuona akipandisha vioo vya gari na kuwasiliana kwa simu na wenzake ambao baada ya muda mfupi walifika na kuwafungia milango. Shahidi huyo alidai miongoni mwa watu walioingia alikuwapo Madilu.

“Wakati dereva ananifanyia uhuni huo ndipo Madilu na mwenzake walianza kunipora cheni ya shingoni na mkononi, simu mbili za mkononi, pochi na dola 2000 huku Madilu akiendelea kunipiga vichwa kwenye paji la uso na kunichoma na bisibisi usoni,” alidai shahidi huyo.

Alidai licha ya mshtakiwa huyo kuwa rumande amekuwa akipokea simu za vitisho kutoka kwa mshtakiwa huyo akimtaka wakutane ampe fedha, ili asiende mahakamani kutoa usahidi.Katika kesi hiyo, mshtakiwa huyo na wenzake wawili wanadaiwa kuwa Januari 29 mwaka jana, walimuibia Kasongo cheni za dhahabu za mkononi na shingo, simu mbili za mkononi vitu vyote vikiwa na jumla ya sh 1,140,000 na kabla ya kuiba alimtishia kwa silaha za jadi na kumjeruhi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Januari 14 mwaka 2009

No comments:

Powered by Blogger.