Header Ads

SHAHIDI AMLIPUA NAIBU GAVANA

*Adai aliikingia kifua kampuni ya Maranda
*Adai waliwekewa bil. 1.8/- zimebaki 115,394/-

Na Happiness Katabazi

SHAHIDI wa pili katika kesi ya wizi wa sh bilioni 1.8 wa fedha za Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT), inayomkabili Farijala Hussein na Mweka Hazina wa CCM Mkoa wa Kigoma, Rajab Shaaban Maranda, ameieleza mahakama kuwa aliyekuwa Naibu Gavana, Juma Reli, ndiye alimweleza asitilie mashaka ingizo la fedha katika Kampuni ya Kiloloma & Brothers.
Shahidi huyo, Mkuu wa Kitengo cha Uendeshaji wa Huduma kwa wateja katika Commercial Bank of Africa ambayo awali ilikuwa ikiitwa United Bank of Africa, Ronald Manongi, alidai washtakiwa hao ni wateja wa benki yao, walifungua akaunti ya kampuni Agosti 31 mwaka 2005 na Septemba 2, mwaka huo huo na kisha akaunti hiyo iliingiziwa sh 1,864,949,294.45 na BoT.
Kiloloma & Brothers ni kampuni inayodaiwa kuchota fedha za EPA na shahidi wa kwanza katika kesi hiyo, Ofisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Estreriano Mahingira, alipotoa ushahidi wake juzi alikana kwamba kampuni hiyo haijawahi kusajiliwa na ofisi yake.
Akitoa ushahidi wake huku akiongozwa na Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface, shahidi huyo alidai akiwa Mkuu wa Kitengo cha Uendeshaji wa Huduma kwa wateja wa benki hiyo, alishtushwa na hali hiyo ya ingizo la fedha ambalo limeingizwa kwenye akaunti hiyo ambayo tangu ifunguliwe ilikuwa na siku mbili.

“Baada ya kuona fedha hizo zimeingia kwenye akaunti ya Kiloloma & Brothers nilifanya mambo mawili; kwanza nilitilia shaka hali hiyo na nikaandika taarifa ya shaka yangu kwa Kurugenzi ya Usimamizi wa Mabenki (BoT) na kuonyesha jinsi akaunti ya kampuni hiyo ilivyofunguliwa na kiasi hicho cha fedha kilivyoingia haraka kwenye akaunti hiyo,” alidai Manongi katika ushahidi wake.
Alidai barua yake ilijibiwa Septemba 25 mwaka 2005 na Naibu Gavana wa BoT, Juma Reli, ambaye mpaka sasa anashikilia wadhifa huo.
Sehemu ya barua hiyo inasomeka ‘Manongi taarifa yako mashaka kuhusu hali hiyo BoT imeipokea na tunakutoa wasiwasi kwamba kampuni hiyo inafanya kazi zake kihalali na ofisi yetu. Septemba 2, mwaka huo tuliingizia kiasi hicho, pia Agosti 17 mwaka huo huo, tuliingizia fedha kampuni ya Rashhaz (T) Ltd’.

Alieleza kuwa baada ya kupokea barua hiyo, aliwaandikia wateja wake (washtakiwa) barua, ili wamweleze hizo fedha zilizotoka BoT walipewa kwa ajili shughuli gani, watakuwa wakizitoa fedha kwenye akaunti yao kwa njia ya fedha taslimu au kuzituma nje ya nchi.
Manongi, alidai Septemba 26, mwaka 2005 wateja wake (washtakiwa) walijibu barua yake ya Septemba 19 mwaka huo huo, ambayo ilisainiwa na Rajabu Maranda ambayo ilieleza kwamba chanzo cha fedha hizo ni kibali cha kuruhusiwa na kampuni ya M/S BC Cars Export Ltd kudai deni lao.
Ifuatayo ni sehemu ya mahojiano kati ya Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface na Shahidi:
Wakili: Ieleze mahakama shughuli yako kubwa pale Benki ya Biashara ya Afrika?
Shahidi: Kuhakikisha benki yetu ina fedha za kutosha za kulipa wateja wetu, kusimamia idara ya huduma kwa wateja na kuhakikisha wateja wanapata huduma ipasavyo.
Wakili: Benki yenu ilianzishwa lini?
Shahidi: Mwaka 2002, wakati huo ilikuwa ikiitwa United Bank of Africa (UBA), lakini mwaka 2007 tulifanya mabadiliko ya jina na kwa sasa inatambulika kwa jina la Commercial Bank of Africa.
Wakili: Shahidi, hebu angalia hizo document zinaonyesha nini?
Shahidi: Zinaonyesha taratibu za kufungua akaunti.
Wakili: Hizo document mbili walipewa kina nani ?
Shahidi: Kiloloma & Brothers ambao ni Farijara na Maranda.
Wakili: Kuna mtu unamfahamu kati yao?
Shahidi: Namfahamu Farijara.
Wakili: Unamfahamu vipi?
Shahidi: Namfahamu katika uendeshaji wa Kiloloma & Brothers, alivyokuwa akija katika benki yetu na kuchukua fedha.
Wakili: Unaweza kumtambua hapa mahakamani amekaa upande gani?
Shahidi: Yule pale amekaa kushoto kizimbani na ndiye mshitakiwa wa kwanza katika kesi hii (alimnyooshea kidole).
Wakili: Fomu hii ya kuomba kufungua akaunti ina maelezo gani mengine?
Shahidi: Ina maelezo ya waombaji kuwa ni raia wa Tanzania, kampuni hiyo itaendeshwa na watu wawili ambao ni Farijala na Maranda.
Wakili: Huyu anayemtambulisha Kiloloma & Brothers kwa benki yenu ni nani?
Shahidi: Ni kampuni ya Rashhaz (T) Ltd.
Wakili: Benki yenu ina mahusiano gani Rashhaz (T) Ltd?
Shahidi: Rashhaz (T) Ltd walikuwa wamefungua akaunti kwenye benki yetu.
Wakili: Nani ni wamiliki wa Rashhaz (T) Ltd?
Shahidi: Kutokana na saini ya akaunti ya Rashhaz, kampuni hiyo inaonekana ni Rajabu Maranda.
Wakili: Hebu angalia fomu hii kwa makini inaonyesha Kampuni ya Kiloloma & Brothers nani ni wakurugenzi wake?
Shahidi: Farijara na Maranda.
Wakili: Fomu hiyo inaitwaje?
Shahidi: Deed of Partnership.
Wakili: Ifungue na uisome paragraph 4, inasemaje…soma kwa sauti.
Shahidi: Inasomeka kwamba Partners hao wamekubaliana kuanzisha ushirikiano kwa ajili ya kuanzisha biashara ya kuuza mafuta.
Wakili: Katika fomu hiyo fungua ukurasa wa nne, angalia paragraph ya 4.1, inasemaje?
Shahidi: Inasema partners hao watafanya biashara ya kuuza mafuta kwa pamoja kwa kutumia jina la Kiloloma & Brothers.
Wakili: Fomu hiyo ilikuja kwenye benki yenu?
Shahidi: Ilikuja kwenye idara yetu kufungua akaunti.
Wakili: Kitaalamu fomu hiyo inaitwaje?
Shahidi: Account Information.
Wakili: Hiyo fomu ukiiangalia imebeba taarifa gani?
Shahidi: Imebeba jina la Kiloloma & Brothers, P. o. Box 3983, Dar es Salaam. Pia inaonyesha aina ya akaunti waliyofungua kuwa ni Current Account, biashara ambayo inafanya na fomu hiyo ya kufungulia akaunti ya pamoja inaeleza Kiloloma & Brothers itafanya biashara ya kukusanya madeni na fomu hiyo ilijazwa na washtakiwa wote wawili.
Wakili: Umebaini kitu gani kipya baada ya kuzipitia hizo fomu mbili nilizokupatia hapa mahakamani?
Shahidi: Nimegundua majukumu mawili tofauti katika fomu hizi. Mosi, jukumu la kukusanya madeni na pili kuuza mafuta.
Wakili: Aina gani ya akaunti ilifunguliwa na Kilolomo & Brothers?
Shahidi: Current Account.
Wakili: Tutajie namba ya akaunti hiyo?
Shahidi: 0101305008.
Wakili: Baada ya akaunti hiyo kufunguliwa, wamiliki wa akaunti hiyo walipewa kitu gani na uongozi wa benki yenu?
Shahidi: Cheque Book na waliomba yenye leaf 25.
Wakili: Mbali na cheque book, kuna kitu kingine benki iliwapatia?
Shahidi: Nakumbuka ni hiyo cheque book ndiyo tuliwapatia.
Wakili: Hebu angalia hayo makabrasha ni kitu gani?
Shahidi: Ni statement of Account.
Wakili: Ya nani?
Shahidi: Kiloloma & Brothers.
Wakili: Kutoka benki gani?
Shahidi: Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) Ltd.
Wakili: Unapenda kutoa mahakamani itumike kama kielezo?
Shahidi : Ndiyo.
Wakili: Kampuni ya Kiloloma & Brothers ilifunguliwa rasmi tarehe ngapi?
Shahidi: Agosti 31, mwaka 2005.
Wakili: Wateja wako wakati wanafungua akaunti hiyo waliweka kiasi gani cha fedha?
Shahidi: Sh 500,000 tu kama walivyotakiwa na masharti ya benki siku hiyo.
Wakili: Baada ya hapo akaunti hiyo iliwahi kupata fedha?
Shahidi: Ndiyo, ilipata fedha toka BoT, Septemba 2, mwaka 2005.
Wakili: Kiasi gani hicho shahidi?
Shahidi: Sh 1,864,949,294.45.
Wakili: Hii fedha iliingia toka BoT kwa njia gani?
Shahidi: Kwa njia ya Telegraph Transfer (TT) toka BoT kuja kwenye akaunti ya Kilolomo & Brothers ambayo ipo kwenye benki yetu.
Wakili: Telegraph Transfer (TT) ni kitu gani hicho?
Shahidi: Ni njia ya utumaji fedha kwa kutumia Electronic.
Wakili: Zaidi ya hapo ilikuwaje?
Shahidi: Benki yetu wakati huo ikiitwa United Bank of Africa, ilipata barua toka BoT.
Wakili: Soma kwa sauti hiyo barua.
Shahidi: Ni barua ya Septemba 2 mwaka 2005 inakwenda kwa wakurugenzi wa Kilolomo & Brothers inayosomeka ‘out standing debt Uk pound 921,878.83 B.C Cars Exports Ltd ya Mumbai India.
Wakili: Barua hiyo ya BoT ilikuwa na ujumbe gani?
Shahidi: Ilikuwa na ujumbe kwamba BoT imeiingizia sh 1,864,949,294.45 kwenye akaunti ya kampuni hiyo iliyopo kwenye benki yetu.
Wakili: Hiyo barua ya BoT nakala yake alikuwa anapewa nani?
Shahidi: Mkurugenzi wa benki.
Wakili: Shahidi, hebu tuweke vizuri, Agosti 31, mwaka 2005 kampuni ilifunguliwa na Septemba 2 mwaka huo huo fedha hiyo iliingia, ulichukua hatua gani?
Shahidi: Mimi kama Mkuu wa Kitengo cha Uendeshaji, baada ya kuona fedha hizo zimeingia kwenye akaunti hiyo nilifanya mambo mawili.
Wakili: Yapi na yataje?
Shahidi: Kwanza nilitia shaka, nikaandika taarifa kwa Kurugenzi ya Usimamizi wa Mabenki nchini pale BoT na kueleza jinsi akaunti ilivyofunguliwa na kiasi cha fedha kilivyoingizwa haraka.
Wakili: BoT walikujibu hiyo taarifa ya mashaka yako?
Shahidi: Ndiyo walinijibu.
Wakili: Hiyo document ni ya nini?
Shahidi: Ni barua ya BoT kuja kwangu.
Wakili; Imeandikwa na nani hiyo barua?
Shahidi: Naibu Gavana.
Wakili: Inasemaje, soma tafadhari.
Shahidi: ‘Taarifa yako ya mashaka uliyoituma kwenye kurugenzi yetu tumeipokea na tunakutoa shaka usiitilie shaka Kampuni ya Kiloloma & Brothers kwani inafanya kazi zake kihalali na BoT ndiyo imewatumia fedha hizo’.
Wakili: Baada ya kupokea barua hiyo ya BoT ulifanya nini?
Shahidi: Sikuishia hapo niliwaandikia wateja hao barua ambao walinijibu wakisema chanzo cha fedha hizo ni realize of debt applied on behalf of principle M/S BC Cars Export Ltd.
Wakili: Ambayo ni nini kwa lugha nyepesi?
Shahidi: Kulipwa deni kwa niaba ya Principle wao ambao ni M/S BC Cars Export Ltd.
Wakili: Katika paraghraph ya barua hiyo waombaji wanasema wanafanya biashara gani?
Shahidi: Maranda anasema anafanyabiashara mpya ya kukusanya deni la kampuni ya nje ambapo deni hilo lipo Benki Kuu kwa miongo miwili.
Wakili: Eh Katika paragraph 4,3,2 isome taratibu ukiwa umetulia ili mahakama isikie?
Shahidi: Katika paragraph hiyo kushuka chini Maranda ananijibu wana kibali maalumu cha kutumia sehemu ya fedha iliyolipwa na BoT kutokana na makubaliano yao na Principle wao M/S BC Cars Exports Ltd na kwamba makubaliano yao yapo Benki Kuu.
Wakili: Soma pia paragraph ya 2 kutoka chini, katika barua ya washtakiwa hawa.
Shahidi: Imeeleza kampuni yao ni entitled katika fedha zilizolipwa na kamisheni hiyo imeidhinishwa na principle wao. Huo ndiyo ujumbe uliopo katika hiyo paragraph.
Wakili: Uliangalia kielelezo cha tano na kielelezo hiki cha saba, unasemaje?
Shahidi: Vinaonyesha walikubaliana na BoT kufanya hivyo na nikaruhusu akaunti yao iendelee kufanya kazi.
Wakili: Iambie mahakama Septemba 2 mwaka 2005 kulitokea nini kwenye akaunti ya washtakiwa?
Shahidi: Siku hiyo fedha iliingia kwenye akaunti na siku hiyo hiyo walitoa sh milioni 30.
Wakili: Septemba 5, mwaka huo, kulitokea nini kwenye akaunti hiyo?
Shahidi: Kulikuwa na cash withdraw fomu ya sh milioni 150 toka kwenye akaunti hiyo ya Kiloloma & Brothers.
Wakili: Hiyo cash draw form nani aliyeidhinisha kampuni hiyo ichukue fedha?
Shahidi: Mimi, kwa sababu nilikuwa Mkuu wa Kitengo.
Wakili: Nani aliombwa walipwe hiyo fedha?
Shahidi: Farijara na Maranda.
Wakili: Septemba 13 mwaka 2005 akaunti hiyo ya Kiloloma ilitokea nini?
Shahidi: Kampuni hiyo ilichukua cash milioni 100 kwa kutumia cheque book ya kampuni yao.
Wakili: Hebu taja namba ya cheque book ya kampuni hiyo?
Shahidi: 062352.
Wakili: Na Septemba 14 mwaka huo, akaunti hiyo ilikumbana na nini tena?
Shahidi: Hawa partners waliiomba benki yetu iwapatie Bankers Cheque.
Wakili: Kazi yake nini?
Shahidi: Ina thamani ya siku ile ile katika mabenki hapa nchini tofauti na cheque za watu binafsi. Na cheque bank ukitumia unaweza kulipwa siku hiyo hiyo. Walitupatia hundi namba 062353 tukawapatia cheque bank yenye namba 029421 iliyokuwa ikilipwa kwa Maranda na tulimlipa sh 284,700,000.
Wakili: Septemba 15 mwaka huo, kilitokea nini kwenye akaunti ya wateja hao?
Shahidi: Kiloloma walifanya cash with draw tena ya sh milioni 300 kwa njia ya hundi ya kampuni yao yenye namba 062354.
Wakili: Nani alikuwa akichukua hizo fedha?
Shahidi: Kiloloma & Brothers.
Wakili: Eh Septemba 28 mwaka huo kilitokea nini tena kwenye akaunti hiyo?
Shahidi: Kampuni hiyo kwa mara nyingine ilifanya cash with draw ya sh milioni 100.
Wakili: Kwa cheki namba ngapi?
Shahidi: Kwa hundi ya kampuni yao namba 0623550.
Wakili: Oktoba 7 mwaka mwaka huu huo, ni kilitokea kwenye akaunti ya wateja wako?
Shahidi: Walifanya tena cash withdraw ya sh milioni 20 kwa hundi ya kampuni yenye namba 062356.
Wakili: Shahidi usichoke, iambie mahakama Oktoba 19 mwaka huo huo tena nini kilitokea kwenye akaunti hiyo?
Shahidi: Kampuni hiyo ilituma fedha nje ya nchi kwa kutumia TT, paundi 200,000 kwenda kwa B.C Cars Export Ltd yenye akaunti HSBC United Kingdom. Na pamoja kutuma hela hiyo nje ya nchi walichukua sh milioni 100.
Wakili: Kitu gani kilitokea Oktoba 21 mwaka kwenye akaunti hiyo?
Shahidi: Walichukua tena cash withdraw sh milioni 45 na walichukua kupitia hundi ya kampuni yao yenye namba 062358.
Wakili: Oktoba 24 mwaka huo huo, kilitokea nini kwenye akaunti yao?
Shahidi: Vilitokea vitu viwili kwenye akaunti hiyo, mosi, walituma nje paundi elfu 150 kwenye kwa B.C Cars ya UK na jambo la pili Kiloloma & Brothers walinunua dola elfu 10 yenye jumla ya sh milioni 11.5 na walinunua kwenye benki yetu hizo dola na walitueleza wamefikia uamuzi wao kwa sababu hawana akaunti ya fedha za kigeni.
Wakili: Turudi nyuma kidogo ile paundi elfu 150 iliyotumwa kwa kampuni ya nje ina thamani kwa kwa fedha ya Tanzania?
Shahidi: 308,700,000.
Wakili: Desemba 6 mwaka 2005 nini kilitokea kwenye akaunti hiyo?
Shahidi: Walichukua tena cash withdraw milioni 5.2 kupitia hundi ya kampuni yao yenye namba 062360.
Wakili: Baada ya tarehe hiyo kumbukumbu zako zinasemaje kuna maagizo au matoleo katika akaunti hiyo?
Shahidi: Kumbukumbu zinanionyesha hakuna utoaji fedha hadi Novemba 8 mwaka 2006 alihamisha sh 41, 920 kwenda kwenye akaunti yao nyingine ya fedha za kigeni dola yenye namba 0101305019.
Wakili: Unasema hii akaunti ya kigeni ni ya nani vile?
Shahidi: Kiloloma & Brothers.
Wakili: Baada ya hapo.
Shahidi: Hakuna uhamisho wa fedha uliofanywa na wateja hao katika akaunti yao.
Wakili: Mbali na sh bilioni 1.8 zilizoingizwa na BoT kwenye akaunti hiyo, kuna fedha yoyote iliwahi kuingia kwenye akaunti hiyo?
Shahidi: Haijawahi kuingia fedha yoyote hadi sasa.
Wakili: Mpaka leo hii akaunti ya wateja hao ina akiba ya kiasi gani?
Shahidi: Ina akiba ya sh 115,394.94 tu.
Baada ya wakili Boniface kumaliza kumhoji shahidi, Hakimu Cypriana William alimtaka wakili wa utetezi Majura Magafu, aanze kumhoji shahidi.
Hata hivyo, Wakili Magafu alidai hawezi kumhoji shahidi huyo kwa sababu hana nyaraka za kibenki zilizotumiwa na Boniface, hivyo kuomba kesi iahirishwe hadi leo, ili upande wa serikali umpatie nyaraka hizo.

Hakimu William, ambaye ni Naibu Mwenyekiti wa Mahakama Kuu Divisheni ya Kazi, pia anasaidiana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Phocus Bambikya na Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Saul Kinemela kuendesha kesi hiyo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Januari 29 mwaka 2009

No comments:

Powered by Blogger.