Header Ads

SHAHIDI BRELA ATOBOA SIRI

Na Happiness Katabazi

SHAHIDI wa pili katika kesi ya wizi wa sh milioni 207 katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) mali ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Naibu Msajili wa Brela, Andrew Mkapa, ameiambia mahakama kuwa ofisi yake iligundua Kampuni ya Rashhaz (T) Ltd haikuwasilisha ripoti ya marejesho ya kila mwaka baada ya vyombo vya habari kulivalia njuga sakata la EPA.

Akitoa ushahidi huo mbele ya Hakimu Mkuu Mfawidhi, Addy Lyamuya, shahidi huyo alidai licha ya ofisi yake kuisajili kampuni hiyo, haijawahi kupitia faili la kampuni hiyo kuona kama ilikuwa ikiwasilisha ripoti ya mahesabu ya kila mwaka (Annual Report).

“Tuligundua kampuni hii haijawasilisha ripoti hiyo baada ya vyombo vya habari kulivalia njuga sakata la EPA, ndipo tuliitisha majalada ya makampuni yote, ili tuweze kuyapitia, lakini kabla hatujafikia kulikagua jalada la kampuni ya Rashhaz (T) Ltd, DPP na Takukuru walifika ofisini na kuondoka na baadhi ya majalada likiwemo jalada la kampuni hiyo,” alieleza shahidi huyo.

Ifuatayo ni sehemu ya mahojiano kati ya wakili Majura Magafu na Mkapa:

Wakili: Katika ushahidi ulioutoa jana(juzi) ulisema kampuni hiyo ilisajiliwa kihalali?
Shahidi: Ndiyo
Wakili: Ulisema miongoni mwa mahusiano kati ya Brela na makampuni baada ya kusajiliwa ni kampuni husika kuwasilisha Annual Report?
Shahidi: Ni kweli
Wakili: Kwa mujibu wa sheria za ofisi yenu Annual Return zinatokana na nini?
Shahidi: Inatokana taarifa za kampuni na zinapaswa kuambatana na vitu vitatu kwanza kuna fomu ya kujaza Annual Return, jina la kampuni, mahali ilipo ofisi, wahusika na anwani ya posta, fomu hiyo inapaswa kuambatanishwa na taarifa ya Mkaguzi wa Mahesabu na taarifa ya hasara na faida iliyopata kampuni kwa mwaka.
Wakili: Katika ushahidi wako uliieleza mahakama kwamba kampuni hiyo haijawahi kuwasilisha Annual Return tangu iliposajiliwa Septemba 12 mwaka 2003 . Je ni utaratibu gani unachukuliwa na Brela wakati kampuni inaposhindwa kuwasilisha taarifa hiyo?
Shahidi: Msajili anapogundua hilo, kwamba kampuni imefanya hivyo anaiandikia barua ya kuwakumbusha ni kwa nini hawawasilishi Annual Return.
Wakili: Kwa mujibu wa kumbukumbu zenu lini mligundua kampuni ya Rashhaz haijawasilisha hiyo ripoti?
Shahidi: Tuligundua pale kizaazaa cha EPA kilipopamba moto kwenye vyombo vya habari na ndipo maofisa wa ofisi yetu waliitisha majalada ya makampuni kwa ajili ya kuanza kuyakagua.
Wakili: Ilikuwa lini?
Shahidi: Novemba mwaka 2007
Wakili: Huoni kwamba Brela hampo makini na kazi yenu?
Shahidi: Tatizo ofisi yetu inatumia muundo wa zamani wa kuhifadhi mafaili badala ya kutumia teknolojia ya kompyuta, hivyo inatuwia vigumu kupitia mafaili yote kwa wakati mmoja kwa sababu mafaili ni mengi mno, lakini pia hiyo tutaichukulia kama ni changamoto kwetu.
Wakili: Mliwaandikia barua wakurugenzi wa kampuni hiyo, ili waweze kuwasilisha Annual Return?
Shahidi: Hatukuweza kuwaandikia kwa sababu hayo majalada ambayo tulipanga tuanze kuyakagua yaliitishwa haraka na DPP, Eliezer Feleshi na Takukuru.
Wakili: Je, DPP na Takukuru wameisharudisha majalada hayo Brela?
Shahidi: Hadi leo ninavyotoa ushahidi bado hayajarudishwa.
Wakili: Hivi kampuni isiyoleta ripoti ya marejesho ya kila mwaka, Brela mnaichukulia imetenda kosa lipi kisheria?
Shahidi: Tunachukulia ni kosa la jinai linaloweza kumfikisha mhusika mahakamani.
Wakili: Je, hilo kosa la jinai limeainishwa kwenye Sheria ya Kanuni ya Adhabu au sheria ya makampuni?
Shahidi: Kosa hilo limeainishwa kwenye sheria ya makampuni.
Wakili: Ni adhabu zipi zimeanishwa kwa mtu anapokuwa na hatia?
Shahidi: Faini kwenye hiyo sheria ili mhusika akileta hiyo ripoti anapigwa penati.
Wakili: Kwa unavyoelewa kampuni hiyo imeshawahi kuburuzwa mahakamani?
Shahidi: Hapana.
Wakili: Unakubaliana na mimi kwamba kampuni hiyo ni halali?
Shahidi: Ndiyo, lakini ni kampuni iliyolala.
Wakili: Katika madhumini 27 yaliyoainisha makubaliano ya awali kati ya kampuni hiyo na ofisi yenu; kuna madhumuni yanayoonyesha kuwa kampuni hiyo itakuwa na jukumu la kukusanya madeni?
Shaihidi: Kweli, yameainisha.
Wakili: Katika makubaliano hayo ya awali hakuna kifungu kilichoonyesha kampuni hiyo inaweza kuingia mkataba na serikali au kampuni yoyote?
Shahidi: Kuna kipengele kinaonyesha kampuni hiyo inaruhusiwa kukusanya madeni.

Baada ya shahidi huyo kumaliza kutoa ushaidi wake, Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface, aliiomba mahakama iairishe kesi hiyo hadi Jumatatu, kwani jana wameshindwa kuleta mashahidi.

“Tunaomba shauri hili liairishwe kwani mashahidi hawajaweza kufika leo lakini hata hivyo Summon tuliyowapa ilikuwa ikionyesha tarehe za mbele si ya leo (jana) kuja kutoa ushahidi, hivyo wametafutwa leo (jana) alfajiri hawakuweza kupatikana, ila tunaahidi Jumatatu watafika na kutoa ushahidi,” alieleza Stanslaus Boniface.

Ombi ambalo lilikubaliwa na Hakimu Lyamuya na kuairisha shauri hilo hadi Jumatatu.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Januari 24 mwaka 2009

No comments:

Powered by Blogger.