Header Ads

MAHAKAMA YARUHUSU MKUTANO TLP KESHO

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, jana iliruhusu uchaguzi wa kumchagua Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), ufanyike kama ulivyopangwa.

Amri hiyo ilitolewa jana jioni na Jaji Geofrey Shaidi baada ya kusikiliza ombi la mwanachama wa chama hicho, Stanley Ndamugoba, anayetetewa na wakili Alex Makulilo, dhidi ya Baraza la Udhamini la TLP, linalotetewa na Desidely Ndibalema.

Kwa mujibu wa hati ya madai, mwombaji alifungua kesi ya madai na kuwasilisha maombi hayo ya zuio la muda juzi na katika ombi hilo, aliomba mahakama hiyo itoe amri ya kuzuia kufanyika kwa mkutano mkuu wa TLP, unaotarajiwa kufanyika kesho.

Jaji Shaidi alisema baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili za kuhusu kukubali au kutokubaliwa kwa ombi hilo, amebaini kuwa ombi la mlalamikaji halina msingi, kwa sababu mkutano utakaofanyika kesho, tayari chama kilishatumia gharama kuuandaa.

“Kwa sababu hiyo, nalitupa ombi la mwombaji na ninaagiza uchaguzi huo ufanyike kama ulivyopangwa na kesi ya msingi iliyopo mahakamani, itaendelea pindi mtakapopewa tarehe,” alisema Jaji Shaidi na kufanya umati wa wanachama waliokuwa wakiongozwa na Mwenyekiti wa TLP anayemaliza muda wake, Augustine Mrema, kuripuka kwa shangwe.

Awali, wakili wa mwombaji, Makulilo aliwasilisha hoja ya kutaka uchaguzi huo uzuiwe hadi kesi ya msingi iliyopo mahakamani itakapomalizika.

Akijibu hoja hizo, wakili wa utetezi, Ndibalema, alidai ombi hilo halina msingi wa kisheria kwa kuwa limeletwa chini ya kifungu kisicho sahihi cha Sheria ya Madai, kwani hakiiruhusu mahakama kutoa amri zilizoombwa na mlalamikaji.

Ndibalema aliendelea kudai kuwa, hata hivyo mlalamikaji si mwanachama wa TLP na kwamba kadi yake ya uanachama imeghushiwa na katika kumbukumbu za chama, hazionyeshi kama waliwahi kuwa na mwanachama mwenye jina hilo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, April 25, 2009

No comments:

Powered by Blogger.