Header Ads

UMEME WAKWAMISHA KESI YA EPA

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, jana ilishindwa kuendelea kusikiliza ushahidi katika kesi ya wizi wa sh milioni 207 wa fedha za Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) inayomkabili Mweka Hazina wa CCM Mkoa wa Kigoma, Rajabu Matanda na wenzake watatu kutokana na kukatika kwa umeme.

Hakimu Mkuu Mkazi wa mahakama hiyo, Addy Lyamuya, jana alialazimika kuahirisha kesi hiyo baada ya kukatika umeme wakati shahidi wa kwanza wa upande wa mashitaka katika kesi hiyo, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, Sifael Mkonyi, alipokuwa akitoa ushahidi wake.

Alisema analazimika kuahirisha kesi kwa kuwa mwenendo wa kesi hiyo hautaweza kurekodiwa kutokana na kukatika kwa umeme.

Awali akitoa ushahidi wake, Mkonyi aliyekuwa akiongozwa na Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface, alidai alimfahamu Maranda Machi 7 mwaka jana alipofika katika Ofisi ya Kikosi Kazi Mikocheni na kumchukua malezo yake.

Alidai alifuata taratibu zote wakati akichukua maelezo ya Maranda na kuiomba mahakama ipokee maelezo hayo kama kielelezo katika kesi hiyo.

Hata hivyo, ombi hilo lilipingwa na Wakili wa utetezi, Magura Magafu, kutoyapokea maelezo hayo kwa sababu katika maelezo hayo kuna sehemu inayomtaka mshitakiwa asaini pindi anapomaliza kuchukuliwa maelezo yake, lakini mteja wake hakusaini.

Wakati Magafu akiendelea kupinga suala hilo ndipo umeme ulikatika, hali iliyomlazimu Hakimu Lyamuya kuahirisha kesi hiyo.

Mbali na Maranda, washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni Farijala Hussein na maofisa wa BoT, Iman Mwakosya, Ester Komu na Bosco Kimela.


Hii ni mara ya pili kwa kesi hiyo kuairishwa kutokana na kukatika kwa umeme.

Maofisa wa mahakama wakizungumza na Tanzania Daima kwa masharti ya kutotajwa majina, walisema hata wao wanakerwa na uongozi wa mahakama kushindwa kufunga jenereta katika mahakama hiyo hasa ikizingatiwa kuwa ni mahakama kubwa na inapokea kesi mbalimbali.

“Hii ni aibu na uongozi wa mahakama unapaswa utambue hiki ni chombo cha serikali ambacho kipo kwa ajili ya kutoa huduma mbalimbali kwa wananchi wake…..yaani huko mitaani saluni zina jenereta, lakini mahakama kama hii haina ni aibu kwa kweli,” alisema mmoja wa maofisa hao.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, April 25, 2009

No comments:

Powered by Blogger.