Header Ads

JWTZ HUU SIYO UUNGWANA

Na Happiness Katabazi

JESHI la Ulinzi katika nchi yoyote ile ni chombo maarufu na nyeti katika masuala ya ulinzi na usalama, mtu anayefanya vitendo vya kishujaa hupewa taswira ya jeshi.

Heshima hiyo iliyonayo Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) ilijengwa zaidi na ukakamavu, nidhamu na uwezo mkubwa wa utendaji wake wa kazi ndani na nje ya mipaka ya nchi.

Panapotokea maafa, mara nyingi tegemeo kubwa la raia ni jeshi lao la ulinzi, kwa kuwa wanajeshi wa jeshi hilo ndio wenye sifa, maarifa, mbinu na vifaa vya kuokoa maisha ya watu au mali zao. Uwajibikaji wao katika maafa kumewafanya wapendwe na wananchi.

Uhuni uliofanywa na askari wa JWTZ mapema wiki hii katika Makutano ya barabara za Morogoro na,Mandela na Sam Nujoma,dhidi ya askari wa Usalama wa Barabarani (Trafiki), Sajini Thomas Mayapila.

Kwa kile eti walichokidai kucheleweshwa na Trafiki huyo aliyekuwa akiongoza magari katika eneo hilo maarufu kama Ubungo Mataa.

Lakini tayari JWTZ imeshatoa taarifa kwa umma kuwa tayari limemkamata Koplo Steven Sagana kwa kuhusika na kosa la kuongoza kufanya uhuni huo na kwamba Jeshi la Polisi nchini limeishaunda timu ya pamoja kuchunguza na kubaini undani wa mazingira ya tukio hilo.

Hata hivyo kuundwa kwa timu hiyo na kukamatwa kwa Kolo Sagana, hakutuzui kulijadili kwa kina tukio hilo la kishenzi ambalo linaendelea kuweka rekodi mbaya kwa JWTZ ya kuwa baadhi ya wajeshi wake wamekuwa ni vinara wa kuvunja sheria za nchi kwa kujiona wapo juu ya sheria.

Tukio hilo limetudhihirishia kuwa jeshi letu bado lina wanajeshi wasio na nidhamu, kwa sababu hata kama wangekuwa wamegadhabika kwa kitendo cha kucheleweshwa bado suluhisho lake si kumvamia na kumpiga Trafiki huyo tena mbele ya hadhara.

Kitendo kile kinashiria kukosekana kwa busara kwa wanajeshi wale waliovaa sare wakiwa kwenye magari yao, niwape jina gani linalostahili kwa kufanya uvunjaji wa amani, kujeruhi na kunajisi sheria za nchi ambazo Amir Jeshi Mkuu wanayemtii, Rais Jakaya Kikwete anazitii?

Sasa hawa ndio mashujaa kweli wa nchi yetu? Labda suala zima la wanajeshi kutoka kambini na kuvamia raia kwa visingizio mbalimbali, kama vile ujambazi na kunyang’anyana ‘mabibi’ na raia vimekuwa vikilaaniwa mara kwa mara na taasisi za kutetea haki za binadamu nchini.

tabia waliyoionyesha imeonyesha jinsi wasivyo na heshima kwa askari polisi na raia. Kwani nini hawataki kuthamini na kutii majukumu ya idara nyingine za serikali?

Septemba 15,2007, alipokula kiapo cha utii mbele ya Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, Rais Jakaya Kikwete, Mkuu wa Jeshi la Ulinzi, Jenerali Davis Mwamunyange, ambapo mimi nilishuhudia tukio hilo na nikapata fursa ya kupiga naye picha ya kumbukumbu, alishutumu na kulaani vikali tabia ya wanajeshi kupiga raia na akaahidi kwamba uongozi wake utaikomesha.

Kwa kuwa chini ya uongozi Jenerali Mwamunyange tayari kumeisharipotiwa matukio kuwa baadhi ya vijana wake wanaendelea kwenda kinyume naye kwa kujichukulia sheria mkononi.

Februali mwaka jana wanajeshi walivamia ofisi za shirika la ugavi wa maji Dar es salaam (Dawasco) linalomilikiwa na serikali, na kuwapiga na kuwanyanyasa watendaji wa shirika hilo na kumpora kamera mwandishi mmoja wa habari.

walitenda tukio hilo baada ya watendaji wa Dawasco kuingia katika moja ya kambi ya JWTZ na kukata maji kwa sababu jeshi hilo lilikuwa ni miongoni mwa wadaiwa sugu.

Ili wananchi waendelee kumheshimu, kumuamini na kutolinganisha kauli yake hiyo na porojo za wanasiasa majukwaani, tunamtaka Jenerali Mwamunyange atetee heshima ya JWTZ.

Tunataka atuthibitishie kwamba wanajeshi wetu si genge la wahuni wanaochukua sheria mikononi . Ikiwa atashindwa kufanya hivyo, raia watashindwa kumuamini na kuiheshimu JWTZ.Sote tuna fahamu kuwa serikali ya awamu ya nne imetia fora kwa kuunda tume pindi jambo linapotokea, tume hizo zimekuwa zikiendeshwa kwa kodi zetu.

Uundwaji wa tume hizo ni kama vile mpango wa serikali kufuja mali za wananchi ambao hulipa kodi nyingi bila ya kuwapo kwa maendeleo waliyoyatarajia.

Kuna sababu gani ya kuunda tume kwa tukio hili la ubungo wakati kila kitu kimefanyika hadharani na watu wameshuhudia? Kwa nini tusiwakamate moja kwa moja waliohusika mpaka tuunguze fedha za wananchi?

Je tume hiyo kweli itaweza kuja na matokeo huru na ya haki ambayo hayatakuwa na chembe chembe za upendeleo kwa tukio ambalo halikuhitaji tume?.

Wananchi tuna wasiwasi mkubwa na utendaji wa hiyo tume kwa kuwa tuna uzoefu mkubwa wa makosa wanayoyafanya wanajeshi huku uraiani kama vile kupiga raia lakini mwisho wa siku hatuwaoni mahakamani, tume zilizoundwa zilifanya kazi gani?

Tabia ya wanajeshi kulindana ndiyo inasababisha baadhi ya wanajeshi wetu kuendelea kukomaa kwa tabia za utovu wa nidhamu kwa kuwapiga raia kwa kisingizio kuwa ‘mwanajeshi ndiye mwenye nchi na kwamba kazi yao ni muhimu mno kuliko kazi nyingine zote’.

Ieleweke wazi kuwa kila kazi ina umuhimu wake katika maendeleo ya taifa letu hivyo hata muuza machungwa,mfagia barabara na mzibua vyoo ni muhimu pia.Kwani bila raia hakuna jeshi cha msingi wale wote wanaojichukulia sheria mkononi wadhibitiwe.

Hata kama trafiki yule hakutoa uzito wa ombi la wanajeshi wale waliosema wanakwenda kuwahi operesheni maalum bado kutoa kipigo si uungwana hata kidogo.

Kitendo kile kilikuwa na nia ya kilidhalilisha jeshi la polisi na askari husika ili lionekana si kitu mbele ya JWTZ, si wangewasiliana na mkuu wa kazi wa trafiki yule?


Kama Wanajeshi wale walikuwa wamebeba vifaa maalum ambavyo havikuhitaji kusubiri foleni, kwa nini uongozi wa JWTZ usingewasiliana mapema na Mkuu wa Trafiki Mkoa husika kwamba watumia barabara kadhaa kusafirisha vifaa hivyo nyeti bila kupata usumbufu?

Wananchi wanaokwenda asubuhi kazini ni mashahidi wa vitendo vya uvunjaji wa sheria za barabarani vinavyofanywa na madereva wa JWTZ huku wakiwa wamewapakia ambao bila shaka nao ni vinara wa kuchochea uvunjaji wa sheria.

Wamekuwa vinara wa kukwepa foleni kwa kupita kwenye barabara za waenda kwa miguu wakiulizwa hutoa kisingizo kwamba wakati wote mwanajeshi yupo kazini.

Nategemea kama kweli jeshi linajali utu na uungwana litatoa aelezo ya kuridhisha na ikiwezekana kuomba radhi kwa tukio hilo la ‘kihuni’
Lisilopendeza machoni mwa jamii iliyostaarabika.

Kama wasipofanya hivyo basi Tanzania itakuwa imejijengea utamaduni ambao majeshi yake ni ‘miungu watu’ wanaoweza kufanya udhalimu wa aina yoyote dhidi ya haki na uhai wa raia bila kukanywa wala kudhibitiwa.

Tutakuwa tunajijengea jehenamu ya aina yake na Tanzania haitakuwa tofauti na kambi za Al Ghareb, Iraq au Guantanamo Bay, Cuba.Tukubali makosa, tukubali kusahihishwa na kama taifa tumrejee Mungu kama wimbo wetu wa taifa wa taifa unavyotuasa.

JWTZ itimize wajibu wake wa kulinda nchi na si kupiga raia wala Trafiki. Trafiki fanyeni kazi bila upendeleo na epukeni ufisadi licha miongoni mwenu mmekuwa mkituhumiwa kuomba rushwa. Hata hivyo kipigo ulichokipata Sajini Thomas Mayapila,na Trafiki wenzako kisiwakatishe tamaa, pole sana na jenga taifa lako bila woga.

Mungu ibariki Tanzania Mungu Ibariki Afrika

0716 774494

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili, Mei 24, 2009

No comments:

Powered by Blogger.