Header Ads

WEZI WA NMB WASOMEWA MASHITAKA 209

Na Happiness Katabazi

WATU watatu, jana walipandishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam na kusomewa mashitaka 209 kwa tuhuma za kuiba sh bilioni moja kwa njia ya mtandao wa kompyuta, mali Benki ya National Microfinance Bank (NMB).

Washitakiwa hao ni karani wa benki hiyo, Mtoro Midole (42), Daudi Kindamba (47) na John Kikopa (46), ambao wote ni wafanyabiashara na wakazi wa jijini Dar es Salaam.

Mbele ya Hakimu Mkazi, Nyigumalila Mwaseba, ilidaiwa na wakili wa serikali E. Njau, kuwa kati ya mwaka 2007 hadi 2009 katika tarehe tofauti, washitakiwa hao pamoja na wengine ambao hawapo mahakamani, walitenda makosa ya kula njama, kughushi na kuiibia NMB na kusaidia wafanyabiashara hao kuibia benki hiyo.

Njau alidai kuwa, Midole akiwa mtumishi wa NMB Makao Makuu, aliwasaidia washitakiwa kuiibia benki hiyo sh 1,018,759,883.64.

Hata hivyo washitakiwa hao, walikana mashitaka hayo na wamepelekwa rumande baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana.

Katika dhamana yao, walitakiwa kutoa nusu ya kiwango cha fedha wanachotuhumiwa kuiba au hati ya mali yenye thamani hiyo.

Mbali na NMB kukumbwa na wizi wa aina hiyo, pia wizi kama huo ulishawahi kuzitikisa benki za CRDB na Barclays.

Watu wanaokabiliwa na kesi ya wizi wa namna hiyo Barclays, katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, ni Mkurugenzi Mtendaji wa Dar es Salaam Cement Muslim na mfanyabiashara maarufu nchini, Merey Ally Saleh maarufu kwa jina la Merey Balhabou na Meneja Mwendeshaji wa Kigamboni Oil Co. Ltd, Abdallah Said Abdallah.

Wengine ni wafanyakazi wa benki hiyo, Winford Mwang’onda, Shubira Mutungi, Naima Saria, Upendo Mushi, Magreth Longway, Emmanuel Mukoni na Ramadhani Khamis, ambao wanadaiwa kuiibia Barclays dola za Kimarekani milioni 1.8 (sawa na sh bilioni 2.4).

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Mei 5,2009

No comments:

Powered by Blogger.