Header Ads

LALA SALAMA KESI YA ZOMBE

* Korti yafunga ushahidi wa washitakiwa
* Aliyekuwa mshitakiwa amtetea mwenzake

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imefunga ushahidi wa utetezi katika kesi ya mauaji ya wafanyabiashara watatu na dereva teksi mmoja, inayomkabili aliyekuwa Kamanda wa Upelelezi Mkoa wa Dar es Salaam (ACP), Abdallah Zombe na wenzake.

Mahakama hiyo imefunga ushahidi huo, baada ya mashahidi wawili wa washitakiwa wa pili na 13 kumaliza kutoa ushahidi wao jana.

Baada ya mashahidi hao kutoa ushahidi wao, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Salum Massati, alisema hatua inayofuata katika kesi hiyo leo ni kwa pande zote mbili kuwasilisha hoja za majumuisho ya ushahidi.

“Kwa sababu upande wa utetezi nao umefunga ushahidi, naahirisha kesi hii hadi kesho (leo), ambapo pande zote zitakuja kutoa hoja za majumuisho ya ushahidi uliotolewa na upande wa utetezi,” alisema Jaji Massati.

Aidha, katika hali isiyotarajiwa, jana Zombe mara kwa mara alionekana akijifuta machozi wakati shahidi wa mshitakiwa 13, Koplo Morris Nyangelela alipokuwa akitoa ushahidi wake.

Nyangelela ambaye awali alikuwa mshitakiwa katika kesi hiyo na baadaye kuachiwa huru, alidai Januari 15, mwaka 2006 waliitwa ofisini kwa Zombe na kupewa mkono wa pongezi kwa kazi nzuri ya kuwaua majambazi.

Alidai askari kupewa mkono wa pongezi ni jambo la kawaida kwa kuwa taarifa za matukio ya uhalifu huanzia kwa askari wa chini na kisha kupelekwa kwa askari wa vyeo vya juu.

Alidai Januari 15, mwaka 2006, akiwa askari polisi wa kituo cha Chuo Kikuu, walipokea taarifa ya kuwapo kwa tukio la uhalifu Barabara ya Sam Nujoma, hivyo yeye na askari wenzake walikwenda eneo la tukio na kukuta lori la Bidco.

Alieleza walipowahoji walielezwa kwamba wameporwa sh milioni tano na kabla ya kuporwa walitishiwa kwa bastola na majambazi waliokuwa wakitumia gari aina ya saloon nyeupe.

Kwa upande wake, shahidi wa mshitakiwa wa pili, DE4595 Koplo Jumanne Mussa (42) kutoka Kituo cha Polisi Oysterbay, jana alijikanyaga alipokuwa akitoa utetezi wake, hali iliyowafanya mawakili wa serikali kumuuliza maswali ya kumtilia shaka kwamba alikuwa amekwenda mahakamani hapo kutoa ushahidi wa uongo.

Mussa akitoa ushahidi wake alidai kuwa, Januari 14, 2006 alimpeleka mshitakiwa wa pili, Christopher Bageni kwenye grocery iliyopo Kijitonyama ambayo ilikuwa imevamiwa na majambazi na kwamba waliwachukua majeruhi na kuwapeleka Hospitali ya Mwananyamala.

Kauli hiyo ilimfanya Wakili wa Serikali, Angaza Mwipopo kuuliza maswali kadhaa ambayo alionekana kushindwa kuyajibu na hata alipopewa kumbukumbu za Jeshi la Polisi azisome alikataa kufanya hivyo.

Hata hivyo, Wakili Mwipopo alidai kwa mujibu wa kumbukumbu za Jeshi la Polisi, siku hiyo ulinzi 122 ambayo ni Bageni, hakufika eneo hilo na aliyefika alikuwa ulinzi 121 (Mkuu wa Kituo cha Polisi Oysterbay).

Bageni wakati akijitetea aliiambia mahakama siku hiyo alikuwa shambani kwake Pugu na kwamba simu na redio call zilikuwa hazipatikani kwani mawasiliano yalikuwa mabovu na kwamba tukio hilo la uhalifu wa Sinza alilipata kupitia redio call.

Mbali ya Zombe, washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni SP Christopher Bageni, SP Ahmed Makelle, Jane Andrew, Emmanuel Mabula, Michael Shonza, Koplo Abeneth Saro, Rajabu Bakari na Festus Gwasabi.

Zombe na wenzake, wanadaiwa kufanya mauaji hayo Januari 14 mwaka 2006, eneo la Mbezi Luis, katika msitu wa Pande, ambapo waliwaua, Ephraim Chigumbi, Sabinus Chigumbi na Mathias Lukombe, ambao ni wafanyabiashara wa madini kutoka Mahenge, Ulanga na Juma Ndugu, ambaye ni dereva teksi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi,Mei 7,2009

No comments:

Powered by Blogger.