Header Ads

WASHITAKIWA WIZI OFISI YA DPP WAONGEZEKA

Na Happiness Katabazi

IDADI ya washtakiwa wa wizi wa gari na kompyuta, mali ya Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) inazidi kuongezeka kutokana na mshtakiwa mwingine kufikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam.

Mshtakiwa huyo Abubakari Kamugisha (31) ambaye ni mfanyabiashara na mkazi wa Kinyerezi, jijini, alifikishwa mahakamani hapo mwishoni mwa wiki na kusomewa shtaka la wizi wa kutumia silaha.

Kuongezwa kwa mshtakiwa huyo katika kesi hiyo kunafanya idadi ya washtakiwa wanaokabiliwa na tuhuma hizo kufikia 12.

Akisomewa mashtaka hayo na Inspekta Emma Mkonyi alidai Machi 5, Tabata Liwiti CCM, Kamugisha aliiba gari STK 5002 Toyota Hiace modeli mpya lenye thamani ya sh 56,972,000, komyuta sita zenye thamani ya sh 4,250,000, printa zenye thamani ya sh 7,435,000, seti ya UPS, laptop na vitabu vya sheria mali ya ofisi ya DPP na vitu vyote hivyo vikiwa na jumla ya thamani ya sh 111,500,000.

Alidai kwamba kabla ya kuiba vitu hivyo alimtishia kwa bunduki Alfa Makamba, mlinzi wa gereji ambayo gari hilo lilikuwa limelazwa.

Mshtakiwa alikana tuhuma hizo mbele ya Hakimu Mkazi, Eva Nkya, na kupelekwa rumande kuwa kesi hiyo haina dhamana kisheria.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni dereva ofisi ya DPP, Ally Ramadhani Mustapha, Haji Mwanga, Bakari Makara, Deogratus Coster, Philipo Jose, Athony Mengi, Mary Lyimo, Jacob Mosha, Wilfred Maleko, Alex Kimario na Hajat Faraji Kileo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Mei 19, 2009

No comments:

Powered by Blogger.