Header Ads

TUMEDHITI HATI ZA KUGHUSHI-DPP

Na Happiness Katabazi

OFISI ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini(DPP) imesema tangu waendesha mashtaka wa kiraia waanze kuendesha kesi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imeweza kudhibiti tatizo sugu la hati za dhamana feki mahakamani hapo.

Mafanikio hayo yalielezwa na Naibu Mkurugenzi wa Mashtaka nchini, Winfrida Koroso kwaniaba ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP)Eliezer Feleshi mbele ya Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe, ambaye jana alifanyaziara katika mahakama hiyo kwaajili ya kuzungumza na mahakimu wakazi na mawakili wa serikali sambamba kusikiliza mafanikio na changamoto zinazowakabili watendaji wa mahakama hiyo kwa ujumla.

Naibu Mkurugenzi wa Mashtaka,Koroso alisema mawakili hao ambao wanatoka katika ofisi yake walianza kufanyakazi Septemba mosi mwaka jana, na kwamba tangu waanze kufanyakazi hiyo ambayo awali ilikuwa ikifanywa na Waendesha Mashtaka toka Jeshi la Polisi wameweza kukabiliana na wimbi la wadhamini wanaowasilisha hati za mali zisizoamishika ambazo ni za kugushiwa ili waweze kuwadhamini ndugu na jamaa zao na nyaraka nyingine za kipelelezi.

Koroso alisema mafanikio hayo yametokana na mawakili hao wa kiraia kushirikiana na kikamilifu na Jeshi la Polisi ambapo wameweza kuzibaini hati nyingi kuwa ni za kughushiwa. Akitaja mafanikio mengine tangu mfumo huo uanze kufanyakazi alisema umewezesha kuboresha uendeshaji mashtaka ,kwani kabla ya mawakili kuanza kazi kulikuwa na mafaili ya kesi 800 yalilikuwa hayaonekani lakini tangu wameanza kufanyakazi mafaili hayo yamepatikana.

“Hata hivyo mchakato huo pia umeleta mafaniko kwani umeweza kupanua wigo wa uwazi katika kesi mbalimbali kwani katika mahakama tumeanzisha kitengo cha kupokea malalamiko ya wananchi wenye kesi zao mahakamani ambao wanaona hawatendewi haki….pia mchakato huu umeweza kututunganisha na wadau ambao ni Polisi, Takukuru na mahakama” alisema Koroso.

Hata hivyo alisema changamoto zinazowakabili ni kukosekana kwa majarada ya kesi, mahabusu kushindwa kutimiza masharti ya dhamana na kwamba vyumba vya waendesha mashtaka katika mahakamani hapo havitoshi hivyo kumuomba Waziri Chikawe awasaidie kutatua tatizo hilo.

Wakichangia mada kwenye mkutano huo, Hakimu Mkazi Henzron Mwankenja, Waliarwande Lema, Mkuu wa Waendesha Mashtaka Kanda ya Dar es Salaam, (ACP) Charles Kenyela walipongeza mfumo huo wa waendeshamashtaka wa kiraia ila walishauri pia bado kuna haja waendesha mashtaka wa polisi waongezewe muda ili waweze kuwapatia uzoefu waendesha mashtaka wa kiraia kwani ni wazi kabisa waendesha mashtaka wa kirai bado hawajapata uzoefu wa kutosha katika kuendesha kesi mbalimbali.

Kwa upande wake Kenyela alisema alisema hali ya ulinzi na usalama katika mahakama hiyo ni finyu kwani hata askari polisi wanaolinda mahakamani hapo hawana vifaa vya kisasa vya kuweza kukabiliana na wahalifu ambao wanaweza kufika mahakamani hapo na visu au mabomu hivyo kuomba mamlaka husika liangalie ni jinsi gani linaweza kutenga fedha kwaajili ya kuweka mfumo ulinzi wa kisasa mahakamani hapo.

‘Ebu fikiria askari wangu wanavirungu tu na bastola wakati mwingine ndiyo wanalinda hapa mahakamani lakini lazima tukubali wahalifu hivi sasa nao kila kukicha nao wanafanya uhalifu wao kisayansi…..atuombei mabaya leo hii mhalifu aje na bomu kaficha au kisu askari wangu hawawezi kumtambua hivyo basi mahakama iwekewe uzio na geti moja ambapo kila anayeingia na kutoka anapekuliwa na kifaa maalum naamini tutakabiliana na hali hiyo” alisema Kenyela huku akionyesha kujiamini.

Kwa upande wake Waziri Chikawe alisema amesikilia maelezo ya waliochangia na kusema ameteembelea mahakama hiyo amejionea kuwa mahakama hiyo ipo katika hali mbaya na kwamba imechoka na akamwelekeza Hakimu Mkuu Mfawidhi wa mahakama hiyo, Addy Lyamuya kushirikiana na mtaalum toka wizarani yake ambapo watampa mchoro wa jinsi wanavyotaka mahakama hiyo ijengwe.

Chakawe hata hivyo alionekana kuguswa na tatizo la upatikanaji wa mashahidi na jinsi ya kuwatunza , alisema tatizo hilo ni kubwa na kuongeza kuwa ndiyo maana wameamua kuamishia mashahidi wa kesi mbalimbali katika ofisi ya DPP kwasababu ofisi hiyo ndiyo inayowahitaji mashahidi na tayari serikali imekusudia kutoa fungu kwenye ofisi ya DPP kwaajili ya mashahidi.

“Nimesikiliza matatizo yenu na pia napongeza ofisi ya DPP kwa mafanikio mliyoyapata ila haya matatizo nitayapeleka kwa wakubwa wenzangu ili tuone tunatumia utaratibu upi kuyapatia ufumbuzi” alisema Chikawe.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumanne, Mei 26,2009

No comments:

Powered by Blogger.