Header Ads

MARANDA NA WENZAKE WAONGEZEWA MASHITAKA

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa mashitaka katika kesi nyingine ya wizi wa sh bilioni 2.2, fedha za Akaunti ya Madeni ya Nje katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT), inayomkabili kada wa (CCM), Rajabu Maranda na mpwa wake, Farijara Hussein, jana ulibadilisha hati ya mashitaka, baada ya kuongezwa mashitaka mawili.

Mwanasheria wa serikali, Oswald Tibabyekoma, aliyekuwa akisaidiwa na wanasheria waandamizi wa serikali, Fredrick Manyanda, Michael Lwena na Cedrick Ephery, mbele ya mahakimu wakazi wanaoongozwa na Fatma Masengi, Benedect Mlingwa na Catherine Revocate, ulidai kuwa umefikia uamuzi huo wa kubadilisha hati ya mashitaka baada ya kuongeza shitaka moja la kula njama na kubadilisha shitaka moja.

Tibabyekoma alidai shitaka linalobadilishwa ni shitaka la tano ambalo lilikuwa ni shitaka mbadala la sita, ambapo sasa shitaka hilo litajitegemea.

Hati hiyo ya mashitaka sasa itakuwa na jumla ya mashitaka saba tofauti na awali ambapo ilikuwa na mashitaka sita.

Baada ya kubadilishwa kwa hati ya mashitaka, washitakiwa walisomewa maelezo ya awali, ambapo ilidaiwa kuwa washitakiwa wote kati ya Machi na Desemba 2005, walikula njama, kuiba, kughushi, kuwasilisha hati za uongo, kujipatia ingizo na kuibia BoT sh bilioni 2.2 kwa kuonyesha hati zinaonyesha kutolewa na ofisi ya Wakala wa Usajili wa makampuni, (BRELA) kwamba wao ni wakurugenzi wa Kampuni ya Money Planers Consultant na Kampuni ya B. Grancel ya Ujerumani imeipatia idhini kampuni yao kukusanya deni la fedha za Kijerumani 3,137,488.40 ambazo ni sawa na sh bilioni 2.2.

Washitakiwa hao wanaotetewa na wakili wa kujitegemea Majura Magafu, walikana mashitaka yote na kiongozi wa jopo la mahakimu wanaosikiliza kesi hiyo, Masengi, aliiahirisha hadi Juni 16, mwaka huu, ambapo itakuja kwa ajili ya kutajwa na kwamba itaanza kusikilizwa rasmi Julai mosi mwaka huu.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Mei 20, 2009

No comments:

Powered by Blogger.