Header Ads

KWA NINI TUSIWE WAKWELI JUU YA MAJANGA?

Na Happiness Katabazi

“UHURU kwa wengi unamaanisha uhakika wa maisha, hata kama ni kwa kutumia uchawi.Isipokuwa kama sitakutana na baadhi ya mambo ya kunitia moyo, msaada wangu utapungua na kichwa changu kitazunguka kama vile ndege anavyomfuata Kifaru.”

Maneno hayo yaliwahi kutamkwa na Baba wa Taifa letu, Julius Kambarage Nyerere alipokuwa akizungumzia umuhimu na raha ya uhuru.

Ikumbukwe kuwa April 29 mwaka huu, kwenye maghala ya silaha ya Kambi ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi (JWTZ) Mbagala, mabomu yalilipuka na kusababisha maafa makubwa ikiwemo watu kupoteza maisha, kujeruhiwa na makazi ya watu kuharibika jambo liliowafanya baadhi ya yao kuhifadhiwa katika kambi maalumu.

Nimelazimika kuitumia nukuu ya Hayati Nyerere katika makala yangu ya leo kwa sababu baadhi ya Watanzania waishio Mbagala na vitongoji jiji la Dar es Salaam, kwa kiasi kikubwa hivi sasa wamekumbwa na wasiwasi mkubwa usalama wao na mali wanaozimiliki.

Wananchi hao hawana uhuru kama ilivyokuwa kabla ya kutokea kwa milipuko hiyo, hawawezi kufanya shughuli zao za kuwaingizia vipato kwa ufanisi.


Kama ilivyo desturi ya serikali yetu mara kwa mara imekuwa na tabia ya kutoa kauli za kutatanisha na zenye kuwafariji wananchi pindi linapotokea tatizo lakini hujua walisemalo si hilo walitekelezalo au kulipanga.

Tabia hii hivi sasa inaonekana kuanza kuota mizizi miongoni mwa viongozi na nina hakika ipo siku watakuja kuumbuka baada ya ukweli kubainika.

Kuna mambo mengi tu ambayo kauli zao zimewaumbua lakini wameshindwa au hawataki kujifunza kutokana na makosa waliyoyafanya ama kwa kiburi au hofu waliyonayo.

Desturi hiyo ya kipuuzi pia iliendelea kutamalaki baada ya tukio hilo kutokea kwa viongozi wetu kutoa kauli za aina hiyo.

Sote tunakumbuka tamko la Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, William Lukuvi, alivyowataka wakazi wa Mbagala warejee katika maeneo yao kwa kuwa uongozi wa JWTZ umemdhibitishia eneo hilo ni salama na wameshadhibiti ulipukaji wa mabomu hayo.

Mapema wiki hii, Mnadhimu Mkuu wa JWTZ, Luteni Jenerali Abdulrahman Shimbo alinukuliwa akiwataka wananchi kutohofia operesheni inayoendelea ya uteketezaji mabomu katika kambi ya Mbagala, aliwataka wananchi kutohofu operesheni hiyo kwa kuwa ni sehemu ya jeshi hilo kusafisha mabomu hayo baada ya mlipuko wa April 29.

Ni jambo lilo wazi kuwa kulingana na mazingira yaliyopo hivi sasa hali si shwari katika eneo hilo licha ya baadhi ya viongozi wetu sasa wamejigeuza kuwa wahudumu wa afya ambao nao miongoni mwao wamekuwa wakitoa kauli za kuwafariji wagonjwa ambao wengine wana hatua mbaya kwa kuwaambia watapona haraka lakini wakijua fika hawasemi ukweli

Hivi tunamdanganya nani katika hili kama siyo kutaka wananchi wenzetu waendelee kuumia na mwisho wa siku serikali itajikuta inatumia fedha zaidi za walipa kodi kwa ajili ya kuwatibia majeruhi wapya wa milipuko hiyo hiyo?

Au serikali yetu inaona raha wananchi wasio na hatia wanavyoanguka na kupoteza fahamu pamoja na kuvuta hewa mbaya ya mabomu pindi yanapolipuka?

Kwanini serikali isione haja ya kutafuta maeneo ya wazi mbali kabisa na maeneo ya Mbagala na kujenga kambi za muda kwa ajili ya kuwahifadhi waathirika na wale ambao bado hawajaathirika na milipuko hiyo, ili JWTZ iweze kulipua mabomu yake kwa nafasi hadi itakapomaliza kufanya kazi hiyo ndipo wananchi ambao nyumba zao hazijaathirika warejee kwenye maeneo yao?

Haingii akilini kwamba serikali yetu yenye watalaamu na wasomi lukuki kuridhia kambi za muda za kuhifadhia wahanga hao kujengwa katika eneo ambalo tayari lilikwisha athirika na milipuko hiyo.

Serikali yetu ina maeneo mengi ya wazi lakini cha kushangaza imeamua kuridhia kujengwa kwa kambi katika eneo hilo.Sote tunafahamu suala hilo ni la dharula lakini bora tuokoe afya na uhai wa watu kwani Katiba ya Nchi inasema kila mtu ana haki ya kuishi na serikali ina jukumu la kulinda mali na usalama wa raia wao.

Endapo serikali itafanyia mzaha jambo hili na mabomu yakaendelea kulipuka na wananchi wakendelea kuumia, siku za usoni, serikali isije ikahamaki pale wananchi watakapojitokeza kwa wingi katika mahakama zetu kufungua kesi dhidi ya Jeshi la Polisi, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, wakitaka walipwe fidia ya mabilioni kwa kile watakachokidai kuwa wamepoteza kuibiwa mali zao, wamepoteza baadhi ya viungo vyao.

Hatupendi tufike huko, naiomba serikali yetu ifikirie upya na kuwahamisha wakazi waishioo eneo hilo mpaka pale hali itakapokuwa salama kweli badala ya salama ya kauli za viongozi ambazo sasa zinaelekea kuywakwaza wananchi

Tusisigane katika hili wala kunyosheana vidole wanaoumia ni Watanzania wenzetu na wanaoteseka zaidi ni wanawake na watoto hivyo nasisitiza kufanywa kwa jitihada za haraka kuwanusuru na adha ya milipuko hiyo.

Inasikitisha mpaka sasa hakuna hata mtaalamu mmoja aliyejitokeza hadharani kutuambia kuwa vishindo na moshi ule wa mabomu vina madhara gani, lakini naamini ipo siku waliokumbwa na vitu vyote hivyo viwili watajitokeza na kuweka bayana walivyoathirika.

Mungu ibariki Tanzania,Mungu ibariki Afrika

0716 774496

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumapili, Mei 17, 2009

No comments:

Powered by Blogger.