Header Ads

MJUMBE WA NEC CCM MATATANI

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kitengo cha Biashara jijini Dar es Salaam, imemwamuru mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (CCM), Ramadhani Madabida na wadaiwa wengine wanne kulipa zaidi ya sh milioni 699 walizojipatia kama mkopo kutoka Benki ya Stanbic jijini Dar es Salaam.

Uamuzi huo ulitolewa hivi karibuni na Jaji Frederick Werema, ambaye alisema amefikia uamuzi huo baada ya kuridhishwa na hoja na ushahidi uliotolewa na mlalamikaji, Dilip Kesaria na Meneja wa benki hiyo, Charles Daniel.

Kwa mujibu wa nakala ya hukumu hiyo, wadaiwa wengine mbali na Madabida ambao nao wametiwa hatiani baada ya kushindwa kurejesha sh 699,860,717 kama mkopo walioupata kutoka kwa benki hiyo ni Kampuni ya Pharmaceutical Investment, Mpewani Trading, Global Trading na Mkurugenzi wa Kampuni ya Pharmaceutical, Salum Shamte.

Jaji Werema alisema mbali ya kuwaamuru wadaiwa hao kurejesha mkopo huo, pia amewaamuru walipe fidia ya asilimia 15 kwa mwaka, kuanzia Septemba mosi 2007 hadi Mei 22, mwaka huu, ambapo hukumu hiyo ilitolewa, na asilimia saba tangu siku ya kutolewa kwa hukumu.

Aidha, Jaji Werema amemtaka Madabida na mwenzake kulipa gharama za uendeshaji wa kesi hiyo kwa Benki ya Stanbic, ambaye ndiye mlalamikaji katika kesi hiyo.

Ilidaiwa kuwa Benki ya Stanibic katika shughuli zake za kibenki ilitoa mkopo kwenye Kampuni ya Pharmaceutical na baada ya Madabida na wenzake kuweka dhamana (guarantee). Hadi kufikia Oktoba 31, 2003 deni lilifikia sh 1,110,444,611 na baadaye kupunguzwa na kufikia sh 971,861,074/-.

“Pamoja na hayo, benki ilipunguza tena deni hilo na kufikia sh milioni 800 Mei 2004 . Na kwakuwa Kampuni ya Pharmaceutical haikuwa na uwezo wa kulipa deni hilo, benki ilipunguza tena deni hilo na kufikia sh milioni 529 ambazo zingelipwa kwa miezi 24, ambapo kila mwezi wadaiwa wangelipa sh 25,649,436 pamoja na faida.

Hata hivyo, wadaiwa walishindwa kurejesha deni hilo, hali iliyosababisha benki kutoa taarifa kadhaa za kuwakumbusha wadaiwa kulipa deni hilo na ilipofika Agosti mosi 2007 deni lilifikia sh 699,807,717, jambo ambalo liliilazimu benki hiyo kufungua kesi katika mahakama hiyo.

Katika hukumu yake, Jaji Werema alisema ameridhishwa na ushahidi uliotolewa mahakamani hapo kuwa Benki ya Stanibic ilitoa mkopo kwa Kampuni ya Pharmaceutical, hivyo kutokubaliana na wadaiwa, ambapo Madabiba na wadaiwa wengine walipinga vikali kuhusika na deni hilo.

“Baada ya kupitia kwa hoja na ushahidi uliotolewa na pande mbili katika kesi hii nimebaini kuwa kulikuwepo na majadiliano kadhaa kati ya pande zote mbili, ambapo nyaraka zilizoletwa mbele yangu zimebainisha kuwapo kwa mkopo ambao ulipunguzwa na kufikia sh milioni 529, ambazo zingelipwa kwa kipindi cha miezi 24.

Aidha, Jaji Werema alisema katika nyaraka hizo zimeonyesha makubaliano ambayo yalisainiwa na Madabida kama Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Pharmaceutical ambayo ndiyo ilikuwa mkopaji mkuu na pia Madabida alisaini kama Mkurugenzi na mtoa dhamana (guarantor) wakati Shamte na mkewe Madabida anayeitwa Zarina Madabida, ambaye ni Mwenyekiti wa UWT-CCM Mkoa wa Dar es Salaam, ambao wote ni wakurugenzi wa kampuni hiyo walisaini kama watoa dhamana (guarantors).

Kwenye utetezi wao, wadaiwa kupitia Madabida walikana kuhusika na deni hilo na badala yake alidai benki ndiyo iliyopaswa kumlipa fidia ya dola za Marekani 105,000, ambazo alitozwa na Medical Store Department (MSD), baada ya benki hiyo kuchelewa kufungua kile alichokiita Local Letters of Credit.

Alidai kuwa Kampuni ya Pharmaceutical iliingia mkataba na MSD ya kusambaza au kuwapatia dawa mbalimbali za thamani ya dola za Marekani milioni 5.1, ambazo wangeziagiza kutoka nje ya nchi na kwa kuwa kampuni hiyo haikuwa na mtaji wa kutosha, iliiomba MSD ifungue hiyo Local Letters of Credit ambapo wangeitumia kufungua kile alichokiita ‘Slave Letters of Credit’.

Madabida aliiambia mahakama kuwa MDS ilitimiza utaratibu huo mwaka 1997 lakini Benki ya Stanbic ilikataa utaratibu huo na baadaye kubadili uamuzi wake na kuikubalia MSD kufungua hiyo Local Letters of Credit mwaka mmoja baadaye na hivyo kuchelewesha usambazaji wa dawa hizo, kitendo kilichoigharimu kampuni na kutozwa kiasi hicho cha pesa kama fidia.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatatu, Juni 1, 2009

No comments:

Powered by Blogger.