Header Ads

KORTI YAAMURU USHAHIDI KESI YA MRAMBA UANIKWE

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imeamuru upande wa mashitaka katika kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 11.7, inayomkabili aliyekuwa Waziri wa Fedha, Basil Mramba na wenzake, kuanika ushahidi na vielelezo watakavyovitumia.

Mbali na Mramba, washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni Daniel Yona, aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini na Katibu Mkuu mstaafu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Grey Mgonja.

Uamuzi huo ulitolewa jana na jopo la mahakimu wakazi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, wanaongozwa na John Utamwa anayesaidiana na Saul Kinemela na Fatma Masengi, ambao walisema wamefikia uamuzi huo, kwani matakwa ya kisheria yanataka upande wa utetezi upate fursa ya kufahamu na kuelewa vielelezo na ushahidi utakaotumika katika kesi inayowakabili.

Akisoma uamuzi wake jana, Hakimu Utamwa, alisema hoja ya upande wa utetezi ya kutaka kupatiwa nyaraka za vielelezo kabla ya wateja wao kusomewa maelezo ya awali si muhimu, bali upande wa mashitaka unapaswa kuanika nyaraka hizo, vielelezo vitakavyotumika katika kesi hiyo.

Akiendelea kusoma uamuzi wake alisema hoja ya upande wa utetezi iliyowasilishwa Jumatatu wiki hii na Profesa Leonard Shaidi ya kutaka kupatiwa nyaraka za vielelezo kabla ya wajeta wao kusomewa maelezo ya awali, alisema hilo siyo la muhimu.

‘Hoja ya upande wa utetezi yakutaka wapatiwe nyaraka nyaraka zitakazotumiwa na upande wa mashtaka katika kesi hii siyo muhimu, cha muhimu hapa ni upande wa mashtaka uanike nyaraka hizo,vielelezo na waakikishe upande wa utetezi unazielewa hizo nyaraka” alisema Utamwa.

Utamwa alisema anaairisha kesi hiyo hadi Juni 19 mwaka huu, ambapo itakuja kwaajili ya kutajwa na pia itaanza kusikilizwa rasmi Julai 20-24 mwaka huu, na kutaka upande wa mashtaka ulete mashahidi wake.

Hata hivyo alimruhusu Mramba kwenda kwenye shughuli za kibunge nje ya Dar es Salaam, kuanzia Mei 24-Agosti 25 mwaka huu, nakuongeza kuwa endapo Mramba ataitajika mahakamani atalazimika kusitisha shughuli za kibunge na kuja kuudhulia kesi yake mahakamani.

Jumatatu wiki hii,upande wa mashitaka katika kesi hiyo ulibadilisha hati ya mashitaka baada ya kufutwa kwa shitaka moja.

Shitaka lililofutwa, linamhusu Mramba peke yake, hivyo anabaki na mashitaka 11 badala ya 12.

Shitaka hilo la tano, awali lilikuwa likisomeka kuwa, Oktoba 10, 2003, mshitakiwa huyo (Mramba), akiwa Waziri wa Fedha, alitumia madaraka yake vibaya kwa kudharau mapendekezo ya Mamlaka ya Mapato (TRA) ambayo yalikataza Kampuni ya M/S Alex Stewart (Assayers) Government Bussiness Corporation, isipewe msamaha wa kodi.

Baada ya ombi hilo kuridhiwa na jopo hilo la mahakimu, upande wa mashitaka uliiomba mahakama iwaruhusu kuwasomea upya maelezo ya awali washitakiwa, ombi ambalo lilizua malumbano makali ya kisheria kati ya upande wa mashitaka na wakili wa upande wa utetezi, Profesa Leonard Shaidi.

Profesa Shahidi ambaye alikuwa akisaidiana na Hurbet Nyange na Joseph Tadayo, walipinga ombi hilo wakidai kuwa hawapo radhi wateja wao wasomewe maelezo ya awali bila upande wa mashitaka kuwapatia nyaraka walizopanga kuzitumia kwenye kesi hiyo.

“Waheshimiwa mahakimu, kabla ya upande wa mashitaka kuwasomea wateja wetu maelezo ya awali, tunaomba watupatie nyaraka walizopanga kuzitumia kwenye kesi hii kwa sababu sheria inataka hivyo, kwa hiyo tunaomba mahakama iwaamuru kufanya hivyo,” alidai Profesa Shaidi.

Akijibu pingamizi hilo, Boniface alidai si lazima kisheria upande wa mashitaka utoe nyaraka hizo kwa upande wa utetezi.

Malumbano hayo ambayo yalidumu kwa takribani robo saa, yalisababisha kiongozi wa jopo hilo la mahakimu wakazi, Utamwa, kuahirisha kesi hiyo hadi Alhamisi wiki hii ambapo mahakama itatoa uamuzi kuhusu pingamizi hilo.

Aprili 17, mwaka huu, Mramba ambaye ni mshitakiwa wa kwanza katika kesi hiyo, kupitia wakili wake, Nyange mbele ya Hakimu Mkazi, Henzron Mwankenja, alikiri kutoa vibali vya msamaha wa kodi kwa kampuni hiyo na kwamba alifanya hivyo baada ya kuagizwa na Ikulu.

Awali, akisoma maelezo ya awali dhidi ya washitakiwa hao, mwanasheria wa Takukuru, Joseph Holle alidai kuwa washitakiwa hao wakiwa na nyadhifa hizo serikalini, walikuwa na jukumu la kuwa waaminifu na makini katika majukumu waliyokabidhiwa kisheria.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Mei 22, 2009

No comments:

Powered by Blogger.