Header Ads

RAUNDI YA KWANZA LIYUMBA KIDEDEA,DOLA IMEJIFUNZA NINI?

Na Happiness Katabazi

VITA ya dhidi ya ufisadi vilianza kwa kishindi.Kwa kishindo hicho hicho vita ya ufisadi itaisha kwani.Kwani ni ufisadi mtupu na usanii mtupu.


Sheria ya TAKUKURU ya 2006 ilitungwa kwa shinikizo la wafadhili, serikali iliburuzwa miguu kwa miaka kadhaa lakini hatimaye ilisalimu amri pale wafadhali walipotishia kuwa hawatatoa mikopo, misaada katika nchi ambazo hazitaaonyesha nia ya kupambana na rushwa(ufisadi sasa), dawa za kulevya na ugaidi.

Tanzania ilisalimu amri moja kwa moja ikatunga sheria ya Ugaidi ambayo ni kinyume kabisa na haki za binadamu na ikatunga sheria ya rushwa iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2006 ambayo inatumika hivi sasa.

Kwahiyo serikali yetu haikuwa na nia ya dhati ya kupambana na majanga hayo, sheria hizo zilitungwa kishabiki,kishikaji na kisanii.

Mawazo ya wananchi ya kutaka ziundwe taasisi huru ya kijamii zenye uwezo wa kupambana na majanga hayo ziligonga mwamba hiovyo nleo hii sheria hizo hazimgusi rais na makamu wake, ,rais wa Zanzibar na Waziri Mkuu.

Hivyo ikiwa rais ni gaidi au ikiwa rais ni fisadi hakuna njia ya kumdhibiti.Taasisi ya Takukuru ni mbwa asiye na meno mbele ya viongozi hao.

Vivyo hivyo sheria za nchi kama ile ya Kanuni ya Adhabu(Penal Code),hazikubadilishwa kuunda dhana na makosa mapya yanayoendana na hali halisi ya majanga hayo yakiwemo wizi wa kutumia mitandao.

Hata neno ufisadi ulikuti katika sheria hizo.Sasa kesi zilizofunguliwa dhidi ya watuhumiwa wa ufisadi na zitakazofunguliwa zitajikuta hazina mguu wa kusimama kisheria.

Hivyo Watanzania wasije kushangaa watuhumiwa kwa kesi za aina hiyo wakiachiwa huru kwa makosa ya kiufundi yaliyofanywa au yatakayofanywa na mawakili wa serikali bila hata kujibu kesi zenyewe.

Hii inatufanya tuamini kwamba baadhi ya watuhumiwa walipelekwa mahakamani kiusanii tu ili kukidhi haja ya kuwwarisha wafadhali kwamba serikali ya awamu ya nne ni makini ni shupavu katika vita dhidi ya rushwa,ufisadi,dawa za kulevya na ugaidi.

Ndiyo maana Rais wetu Jakaya Kikwete sasa ni rais bora wa Afrika ana haki ya kukaribishwa Ikulu ya Marekani,Ikulu ya Elysee-Ufaransa ,Ikulu ya Uingereza Buck Gham , kwasababu huyu sasa ni shujaa wa Afrika katika vita dhidi ya ufisadi ,ugaidi na dawa za kulevya.

Haijalishi kwamba ukweli usiopingika ni kwamba aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala(BoT) Amatus Liyumba na Meneja Mradi wa benki hiyo, Deogratius Kweka waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya jinai namba 27/2009 iliyokuwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Alhamisi wiki hii, walishinda mzunguko wa kwanza katika vita hivyo vya ufisadi dhidi ya Serikali, baada ya mahakama hiyo kuwaachilia huru baada ya kubaini hati ya mashtaka imekosewa.

Haijalishi kwamba mtandao wa dawa za kulevya umeongezeka na Mafisadi Papa wanaotumia vijana wetu kusafirisha dawa hizo ndani na nje ya nchi hawajakamatwa.


Jeshi la Polisi wanawajua,Rais alisema anawajua hao mafisadi papa wa dawa za kulevya.Je tuseme kwamba hawa ni ndege wa mabawa yanayofanana na hivyo wanaruka pamoja?

Hiki kimya cha kuficha mapapa wa dawa za kulevya serikali ya awamu ya nne imekipata wapi?

Rais wetu alivyoingia madarakani alitutangazia kuwa ana orodha ya mapapa hao na kuwa angewataja na wangeshughulikiwa, mbona ajamtaja hata mmoja?

Wasiwasi wetu mkubwa ni kwamba Liyumba ,anayedaiwa kuwa ni marehemu ambaye alikuwa ni Gavana wa BoT, Daud Balali, Danile Yona, Basil Mramba,Gray Mgonja na wale wote ambao wanatuhumiwa kwa kashfa za ufisadi ambazo zipo kesi mahakamani au hazipo mahakamani wanaoenekana ni watu wa serikali na wanachama wa Chama cha Mapinduzi(CCM).

Rais Kikwete na serikali yake na chama chake hawana haja ya kuomba tena kuchaguliwa ikiwa hawataweza kulimaliza hili sakata la ufisadi.

Lakini Watanzania tujiulize pia kama ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG)inayoongozwa na Johnson Mwanyika na ile ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP)inayoongozwa na Eliezer Feleshi zimejipanga inavyostahili kupambana na ufisadi unaotishia ulinzi na usalama wa dola hivi sasa?

Kilichojionyesha katika kuachiliwa huru kwa Liyumba na kisha kukamatwa kwa muda mfupi na Alhamisi kufunguliwa kesi upya, ni udhaifu katika taaluma ya uendeshaji mashtaka kwa mujibu wa Sheria za Jinai.

Pamoja na kwamba mawakili wa serikali wanaoendesha kesi hizo waandamizi,inadhiirika kwamba taaluma yao kisheria haitoshi.

Je hii siyo ishara mbaya katika kesi zote za matumuzi mabaya ya ofisi za umma na wizi wa EPA zilizopo mahakamani hivi sasa?

Je hivi sasa si kweli kuwa mafisadi ambao hawajafikishwa mahakamani kujibu tuhuma za kashfa ya ununuzi wa Rada, ndege ya rais, , helkopta za JWTZ, Kagoda, Kiwira,Meremeta,Tangold, wanasherehekea na kugonganisha glasi zao za mvinyo?

Tayari upande wa serikali katika baadhi ya kesi zilizopo katika Mahakama ya Kisutu kwa sisi ambao siku tano za juma tunashinda hapo ,tumeshuhudia wameonyesha kubabaika kwa kubadilishabalisha hati za mashtaka kwa kuongeza au kupunguza mashtaka.

Je itakapotekea watuhumiwa wa kuachiriwa huru si kesi zitakuwa zimekwisha kwa kishindo kile kile kama zilivyofunguliwa kwa kishindo?

Tuseme nini sasa.usanii mtupu au ufisadi mtupu unaofanywa na mawakili wetu wa serikali?

Kama mawakili wa serikali hawana taaluma ya kutosha kwanini wasiombe ushirikiano wa kitaalum toka kwa mawakili wengine wenye ujuzi ambao mawakili wengine binafsi walikuwa walimu wenu vyuoni?

Serikali sasa iache uchoyo na ukiritimba katika mambo ya kitaaluma, ipende kushirika wanataluuma wenye uwezo kwenye maeno yao. Naomba kutoa hoja.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

0716 774494

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumapili, Mei 31, 2009

No comments:

Powered by Blogger.