Header Ads

UPELELEZI KESI YA MEREY HAUJAKAMILIKA

Na Happiness Katabazi

UPANDE wa mashitaka katika kesi ya wizi wa dola za Marekani milioni 1.8 (sawa na sh bilioni 2.4) inayomkabili Mkurugenzi Mtendaji wa Dar es Salaam Cement Muslim na mfanyabiashara maarufu wa mafuta nchini, Merey Ally Saleh (41), jana uliomba kuahirishwa kwa kesi hiyo kwa vile upelelezi wake haujakamilika.

Mwendesha Mashitaka Mkuu wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam (ACP) Charles Kenyela, mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Euphemia Mingi, aliiambia mahakama kuwa kesi hiyo jana ilikuja kwa ajili ya kutajwa lakini anaomba iahirishwe kwa vile upelelezi bado haujakamilika.

Naye wakili wa Merey, Martin Matunda, aliomba mahakama kubadilisha wadhamini wa mshitakiwa Merey Ally, baada ya Sahau Kambi, aliyemdhamini awali kufariki. Matunda alidai kuwa mteja wake kwa sasa atadhaminiwa na Abel Mshoro, ombi ambalo lilikubaliwa na mahakama hiyo.

Mbali na Balahbou, washitakiwa wengine ni Meneja Mwendeshaji wa Kigamboni Oil Co. Ltd, Abdallah Said Abdallah (48), wafanyakazi wa Benki ya Barclays, Winford Mwang’onda, Shubira Mutungi, Naima Saria, Upendo Mushi, Magreth Longway, Emmanuel Mukoni na Ramadhani Khamis.

Washitakiwa wote wanadaiwa kuwa kati ya Oktoba 27 hadi Novemba mwaka jana, kwa nyakati tofauti, walikula njama za, kughushi ujumbe wa kasi (swift message), kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na kuiba dola za Marekani 1,081,263.00, sawa na sh bilioni 2.4, mali ya Benki ya Barclays.

Mapema Machi mwaka huu, Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Robert Manumba, alitahadharisha mabenki kuwapo kwa mbinu mpya ya wizi unaotumia teknolojia ya kisasa ya kompyuta, ambapo benki za CRDB na Barclays zilikwisha kukumbwa na wizi huo.

Alisema aina hiyo ya wizi ni ngeni nchini na wahusika wanaweza kuchota fedha nyingi kuliko wizi uliozoeleka wa kughushi hundi, saini au ule unaofanywa kwa kuvamia na kupora kwa nguvu kwa kutumia silaha za moto.

Wizi huo ulianza kujitokeza kuanzia mwaka jana, ambapo wezi hao wa mtandao, walifanikiwa kuwashawishi baadhi ya wafanyakazi wa benki na watu wengine kupitisha fedha hizo kwenye akaunti zao.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Mei 20, 2009

No comments:

Powered by Blogger.