Header Ads

UAMUZI KESI YA LIYUMBA BADO

Na Happiness Katabazi

KWA mara nyingine, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, jana ilishindwa kutoa uamuzi wa kumwachilia huru mshitakiwa wa kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma, aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki ya Tanzania (BoT), Amatus Liyumba na Meneja Miradi wa benki hiyo, Deogratius Kweka, au la.

Hakimu Mkazi, Waliarwande Lema, alisema jana kuwa ameshindwa kutoa uamuzi huo kwa kuwa hajamaliza kuandaa uamuzi huo. ‘Sijamaliza kuandaa uamuzi, hivyo naahirisha kesi hadi Mei 27 mwaka huu,” alisema Lema.

Kabla ya kuanza kwa kesi hiyo, makachero kutoka Jeshi la Polisi na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) walikuwa wametanda pembe zote za mahakama hiyo, ikiwamo ndani ya chumba kilichokuwa kikiendeshwa kesi hiyo, ambao miongoni mwao walidai wamefika kwa ajili ya kuwakamata washitakiwa hao endapo wataachiliwa huru na mahakama.

Hii ni mara ya tatu kwa Hakimu Lema kushindwa kutoa uamuzi kuhusu ombi hilo.
Machi 30, mwaka huu, Lema alianza kuendesha kesi hiyo baada ya Hakimu Mkazi, Hadija Msongo, kujitoa kuendesha kesi hiyo baada ya jamii kupitia vyombo vya habari kulalamikia dhamana ya Liyumba aliyopewa Februari 17.

Awali alipanga kutoa uamuzi kuhusu ombi hilo, April 30, Mei 6 na jana lakini akashindwa kafunya hivyo kama anavyoahidi kwa maelezo kuwa ajamaliza kuandaa uamuzi huo.

April mwaka huu, wakili wa utetezi Majura Magafu anayesaidiana na Profesa Gamalieli Mgongo Fimbo, Hurbet Nyange na Hudson Ndyusepo aliomba washtakiwa waachiliwe huru kwasababu hati ya mashtaka ina kasoro, na pia itupile mbali kibali cha DPP cha kufungua kesi hiyo kwa madai kuwa nacho kina dosari za kisheria.

Hata hivyo Stanslaus aliunga mkono hoja ya Magafu ya kudai kuwa hati ya mashtaka ina kasoro licha alipinga vikali kuwa kibali cha DPP kina kasoro za kisheria.

Machi 30, mwaka huu, Lema alianza kuendesha kesi hii baada ya Hakimu Mkazi, Hadija Msongo ambaye ndiye alikuwa nayo tangu ilipofunguliwa Januari 27, mwaka huu, kujiondoa baada ya jamii kupitia vyombo vya habari kulalamikia dhamana ya Liyumba.

Februari 17, mwaka huu, hakimu Msongo alimwachia kwa dhamana iliyozua utata Liyumba.
Moja ya masharti ambayo hayakutimizwa na Liyumba, ni kuwasilisha mahakamani hati zenye thamani ya sh bilioni 55, wadhamini wawili wa serikali wakiwa na barua kutoka kwa waajiri wao na kukabidhi hati za kusafiria mahakamani hapo.

Lakini siku hiyo, Liyumba aliwasilisha hati yenye thamani ya sh milioni 882, hati ya kusafiria ambayo muda wake wa matumizi umekwisha, huku wadhamini wawili wakiwa hawana barua zilizosainiwa na mwajiri wao kama masharti yalivyotolewa na mahakama.


Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Mei 22, 2009

No comments:

Powered by Blogger.