Header Ads

CASS:CHUO CHENYE MKAKATI WA KULETA UFANISI KWENYE UONGOZI


MEI 11 mwaka huu, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kinachoongozwa na Profesa Rwekaza Mukandala, kiliandika historia nyingine ya kimaendeleo baada ya Chuo cha Fani ya Sayansi za Jamii (CASS) kuzinduliwa na Rais wa Uganda, Yoweri Museveni. Katika makala hii, Mkuu wa Chuo hicho kipya, Profesa Bertram Mapunda (52), anazungumzia kwa mapana madhumuni ya kuanzishwa kwa chuo hicho na masuala mengine ya kitaalumu. Mwandishi Wetu HAPPINESS KATABAZI anaelezea zaidi.
Swali: Tueleze kwa nini Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kiliamua kuanzisha CASS?

JIBU: Asante. Kwanza ieleweke wazi kuwa mkutano wa 180 uliofanyika Agosti mosi, 2008, Baraza la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam liliidhinisha muundo mpya wa utawala wa Chuo pamoja na muunganisho wa vitengo vyake vya kitaaluma. Baraza liliidhinisha ngazi tatu za kiutawala kwenye shughuli za kitaaluma ambazo ni idara (ngazi ya chini), vyuo vya kampasi/skuli/taasisi (ngazi ya kati) na utawala wa juu wa chuo.
Kwa muundo huo, vitivo vilivyokuwapo Kampasi ya Mlimani vinafutwa isipokuwa kwa Kitivo cha Sheria ambacho mchakato wake wa mabadiliko umepewa muda. Katika mabadiliko, baraza liliidhinisha kuanzishwa kwa vyuo vya kampasi yaani Campus Colleges tatu ambazo ni Chuo cha Uhandishi na Teknolojia.
Chuo hiki kilikuwapo kwa hivyo kinaendelea, Chuo cha Fani ya Sayansi za Jamii (Collage of Arts and Social Sciences) ambacho kinatokana na idara zilizokuwa chini ya Kitivo cha Fani na Sayansi za Jamii, Chuo cha Sayansi Asilia na Sayansi Tumizi (Collage of Natural and Applied Sciences) kitachojumuisha idara zilizokuwa chini ya Kitivo cha Sayansi na Kitivo cha Sayansi na Teknolojia za Majini. Hivyo kimsingi CASS imeanzishwa ili kuleta ufanisi kwenye uongozi na utawala.
Lengo hasa la kuanzishwa kwa chuo hiki ni kupunguza urasimu wa kiuongozi uliokuwapo, kwani mfumo wa zamani wa kiutawala chuoni hapo ulikuwa ni wa ngazi nne ambazo ni idara, kitivo, chuo na chuo kikuu. Kwa utaratibu huo mpya ngazi ya kitivo imefutwa. Na ndani ya chuo hicho kipya kuna idara kumi nazo ni Idara ya Uchumi, Sanaa za Maonyesho, Lugha za Kigeni na Isimu. Nyingine ni Fasihi, Geografia, Historia na Akiolojia, elimu ya Siasa na Utawala,Takwimu, Filosofia, Socialojia na Anthropology, elimu ya dini idara ambayo bado haijaanza kufanyakazi.
Kwa hiyo, CASS sasa itakuwa na madaraka ya kufanya maamuzi mbali mbali yatakayotatuliwa kwa haraka, na kwa mfumo huu mpya chuo hiki kimepewa madaraka zaidi kuliko kilivyokuwa kitivo kwa maana hiyo maamuzi ambazo zamani yaliyokuwa yanafanywa na uongozi wa UDSM sasa yatafanywa na CASS. Hili ni jambo la kujivunia sana, kwa hiyo tunatarajia kwa muundo huu mpya kutakuwepo na mabadiliko ya kiutendaji yatakayoleta ufanisi na tija.

Swali: Ni changamoto zipi CASS inakabiliana nazo licha ya kuzinduliwa hivi karibuni?

Jibu: Bado miundombinu ni tatizo hususani ofisi za walimu bado hazijitoshelezi, vyumba vya wanafunzi tungependa wanafunzi wawe wanaishi karibu na chuo hasa ukizingatia masomo yanaanza asubuhi. Hakuna sehemu ya kupumzikia wanafunzi. Pia tunatatizo jingine la wafanyakazi kutokana na uamuzi wa ulitolewa na serikali ya awamu ya pili iliyokuwa ikiongozwa na Rais Ali Hassan Mwinyi, iliposimamisha ajira za serikali wakiwamo watendaji wa UDSM kutokana na kile kilichoelezwa matatizo ya uchumi. Kwa hiyo muda mrefu chuo kikuu hakikuajiri wafanyakazi tangu kipindi kile cha mwaka 1990. Matokeo yake leo hii UDSM ina idadi kubwa ya wahadhiri wenye umri wa kustaafu. Kwa hiyo hapa katikati kuna pengo kati ya wahadhiri wenye umri wa kustaafu na wale wanaoajiriwa. Asilimia 50 ya wahadhiri ni wale walioajiriwa miaka ya 2000 ambao wapo katika ngazi ya wahadhiri wasaidizi na Tutor Assistan.

Swali: Hali hiyo ina madhara gani?

Jibu: Wapo wahadhiri wenye uzoefu ndiyo wanastaafu sasa, ile hali ya wahadhiri wasaidizi kurithi uzoefu kwa wahadhiri waandamizi ambao wapo kwenye umri wa kustaafu inashindikana. Matokeo yake wahadhiri wasaidizi wanakosa uzoefu wa kitaaluma.

Swali: Una shauri nini kifanyike kuepuka hali hiyo?

Jibu: Wahadhiri wanaostafu serikali ione haja ya kuwapatia mikataba ya muda mrefu kama miaka mitano kwa wahadhiri hao wastaafu, ili waweze kuendeleza mchango wao katika vyuo vyetu. Kama hilo litashindikana basi pendekezo jingine naiomba serikali itoe upendeleo maalum kwa wahadhili hao wanaostaafu, waruhusiwe kustaafu wakiwa na umri wa miaka 65 badala ya 60 kama ilivyo sasa. Ikumbukwe kuwa historia ya chuo hicho anachokiongoza kwa sasa kilianzishwa 1964 wakati huo ndipo Kitivo cha Fani ya Sayansi ya Jamii kilipozalishwa. Kwa hiyo, hadi leo kitivo hicho kilipobadilika na kuwa chuo Mei 11 mwaka huu, kina umri wa miaka 45.

Alikotokea Profesa Mapunda

Profesa Mapunda kabla ya kuwa mkuu wa chuo hicho kipya, alikuwa Mkuu wa Idara ya Historia iliyokuwa chini ya Kitivo cha Fani na Sayansi za Jamii, Aliongoza idara hiyo tangu mwaka 2003 hadi Mei 2009.

Aliajiriwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Agosti 1989 kama Tutor Assistant ikiwa ni miezi michache kuhitimu Shahada ya Kwanza ya Elimu ya Malikale (Archaeology), lakini hakuweza kufanya kazi hiyo kwa muda mrefu, kwani mwezi mmoja baadaye alikwenda Marekani kuchukua shahada ya pili na ya tatu ya fani hiyo hiyo. Alirejea nchini 1995 na kuanza kufundisha historia chuoni hapo.

Alitenda kazi zake vizuri na kujiamini kwake ndiko kulikosababisha kupandishwa vyeo na wakuu wake wa kazi.

0716 774494
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Mei 28,2009

No comments:

Powered by Blogger.