Header Ads

MAHAKAMA:MwanaHALISI LIMEMKASHIFU ROSTAM AZIZ

*Latakiwa kumlipa fidia ya shilingi bilioni tatu
*Ni kwa kumhusisha na umiliki wa Richmond
*Latakiwa kumuomba radhi ukurasa wa kwanza
*MwanaHALISI kukata rufaa kupinga hukumu

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, imeliamuru gazeti la kila wiki la MwanaHALISI na washitakiwa wengine kumlipa Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz fidia ya shilingi bilioni tatu kwa kuandika habari za kumkashifu na za uongo zilizomhusisha na umiliki wa kampuni ya Richmond.

Mbali na hilo, Mahakama Kuu katika hukumu yake ambayo inaweza kuibua mjadala mkubwa katika taaluma ya uandishi wa habari kwa siku zijazo, imeliamuru gazeti hilo, kuandika habari yenye uzito ule ule katika ukurasa wa kwanza kukanusha habari hiyo dhidi ya Rostam.

Uamuzi huo wa Mahakama Kuu umechukuliwa baada ya Rostam kupitia kwa wakili wake, Kennedy Fungamtama kufungua kesi dhidi ya MwanaHALISI akilalamikia habari iliyochapishwa ukurasa wa kwanza Februari 13, mwaka jana iliyokuwa na kichwa cha habari kisemacho Richmond ya Rostam Aziz-Ikulu.

Mbali ya MwanaHALISI (Mhariri na mchapishaji), wadaiwa wengine katika kesi hiyo ya madai namba 53/2008 iliyofunguliwa na Rostam ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu wa CCM ni kampuni za uchapishaji za Printech Ltd na Standard Printers.

Taarifa ambazo Tanzania Daima Jumatano imezithibitisha kutoka Mahakama Kuu na kwa mawakili wa pande zote mbili zinaeleza kuwa, Jaji Makaramba alitoa hukumu Aprili 30 mwaka huu baada ya kusikiliza malalamiko ya upande wa mashitaka, baada ya walalamikaji, ambao ni gazeti la MwanaHALISI kutowasilisha utetezi wake katika muda uliotakiwa.

Jaji Makaramba ambaye kabla ya kuteuliwa kushika wadhifa huo, alikuwa Kamishna wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na Mhadhiri wa Kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alisema kwa sababu hiyo aliamua kusikiliza ombi la wakili wa mlalamikaji la kutaka mahakama hiyo itumie Order 8 Rule 14 ya Sheria ya Kesi za Madai ya mwaka 2002.

Sheria hiyo ambayo kwa mujibu wa Jaji Makaramba ilitumika pia kuamua kesi kati ya Kilindu dhidi ya CRDB mwaka 1994 inaipa mahakama mamlaka ya kutoa hukumu baada ya kusikiliza hoja za upande wa mmoja pale tu upande mwingine unaposhindwa kuwasilisha utetezi wake kwa wakati.

“Baada ya kusikiliza ombi la Fungamtama kwa makini na kwa kuwa hakuna ubishi kwamba upande wa utetezi umeshindwa kuwasilisha utetezi katika waliopewa na mahakama, natoa hukumu kwa wadaiwa wote na nawaamuru wadaiwa wote kulimpa fidia mlalamikaji sh bilioni tatu,” alisema Jaji Makaramba.

Sambamba na wadaiwa kuamriwa kulipa kiasi hicho cha fidia, Jaji Makaramba amewazuia wadaiwa kuchapisha na habari kama ya awali ambazo zilisababisha mlalamikaji kufungua kesi hiyo kwa sababu habari hiyo ni ya uongo na yenye lengo la kumkashifu mlalamikaji.

Kutokana na hukumu hiyo, tayari Fungamtama ambaye ni wakili wa ameshaliandikia gazeti la MwanaHALISI na kiwanda kilicholichapa gazeti hilo, barua Mei 8 mwaka huu, akilipa siku 14 tangu siku ya hukumu kuwa limeshatekeleza hukumu hiyo ya mahakama. Amri hiyo inafikia mwisho wake kesho Alhamisi.

Fungamtama katika barua yake hiyo, ameieleza MwanaHALISI kwamba, iwapo watashindwa kutekeleza amri hiyo ya katika kipindi hicho, basi watachukua hatua kutekeleza hukumu ya mahakama iliyowapa ushindi.

Akizungumza na Tanzania Daima Jumatano kwa simu, Wakili wa MwanaHALISI, Mabere Marando alikiri kuitambua hukumu hiyo na akasema tayari walikuwa wamewasilisha mahakamani kusudio lao kwa kukata rufaa kupinga uamuzi wa Jaji Makaramba.

Mbali ya hilo, Marando alikiri kuchelewa kwao kuwasilisha utetezi kwa wakati uliopangwa na kwamba walipoomba kuongezewa muda Jaji aliwakatalia.

“Ni kweli kwamba tulichelewa ku- file (kuwasilisha) utetezi tukaomba kuongezewa muda, Mheshimiwa Jaji akakataa. Mwenzetu (Rostam) akaomba apewe hukumu moja kwa moja. Jaji akakubali na Aprili 30, hukumu ikatoka.

“Sisi tunavyojua mlalamikaji alipaswa kupewa muda wa kuwasilisha ushahidi wake dhidi yetu hata kama kesi hiyo iliamriwa isikilizwe kwa upande mmoja. Lakini haikuwa hivyo Jaji kampa bilioni tatu. Ameshatoa hukumu. Tunaamini Mheshimiwa Jaji alikosea ndiyo maana tunapinga hukumu yake,” alisema Marando.

Akizungumza na Tanzania Daima Jumatano ofisa mmoja wa juu wa Printech ambao ni washitakiwa wa tatu katika kesi hiyo baada ya Mhariri na Mchapishaji wa MwanaHALISI, alisema kampuni yao ina makubaliano ya kisheria na gazeti hilo la kutohusika kwa namna yoyote na shauri lolote litakalotokana na habari wanazoziandika.

Kwa upande wake, Mhariri Mtendaji wa magazeti ya Serikali ambao ndiyo wamiliki wa kampuni ya kuchapisha magazeti ta Standard Printers Ltd, Isaac Mruma alilieleza gazeti hili kwamba, waliingizwa kwa makosa katika kesi hiyo kwani wao hawachapisha toleo la gazeti ambalo lililalamikiwa.

Mruma ambaye alikiri kupata kulichapa gazeti hilo katika mitambo yao, alisema jambo hilo lilitokea muda mrefu kabla ya habari hizo kuandikwa.

Hata hivyo Mruma alisema alikuwa akikusudia kuwasiliana na mwanasheria wao ili kuiangalia hukumu hiyo ambayo wametajwa wakiwa si wahusika.

Wakati Mruma akitoa kauli hiyo, katika barua ya wakili wa Rostam kwenda kwa washitakiwa, hakuiorodhesha Standard Printers Ltd katika barua yake ya Aprili 8, ambayo iliwapa walalamikiwa siku 14 za kutekeleza hukumu ya Mahakama Kuu.

Katika hati yake ya madai ya kesi hiyo ambayo ilifunguliwa Aprili 22, 2008, Rostam anadai kuwa, gazeti la MwanaHalisi la Februali 13-19 la mwaka jana, lenye namba 084, liliandika liliandika na kuchapisha ya habari ukurasa wa mbele habari iliyokuwa na kichwa cha habari- “Richmond ya Rostam Aziz-Ikulu. Ndiye aliyeileta nchini. Lowassa alimuingiza”

Kwa mujibu wa hati hiyo, Rostam anadai kuwa katika matoleo mengine ya gazeti hilo hilo la MwanaHALISI lilikuwa likiandika habari zilizokuwa na lengo la kumkashifu.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumatano, Mei 13, 2009

No comments:

Powered by Blogger.