Header Ads

MSHITAKIWA EPA AMLIPUA OFISA BOT

Na Happiness Katabazi

MSHTAKIWA wa kwanza katika kesi ya wizi wa bilioni 1.86 za Fedha za Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA), Bahati Mahenge, amedai aliagizwa na ofisa wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) akafungue kampuni ya mfukoni ya Changanyikeni Residential Complex kwa ajili ya wakubwa.

Madai hayo ya Mahenge ambayo aliyaandika wakati akichukuliwa maelezo ya onyo katika Ofisi za Tume ya Rais ya Kuchunguza Wizi wa EPA, Mikocheni, Machi 12 mwaka jana, ambayo yalisomwa jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na shahidi wa kwanza wa upande wa mashtaka, mpelelezi wa wizi wa kughushi nyaraka toka Makao Makuu ya Upelelezi wa Jeshi la Polisi, ASP Deustedint Mataba.

Mataba akisoma maelezo hayo, alidai Mahenge alieleza mshtakiwa wa pili katika kesi hiyo ni baba yake mdogo na kwamba aliwahi kufanya kazi katika Kampuni ya Dar Air Service iliyokuwa ikimilikiwa na mshtakiwa huyo.

Alieleza wakati akifanyakazi hapo alifahamiana na ofisa huyo wa BoT aliyemtaja kwa jina moja la Berya (sasa marehemu) na kwamba alimtaka afungue Kampuni ya Changanyikeni Residential Complex.

“Siku inayofuata nikakutana na Berya na Manase (mshtakiwa wa pili) katika mgahawa wa City Garden, wakaniambia wakati nitakapofungua kampuni hiyo nisiandike jina langu la Bahati bali nitumie jina la kufikirika la Samson Mapunda ambapo kwa mujibu wa jina hilo la kufikirika nikawa mkurugenzi wa kampuni hiyo feki,” alidai Mahenge katika maelezo hayo.

Alidai baada ya kuelezwa hayo Berya hakuonyesha kushtuka kwani alikuwa akijua mpango mzima na kuongeza kuwa ofisa huyo ndiye alimpigia simu na kumtaka akafungue akaunti ya kampuni hiyo katika Benki ya CRDB Tawi la Kijitonyama ambapo alijaza fomu hizo, akabandika picha yake halisi huku akitumia jina la bandia la Samson.

Mahenge ambaye anatetewa na wakili wa kujitegemea Majura Magafu , alidai baada ya mchakato huo kumalizika akaunti hiyo iliingiziwa sh bilioni 1.86 toka BoT na wakati mwingine alikuwa akiletewa hundi na Manase na alikiri kutoifahamu Kampuni ya Marubeni Ltd ya Japan ambayo kwa mujibu wa hati ya kuhamisha deni inaonyesha kampuni hiyo ya nje ililiridhia kampuni ya Changanyikeni ikusanye deni lake wanaloidai.

Kesi hii ilianza kusikilizwa rasmi juzi ambapo shahidi wa kwanza ASP Mataba alianza kutoa ushahidi wake lakini hata hivyo alishindwa kumalizia baada ya Magafu kuwasilisha pingamizi kuwa kabla ya mteja wake hajachukuliwa maelezo ya onyo kwenye tume ile alifanyiwa ukatili.

Sababu hiyo ilisababisha jopo hilo kukukabili kufanyika kwa kesi ndogo ambapo upande wa mashtaka ulileta mashahidi watatu.
Leo upande wa utetezi katika kesi hiyo ndogo unatarajiwa kuleta mashahidi watatu ili kuthibitisha jinsi mshtakiwa alivyofanyiwa ukatili.

Mbali na Mahenge anayetetewa na wakili wa kujitegemea Majura Magafu, washtakiwa wengine katika kesi hiyo Manase Makale, Davis Kamungu, Godfrey Mosha na Eda Makale wanatetewa na Mabere Marando, Michael Ngaro na Mafuru.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Mei 15,2009

No comments:

Powered by Blogger.