Header Ads

MAHAKAMA YAZUIA UCHAGUZI TUCTA

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam, imetoa amri ya kuzuia kufanyika kwa uchaguzi wa Katibu Mkuu wa Shirikisho la Wafanyakazi nchini (TUCTA), hadi kesi ya msingi iliyofunguliwa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Shirikisho hilo, Nestory Ngula, itakapotolewa uamuzi.
Uamuzi huo ulitolewa na Hakimu Mkazi, B. Mashabara, aliyesema amekubalina na ombi moja la Ngulla anayetetewa na Dk. Sengondo Mvungi na Deo Mwarabu, kuwa endapo TUCTA itafanya uchaguzi, bila kesi ya msingi kumalizika, ataathirika.

“Nakubaliana na hoja za mawakili wa mwombaji kuwa endapo uchaguzi utafanyika bila kesi ya msingi iliyopo mahakamani kuamriwa ni wazi kabisa Ngulla ataathirika zaidi kuliko mdaiwa na kwa sababu hiyo natoa amri kwa mdaiwa ambaye ni rais wa TUCTA, kumzuia kuitisha uchaguzi huo.

Hata hivyo Hakimu Mashabara alishindwa kutolea uamuzi wa ombi la pili la Ngulla aliyetaka mahakama itoe amri ya kutozuiliwa kuingia ofisini na kufanya kazi zake kama Katibu Mkuu hadi kesi ya msingi, itakaposikilizwa.

Katika kesi ya msingi iliyopo mahakamani hapo, Ngulla anapinga kuwa amejiuzulu wadhifa huo na kuwa taarifa za vikao viwili vya Kamati ya Utendaji ya TUCTA vilivyofanyika Machi 30 mwaka huu, vilivyoibuka na maazimio kuwa yeye amejizulu si sahihi kwani hajawahi kutangaza hivyo.

Kwa mujibu wa hati hiyo ya kesi ya msingi, Ngulla anaeleza kisheria Katibu Mkuu anajiuzulu kwa barua na kwa mujibu wa Katiba ya TUCTA; barua hiyo inapelekwa kwa Baraza Kuu la Shirikisho hilo.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Mei 29,2009

No comments:

Powered by Blogger.