Header Ads

'NILIPONZWA NA ZOMBE

*Aliyesema marehemu waliuawa Pande kutoa ushahidi leo

Na Happiness Katabazi

MSHITAKIWA wa 10 katika kesi ya mauaji ya wafanyabiashara watatu na dereva teksi mmoja, Koplo Abeneth Saro (45), ameiambia mahakama kuwa watuhumiwa aliowashuhudia kuwa walikamatwa Sinza wakiwa hai ndio waliouawa.

Sambamba na hilo, mshitakiwa wa 11, Rashid Lema, ambaye tangu washitakiwa wenzake waanze kujitetea Febuari 3 mwaka huu, hajawahi kuhudhuria mahakamani kutokana na afya yake kuwa si ya kuridhisha, leo anatarajiwa kuanza kutoa ushahidi wake.

Mshitakiwa Lema ndiye aliyeeleza katika maelezo yake kwamba mauaji hayo yalifanyika katika msitu wa Pande.
Akitoa utetezi wake jana, Koplo Abeneth ambaye ni askari kutoka Idara ya Upelelezi, Kituo cha Urafiki, alidai yeye alikuwa ni miongoni mwa askari walioongozana na mshitakiwa wa tatu, SP-Ahmed Makele, pamoja na mshitakiwa wa tano, Jane Andrew, Januari 14 mwaka 2006 kwenda Sinza Palestina, ambapo alishuhudia watu wanne wakikamatwa na askari.
Alipoulizwa na Wakili wa Serikali Mugaya Mutaki kwamba watuhumiwa aliowashuhudia ambao walikamatwa siku hiyo ndio waliokamatwa na kuuawa, alikiri kuwa ndio waliouawa, ingawa hakuweka wazi kuwa waliuawa na nani.
“Tarehe hiyo na hao washitakiwa wenzangu tulikwenda katika eneo hilo kufuatilia tukio la ujambazi na wenzangu walishuka mimi nilikuwa na pistol, nilibaki ndani ya gari na baadaye nilishuhudia watuhumiwa wanne waliokamatwa na askari, lakini baadaye nikaja kusikia kuwa wale watu ndio wameuawa,” alidai Koplo Abeneth.
Kwa upande wake, mshitakiwa wa tisa, Michael Shonza, ambaye alitoa utetezi wake juzi na jana, alianza kuhojiwa na Wakili wa Serikali Angaza Mwipopo, alidai mkono wa pongezi aliopewa na Kaimu RPC, Zombe, ndio uliomponza hadi akashitakiwa kwenye kesi hiyo.
Ifuatayo ni sehemu ya mahojiano kati ya wakili Majura Magafu na mshitakiwa Abeneth:
Wakili: Unafanya kazi wapi?
Abeneth: Kituo cha Polisi Urafiki.
Wakili: Ulijiunga na Polisi lini?
Abeneth: mwaka 1983.
Wakili: Kituo chako cha kwanza kufanyia kazi ni kipi?
Abeneth: Oysterbay hadi mwaka 1996 nikahamishiwa Magomeni na mwaka 2004 nikaamishiwa Urafiki, ambapo nilifanya kazi hadi nahusishwa na kesi hii.
Wakili: Januari 14 mwaka 2006 jioni ulikuwa wapi?
Abeneth: Nilikuwa Polisi Magomeni.
Wakili: Hapo Magomeni ulikwenda kwa shughuli gani?
Abeneth: Tulikwenda pale kupewa maelekezo ya kazi na OCD wa Magomeni, Isunto Mantege.
Wakili: Zoezi la kupangiwa kazi liliisha saa ngapi?
Abeneth: Saa 12 jioni.
Wakili: Wewe ulipangiwa eneo gani la doria?
Abeneth: Nilipangiwa na Jane Andrew, PC Edson, PC Seleman, PC Emmanuel na PC Frolian, tulipangiwa Ubungo Terminal, Mabibo na wote tulikuwa kutoka Idara ya Upelelezi.
Wakili: Hebu tuambie mlitumia usafiri gani kutoka Magomeni kwenda kwenye doria?
Abeneth: Kwanza niliongezewa askari waliovaa sare na natulitumia daladala tofauti, ila mimi na mshitakiwa wa tano tulipanda daladala moja tukashuka kituo cha basi Urafiki, tukaanza kwenda kituoni, kabla hatujafika, Makele alikuwa kwenye gari na askari waliokuwa wamevalia sare za jeshi, wakashuka, akatuambia sisi tupande kwenye lile gari na tuwe makini, kwani kuna tukio la ujambazi limetokea Barabara ya Sam Nujoma, hivyo tulikuwa tunaenda kwenye hilo tukio.
Aliwasha gari na kuingia Barabara ya Morogoro, kisha tukaingia Barabara ya Shekilango, halafu tukafika Mugabe, tukaingia ndani, halafu tukakata kushoto, mbele tukakuta umati wa watu na askari mmoja ambaye alikuwa amevalia sare, alilisimamisha gari letu. Makele na Jane walishuka na kwenda kuzungumza naye, mimi nilibaki ndani ya gari na radio call.
Wakili: Katika kundi lenu la doria nani alikuwa na silaha?
Abeneth: Mimi nilikuwa na pistol na wawili walikuwa wameambiwa waende Urafiki kuchukua silaha.
Wakili: Kwa mara ya kwanza ulijua lini wewe unahusishwa kwenye kesi hii ya mauaji?
Abeneth: Mwanzoni mwa Februari mwaka huo wa 2006, nilipoitwa kwenye Tume ya Jaji Kipenka Mussa kwa ajili ya kuhojiwa.
Wakili: Ujumbe wa wewe kuitwa kwenye tume hiyo uliupata wapi?
Abeneth: Ililetwa summons kituoni Urafiki ikinitaka mimi na Jane twende kwenye Tume ya Kipenka kuhojiwa.
Wakili: Mlikwenda?
Abeneth: Tulikwenda mimi na Jane, ila tulikwenda kwa siku tofauti. (Hata hivyo Jane juzi wakati akitoa ushahidi wake alikana kuitwa na Tume ya Kipenka na kuhojiwa).
Wakili: Uliwahi kuhojiwa kwenye tume iliyoundwa na IGP-Said Mwema iliyokuwa ikiongozwa na ACP-Mgawe?
Abeneth: Sijawahi kuitwa.
Wakili: Mbali na Tume ya Kipenka uliwahi kuandika maelezo sehemu nyingine?
Abeneth: Februari 19 mwaka 2006 niliandika maelezo Kituo cha Polisi Kati nilipokuwa nimekamatwa.
Wakili: Ulihojiwa nini?
Abeneth: Nilitoa maelezo kama ninayoyatoa (leo) jana hapa mahakamani.
Wakili: Wewe unatuhumiwa na kesi ya mauaji, unaomba mahakama ikufanyie nini?
Abeneth: Sikushiriki kukamata wala kuua watu hao na ninaamini mtukufu jaji mahahakama yako itatenda haki.
Ifuatayo ni sehemu ya mahojiano kati ya wakili wa Serikali Mugaya Mutaki na Abeneth:
Wakili: Baada ya kuandika maelezo yako ulisomewa?
Abeneth: Ndiyo nilisomewa na niliweka saini yangu.
Wakili: Hebu yatambue kama maelezo haya ni yako?
Abeneth: Mmh jina, kabila, shule niliyosoma zipo sahihi, lakini hayo maelezo na hiyo saini si yangu.
Wakili: Kwa hiyo Tume ya Mgawe, Sidney Mkumbi zilikusingizia?
Abeneth: Sijui.
Wakili: Kwanini tukio litokee Barabara ya Sam Nujoma nyie mkakimbilia Barabara ya Shekilango?
Abeneth: (kigugumizi), muulize Afande Makelle (mshitakiwa wa tatu). Afande Makelle alitueleza huenda majambazi wamekimbilia kwenye gereji kubadilisha pleti namba za gari, kwani ni desturi ya wahalifu kubadilisha pleti namba pindi wanapofanya matukio, ili wasikamatwe haraka.
Wakili: Gereji gani hizo?
Abeneth: Tulikagua gereji mbili, moja inaitwa MK na nyingine ni gereji bubu, lakini hata hivyo hatukufanikiwa.
Wakili: Ulisema hukushuka kwenye gari ulipofika eneo la tukio, wakati ni wewe ulikuwa umebeba pistol, sasa kwanini hukushuka? Je, hiyo ndiyo busara ya askari mpelelezi?
Abeneth: (kimya). (Watu wakaangua kicheko). Eeh mtukufu jaji nilibaki kwenye gari na radio call.
Wakili: Unaufahamu msitu wa Pande?
Abeneth: Siufahamu.
Wakili: Kuna ushahidi ulitolewa hapa mahakamani kwamba wewe ni miongoni mwa askari walioenda Pande kwenye tukio la mauaji?
Abeneth: Si kweli.
Ifuatayo ni sehemu ya mahojiano kati ya Wakili wa Serikali Angaza Mwipopo na mshitakiwa wa tisa, Michael Shonza.
Wakili: Juzi katika ushahidi wako ulisemwa ulipewa mkono wa pongezi na mshitakiwa wa kwanza (Zombe), je, hukuona umuhimu wa kuhoji ni kwanini unapongezwa wakati wewe umedai hukushiriki kukamata majambazi siku hiyo?
Shonza: (kimya).
Wakili: Hujawahi kumweleza kiongozi yeyote kuwa wewe hukuhusika na kukamata majambazi siku hiyo na kwamba unashangaa ni kwanini unapongezwa?
Shonza: Nilimweleza Sajenti Nico wakati ananihoji Makao Makuu ya Upelelezi.
Wakili: Pongezi ulizopewa na Zombe zilikuwa ni za nini?
Shonza: Kukamata majambazi.
Wakili: Wewe uliona ni kawaida kupongezwa?
Shonza: Eeh… kwani askari waliopongezwa ni wa Kituo cha Chuo Kikuu ambacho mimi nafanya kazi, hivyo na mimi niliona ni kawaida.
Wakili: Tangu uanze kazi polisi ulishawahi kupongezwa?
Shonza: Awali nilishawahi kupongezwa kwa kukamata silaha.
Wakili: Wewe siku hiyo ya Januari 14 mwaka 2006, ulisema ulikuwa Makongo Juu kwenye doria na wenzio walikuwa Sinza, sasa kwa nini ulikubali kupongezwa wakati hukushiriki kukamata watuhumiwa wa ujambazi?
Shonza: (kimya).
Wakili: Haya maelezo yako yanaonyesha uliyaandika kwenye Tume ya Mgawe, ni yako kweli?
Shonza: Mtukufu jaji, si yangu, licha ya kwamba nilihojiwa na tume hiyo.
Wakili: Iambie mahakama hii jina la ukoo wako ni lipi?
Shonza: (kimya).
Wakili: Tume ya Mgawe na ACP-Isaac Mugasa walikuwa wana sababu gani ya kukusingizia?
Shonza: Kwa sababu mimi ni mtumishi katika Jeshi la Polisi, hivyo ilikuwa rahisi kwao kupata particulars zangu.
Ifuatayo ni sehemu ya mahojiano kati ya Mzee wa Baraza Magreth Mossi na Shonza:
Mzee wa Baraza: Huoni ule mkono wa pongezi ndio umesababisha uingizwe kwenye hii kesi ya mauaji?
Shonza: Huo mkono wa pogezi mtukufu jaji ndio umeniponza hadi leo hii nimesimama kizimbani nikikabiliwa na kesi hii ya mauaji.
Jaji Massati aliahirisha kesi hiyo hadi leo baada ya kukubali ombi la wakili wa mshitakiwa wa 11 na 12 (Rashid Lema na Rajabu Bakari) kuomba kesi hiyo iahirishwe, ili aweze kupata fursa ya kwenda gerezani kumuona Lema.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Alhamisi, Februali 19 mwaka 2009

No comments:

Powered by Blogger.