Header Ads

SIKU YA SHERIA NCHINI,TUJADILI CHANGAMOTO

Na Happiness Katabazi

KILA Februari mbili ya kila mwaka, Mahakama ya Tanzania imejiwekea utaratibu wa kusherehekea Siku ya Sheria ambayo inaashiria mwanzo rasmi wa kazi za mahakama kwa mwaka huo.

Lakini mwaka huu, Mahakama ya Tanzania, tarehe ya leo ndiyo imeifanya kuwa Siku ya Sheria nchini. Na kauli mbiu ya mwaka huu ni: “Nafasi ya mahakama katika kutekeleza shughuli za mamlaka ya nchi kulingana na dhana ya mgawanyo wa madaraka’.

Kwa sababu hiyo, leo Rais Jakaya Kikwete atawaongoza wadau wa sheria na mahakama katika siku hiyo ya sheria ambayo kitaifa inaadhimishwa Mahakama Kuu Barabara ya Kivukoni Front Dar es Salaam. Jaji Mkuu, Agustino Ramadhani, atakagua gwaride rasmi lililoandaliwa na Jeshi la Polisi ambalo litaashiria ufunguzi rasmi wa shughuli za mahakama kwa mwaka huu.

Wakati Watanzania leo tukiadhimisha siku hii, ni vyema tukaangalia wapi tumetoka na tulipo sasa katika sheria na hali za mahakama zetu nchini.

Changamoto zinazoendelea kuzikabili mahakama zetu ni pamoja na mlundikano wa kesi, uchakavu wa majengo ya mahakama nyingi, tuhuma za rushwa kwa baadhi ya watendaji wa mahakama, ulinzi legelege katika mahakama zetu, utaratibu mbovu wa kuruhusu watu kuingia mahakamani na mifumo ya uhakika ya maji safi na taka na upungufu wa majengo ya mahakama, ukosefu wa majenereta na mfumo wa kompyuta.

Hivyo leo tukiwa tunaadhimisha siku hiyo ni vyema tutambue kwamba bado Mahakama ya Tanzania inakabiliwa na matatizo hayo niliyoyaainisha ambayo endapo viongozi wa mahakama na wanachi kwa ujumla wakisimama kidete kuipigia kelele serikali ili iongeze bajeti kwa mhimili wa mahakama naamini matatizo haya yatakoma.

Hii ni mara ya tatu kuandika makala ya matatizo yanayoikabili mahakama zetu lakini na kwa kiasi fulani baadhi ya matatizo kama huduma ya makaratasi, mafaili, ongezeko la mahakimu japo bado halijakidhi mahitaji limeanza kutatuliwa na mamlaka husika.

Miaka iliyopita mwananchi aliyekuwa akifika katika mahakama zetu za mwanzo na wilaya kwa nia ya kufungua kesi alikuwa akitakiwa atoe fedha ya kununulia karatasi ya kufungulia kesi lakini hivi sasa suala hilo halipo.

Kuhusu ucheleweshwaji wa kesi, watu wengi wanaitupia lawama moja kwa moja mahakama huku wakieleza kuwa katika kesi za jinai, kwa sisi tunaoshinda mahakamani kwa siku tano za Juma, tumekuwa tukishuhudia upande wa upelelezi katika kesi za jinai ndiyo umekuwa kikwazo kikubwa kwa kesi hizo kushindwa kumalizika kutokana madai kwamba upelelezi wa shauri husika haujakamilika hali inayomsababisha hakimu kuahirisha kesi.

Licha ya upelelezi kukamilika pia kuna baadhi ya mashahidi kwa makusudi tena bila kwa sababu za msingi wamekuwa wakishindwa kufika mahakamani kutoa ushahidi ili kesi hizo ziweze kukamilika na kutolewa uamuzi kwa haraka na hakimu husika aweze kuendelea kuendesha kesi za wananchi wengine ambao wengine wanasota magerezani.

Kwa upande wa rushwa kuna baadhi ya mahakimu na makarani wamekuwa wakituhumiwa waziwazi kwamba ni vinara wa rushwa katika kesi mbalimbali na tuhuma hizo zimekuwa zikitolewa na baadhi ya ndugu wa watuhumiwa kwenye ‘korido’ za mahakama utakuta wakati mwingine watuhumiwa wa ndugu waliokuwa wakitoa tuhuma hizo, mwisho wa siku ndugu zao wanashinda kesi.

Kwa kweli tuhuma kama hizi zinaweza kuwa na ukweli ama si za kweli lakini tukubaliane kwamba zinachafua sifa za mahakama zetu kwani inaonekana haitoi haki kwa mujibu wa sheria bali inatoa haki kwa mujibu wa rushwa.

Kuhusu usalama wa mahakama zetu, hasa hizi mahakama za mikoa kushuka chini ulinzi wake ni hafifu mno na katika kuthibitisha hili ni Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, mahakama hii ni maarufu na inaendelea kujizolea umaarufu kwa kuendesha kesi mpya za vigogo wa serikali, kesi za EPA lakini vyombo vya ulinzi na usalama hapo awali hawakuona umuhimu wa kuimarisha ulinzi katika mahakama hiyo hadi vyombo vya habari vilipopiga kelele kwamba ulinzi uongezwe.

Kwa sasa vyombo hivyo vya ulinzi vimeanza kuweka ulinzi wakati kesi hizo zikiendelea, lakini naeleza ulinzi huo hautoshi kwani kutokana na hali ilivyo sasa Kisutu, tunataka kuona mahakama inazungusha uzio wa uhakika mahakama hapo na kuweka kampuni za ulinzi kwa saa 24; walinzi hao watakuwa wakiwatambua wanaoingia na wanaotoka katika mahakama hiyo.

Ama sivyo tutakuwa tunafanya biashara ya ‘kumvalisha mbu miwani’. Wiki iliyopita Hakimu Mkuu Mfawidhi wa Kisutu, Addy Lyamuya, alilazimika kupiga simu polisi kuomba polisi waje kuimarisha usalama mahakamani hapo, lakini kwa mujibu wa taarifa toka kwa baadhi ya watendaji wa mahakama hiyo zilidai kwamba kulikuwa na njama za kutaka kunyofolewa kwa majalada ya kesi za EPA.

Iwe iwavyo tunataka kuona ulinzi ukiimarishwa mahakamani hapo na katika mahakama nyingine kwani ni fedha nyingi za walipa kodi zinatumika kwa ajili ya kuendesha kesi mbalimbali, hivyo tusingependa kusikia nyaraka za kesi fulani zimepotea ni kheri tukatumia fedha nyingi kujenga ufa ili mahakama ambazo ni kimbilio la wananchi wanaotafuta haki wapate haki.

Nitakuwa sitendi haki kama sitatoa pongezi kwa mhimili wa mahakama kwa harakati zake kuendeleza ujenzi wa mahakama katika baadhi ya mikoa.

Aidha wakati leo tukiwa tunaadhimisha siku ya sheria bado, sheria dhalimu zinaendelea kutumika nchini. Na ikumbukwe mahakama haiwezi kuzitupa sheria hizo tunazodai kwamba ni mbaya bila ya sisi wananchi kupeleka maombi yetu mahakamani kwamba mahakama zizitupilie mbali sheria hizo.

Wananchi hususani waandishi wa habari wenzangu tusiishie kulalamika mitaani na kwenye magazeti kwamba Sheria ya Magazeti ya mwaka 1976, twende mbele zaidi kwa kufungua kesi ya kikatiba pale Mahakama Kuu kupinga sheria hiyo, la sivyo sheria hiyo itaendelea kuwepo na kukandamiza uhuru wa habari nchini.

Nimalizie kwa kutoa rai kwa mahakama kwamba wakati umefika kwa wananchi kuhamasishwa kuwa mahakamani ni sehemu ya amani ambapo watu hufika na kupata haki wanayostahili ili baadhi ya wananchi waondokane na dhana ya kuamini unapokuwa na kesi au ndugu yako akiwa na kesi mahakamani ni lazima atoe rushwa ndiyo ashinde kesi au kupata dhamana.

Na suala hili litafanikiwa kama kuanzia sasa mhimili wa mahakama utafungua milango kwa waandishi wa habari za mahakamani na kuwaandalia mafunzo ya kisheria ya muda mfupi waandishi wa habari za mahakamani ili waweze kuboreka katika nyanja hiyo ya kuripoti kesi za mahakamani.

Kwani hivi sasa mahakama ya Tanzania imeendelea kujijengea heshima mbele ya jamii kutokana na majaji na mahakimu wake kutoa maamuzi mazito katika kesi mbalimbali ambazo zimekuwa zikigusa hisia za wananchi wengi, hali hiyo tunaweza kuielezea kuwa hivi sasa imeleta mwamko kwa wananchi kupeleka kesi zao mahakamani.

Tuache kulaumiana, wadau wa sheria nchini na Mahakama nchini tushirikiane kikamilifu ili kuleta ufanisi kwa maslahi endelevu ya nchi yetu.

Hivyo wakati leo tukisherehekea siku ya sheria nchini ni lazima tutambue bado kuna changamoto nyingi zinaikabili Mahakama Tanzania na wahusika hawanabudi kuzikabili changamoto hizo.

Mungu ibariki Afrika, Mungu Ibariki Tanzania

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Februari 6 mwaka 2009

No comments:

Powered by Blogger.