Header Ads

KORTI KUU YATOA DHAMANA KWA VIGOGO WA BOT

Na Happiness Katabazi

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, jana ilitoa masharti ya dhamana kwa kesi ya uhujumu uchumi na kuisababishia serikali hasara y ash bilioni 104,inayomkabili Mkurugenzi wa Benki Kuu ya Tanzania(BoT), Simon Mkonga na wenzake watatu.


Uamuzi huo ombi la dhamana lilowasilish mwishoni mwa mwezi Septemba mwaka huu, mahakamani hapo,ulitolewa na Jaji Emil Mushi ambaye alisema amekubaliana na ombi la mawakili wa washitakiwa Mpare Mpoki na Richard Rweyongeza kwasababu kwasababu kisheria mahakama hiyo ndiye yenye mamlaka ya kutoa dhamana kwa washitakiwa wa kesi ya uhujumu uchumi.

Jaji Mushi alisema ili mshitakiwa apate dhamana ni lazima kila mmoja asaini bondi ya bilioni 13, kutoa hati au fedha taslimu sh bilioni 13 na kuwa na wadhamini wawili watakaosaini bondi ya kiasi hicho cha fedha, kusalimisha hati ya kusafiria, kutotoka nje ya Dar es Salaam hadi kwa kibari cha mahakama na kila Jumatatu kabla ya saa sita mchana kuripoti kwa Mkuu wa Polisi Mkoa Ilala na kwamba hati hizo zipelekwe kwa Msajili wa Mahakama Kuu ili asikague.

Septemba 18 mwaka huu, Hakimu Samwel Maweda ambaye ndiye anasikiliza kesi ya msingi iliyofunguliwa katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala dhidi ya washitakiwa hao, alitupia mbali hoja ya utetezi iliyokuwa ikidai kuwa mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza kesi hiyo.

Hakimu Maweda alisema hoja hiyo iliyowasilishwa na wakili wa utetezi, Mpare Mpoki, imeshangaza na kusema kwamba hakubaliani nayo kwani ina nia ya kupotosha kwa makusudi kifungu cha 29 cha Sheria ya Uhujumu Uchumi iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002, na kifungu cha 245(1,2,3) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai.

Alisema kifungu hicho cha sheria kinatamka wazi kwamba, mtuhumiwa wa kesi ya aina hiyo anapokamatwa anapaswa kupelekwa katika mahakama za chini kwa ajili ya hatua za awali.

“Kwa sababu hiyo ya kisheria, natupilia mbali hoja hiyo ya upande wa utetezi kwa sababu ina lengo la kupotosha kifungu hicho cha sheria kwani kesi hiyo imefunguliwa kihalali na washitakiwa walisomewa mashitaka yao na hawakupaswa kujibu chochote kwa sababu mahakama hii haina mamlaka ya kusikiliza,” alisema Hakimu Maweda.

Pia alisema anatupilia mbali pingamizi la upande wa utetezi lililotaka mahakama hiyo iwaachilie huru washitakiwa kwa sababu hawakupaswa kushitakiwa kwa kuwa wana kinga ya kutokushitakiwa kama ilivyoainishwa kwenye kifungu cha 65(1)(c) cha Sheria ya BoT.

“Nakubaliana na hoja ya upande wa mashitaka kwamba washitakiwa hao wakati wanatenda makosa hayo walikuwa na nia mbaya, na ikumbukwe sheria hiyo ya BoT inaweka kinga ya kutoshitakiwa kwa wafanyakazi wanaotenda makosa wakiwa na nia njema...hivyo natupilia mbali pingamizi hilo,” alisema.

Mbali na Mkango, washitakiwa wengine ni Simon Jengo na Naibu Mkurugenzi Fedha za Nje, Kisima Mkango, Kaimu Mkurugenzi wa Kitengo cha Sheria, Bosco Kimela pamoja na Mkurugenzi wa masuala ya kibenki, Ally Bakari.

Katika kesi hiyo, washitakiwa hao wanadaiwa kwa nyakati tofauti kati ya mwaka 2004 na 2007, waliisababishia serikali hasara hiyo kwa kudanganya miongozo kwa kuongeza gharama za uchapishaji wa fedha za noti ikilinganishwa na gharama halisi.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumamosi, Oktoba 10,2009

No comments:

Powered by Blogger.