Header Ads

MRAMBA AITEGA SERIKALI

*Sasa agoma kutaja orodha ya mashahidi wake
*Mjadala mzito waibuka, Mahakama kuamua leo


Na Happiness Katabazi

UPANDE wa utetezi katika kesi ya matumizi mabaya ya ofisi za umma na kuisababishia hasara serikali ya sh bilioni 11.9, inayomkabili aliyekuwa Waziri wa Fedha, Basil Mramba na wenzake wawili, umekataa kutaja orodha ya mashahidi wake.


Msimamo huo mkali ulitolewa jana na jopo la mawakili wa upande huo, linaloongozwa na Hurbet Nyange, Peter Swai, Profesa Leonard Shahidi pamoja na Cuthbert Tenga, mbele ya jopo la Mahakimu Wakazi wanaosikiliza kesi hiyo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, John Utamwa, Sam Rumanyika na Saul Kinemela.

Awali kabla ya mawakili hao kuanza kuwasilisha pingamizi hilo, Wakili Kiongozi wa Serikali, Stanslaus Boniface akiwa na Fredrick Manyanda, waliikumbusha mahakama kuwa kesi hiyo jana ilikuja kuona upande wa utetezi umebaini nini katika Waraka Na. 2, wa Jaji Mkuu wa mwaka 1999, ya Sheria za Mwenendo wa Makosa ya Jinai na Sheria ya Mahakama za Mahakimu Wakazi ili kujibu ombi la upande wa mashitaka lililowataka wataje orodha ya mashahidi wao.

Akijibu hoja hiyo wakili wa Mramba, Nyange aliieleza mahakama kuwa kwa niaba ya mteja wake, msimamo alioutoa juzi bado haujabadilika wa kukataa kutaja orodha ya mashahidi.

“Vile vile leo (jana) napenda kuongezea nguvu msimamo wangu kwa vifungu vya sheria na kwa ufasaha kabisa tunaheshimu nafasi ya Jaji Mkuu kutoa miongozo ya kisheria kuhusiana na miendeno ya kesi mahakamani.

“Pamoja na hayo kwa niaba na kwa nafasi niliyonayo kama wakili, pia ofisa wa mahakama nipo hapa kuisaidia mahakama kufikia maamuzi sahihi ya kisheria na si vinginevyo, hivyo napinga ombi la upande wa mashitaka la kutaja orodha ya mashahidi,” alidai Nyange.

Nyange ambaye alikuwa akiwasilisha hoja hizo kwa tahadhari kubwa, alieleza kuwa kutokana na barua yenye kumbukumbu namba JWC/C40/8/135 ya Mei tano mwaka 1996 na Waraka namba mbili wa Jaji Mkuu wa mwaka huo, na kupitia kwa makini ukurasa wa mwisho, aligundua mapungufu yakiwemo ya sahihi ya Jaji Mkuu, marehemu Francis Nyalali na kuongeza kuwa ana shaka kama barua hiyo iliandikwa na Jaji huyo.

Wakili huyo aliendelea kudai kuwa mahakama itakuwa imekiuka sheria endapo itatumia taratibu nyingine ambazo hazijaainishwa kwenye kifungu cha sita cha Judicatural Application of Law, sura ya 128(JALA), ambapo kifungu hiki kinaeleza Mahakama Kuu inapaswa kufuata sheria zilizoandikwa na kutangazwa kwenye gazeti la serikali, nguvu zilizowekwa katika mahakama, vitabu mbalimbali vya sheria hivyo mahakama ya hakimu Mkazi inapaswa kufuata kifungu hicho.

Nyange aliendelea kuchambua sheria kwamba kifungu cha 192(6), cha Sheria ya Makosa ya Jinai ya mwaka 2002, inampa Waziri wa Sheria kutunga sheria kwa kushirikiana na Jaji Mkuu, kisha itangazwe kwenye gazeti la serikali, pia hana pingamizi juu ya kifungu cha 71(1), cha Sheria ya Mahakama za Mahakimu Wakazi, kinachoeleza Jaji Mkuu ana uwezo wa kutengeza utaratibu na kutoa maelekezo ya jinsi mahakama wakati zitakavyoendesha kesi.

“Kwa hiyo kwa heshima na taadhima tunatamka kuwa waraka wa Jaji Mkuu sio sheria na endapo mahakama hii itauona kuwa ni sheria basi waraka huo ulitengenezwa kinyume na kifungu cha 192(6), na auendani kabisa na matakwa ya kifungu chenyewe,” alidai Nyange.

Aidha alidai, muda ambao mshitakiwa anatakiwa kutaja mashahidi wake ni baada ya upande wa mashitaka kufunga kesi yake na mahakama ikamwona mshitakiwa ana kesi ya kujibu, hapo ndipo mahakama inawajibu wa kumuuliza mshitakiwa kama ana mashahidi, endapo atakuwa nao atatakiwa kujata orodha ya mashahidi wake.

“Maelekezo ya Jaji Mkuu na waraka wake huo unapingana na kifungu cha 231 (4), cha Sheria ya Makosa ya Jinai, ambayo ndiyo sheria mama ya makosa hayo, kwani kifungu hicho kinataja wazi muda wa mshitakiwa kutaja orodha ya mashahidi wake,” alidai Nyange na kusababisha watu wanaoudhuria kesi hiyo kuangua vicheko mara kwa mara.

Wakili huyo alidai kesi inayomkabili mteja wake (Mramba) ni mpya nchini ambapo kwa lugha ya Kiswahili inaitwa (kesi za ufisadi) na kama mteja wake atalazimishwa na mahakama kutaja orodha ya mashahidi hadharani, atakuwa hajatendewa haki,”

Katika kuiunga mkono hoja hiyo wakili wa mshitakiwa wa pili (Yona), Cuthbert Tenga, alikubali hoja hiyo iliwasilishwa na wakili mwezake Nyage, ambapo pia aliupinga vikali Waraka wa Jaji Mkuu kwa kufafanua kuwa, ulitolewa kwa shughuli za kiutalawa katika mahakama na posho za mashahidi hivyo waraka huo hauna kitu kipya.

“Nasema waraka wa Jaji Mkuu ulitolewa kwa ajili ya utawala na posho za mashahidi wanaofika mahakamani kutoa ushahidi, hata ulipotengenezwa alipewa IGP na Mwendesha Mashitaka wa Serikali kutokana na taasisi hizi mbili kuhusika kikamilifu katika kesi za jinai mahakamani, hivyo ieleweke wazi waraka wa Jaji Mkuu upo kwa ajili ya posho za mashahidi. ”alidai Tenga na kusababisha watu kuangua vicheko.

Wakili wa tatu kujibu hoja alikuwa wakili wa mshitakiwa wa tatu (Mgonja), Profesa Shahidi ambapo pia aliupinga waraka kutumiwa na upande wa mashitaka katika kesi hiyo, kwa lengo la kuwalazimisha watoe orodha ya mashahidi.

Alidai kuwa kwa mujibu wa kifungu cha 192(6) cha Sheria ya Jinai, kinampa uwezo Waziri wa Sheria kutunga sheria kwa kushirikiana na Jaji Mkuu na ikishatungwa, lazima itangazwe kwenye gazeti la serikali.

“Taarifa ya umma kutangazwa kwenye gazeti la seriakali ni kitu muhimu, wananchi wataisoma na kuifahamu na ndiyo maana jana (juzi) mawakili wote wa utetezi tulisema hatuujui huo Waraka Na.2 wa Jaji Mkuu wa mwaka 1999, kwa sababu haujawahi kutangazwa kwenye gazeti la seriakali, hivyo naungana na mawakili wenzangu kukataa ombi la upande wa mashitaka la kuutaka upande wa utetezi kujata orodha ya mashahidi sasa kwani huu siyo wakati wake kisheria,” alidai Profesa Shahidi.

Akipangua hoja za mawakili wa utetezi kwa mwembwe, wakili Kiongozi wa Serikali, Boniface alidai ukiangalia waraka wa Jaji mkuu wakati huo Francis Nyalali una majina yake na kuongeza kuwa, upande wa utetezi umeonyesha wasiwasi kuhusu waraka huo.

Alidai kuwa ni jukumu la upande huo kuleta ushahidi utakaoishawishi mahakama kuwa waraka huo sio wa Jaji Mkuu kwani wao wanafahamu kwamba waraka huo ni wa jaji Mkuu.

Bonicafe, alidai upande wa mashitaka unakataa hoja ya kuwa Waraka huo haukinzani na Sheria ya Makosa ya Jinai kwa sababu tayari wakili Tenga alishaiambia mahakama hiyo kuwa waraka huo hauna kitu kipya na kuhoji kuwa kama haina kitu kipya ni kwanini upande huo unadai waraka huo unapingana na Sheria ya Makosa ya Jinai na kuhoji kuwa kama hauna kitu kipya mgongano unatoka wapi?.

“Tunaona upande wa utetezi umejichanganya, sisi tumewambia wataje orodha ya mashahidi siyo wawaite mashahidi mahakamani, sasa sioni kama kunakubisha katika hili, sisi tulitaka mtaje orodha ya mashahidi siyo kuwaita, ugumu uko wapi. Nafikiri upande wa utetezi hawakutuelewa,” alidai Boniface nakusababisha watu kuangua vicheko.

Hata hivyo Utamwa umeutaka upande wa utetezi leo kuzijibu hoja hizo mahakamani ambapo usikilizwaji wa awali wa kesi hiyo inayovuta hisia za wengi, unaendelea.

Juzi Wakili wa serikali Boniface baada ya kumaliza kutaja idadi ya mashahidi 17 kuwa ndiyo wanatarajiwa kutoa ushahidi kwa upande wa mashitaka, aliutaka upande wa utetezi nao utaje na orodha ya mashahidi wao watakaowaletwa kutoa ushahidi katika kesi hiyo.

Mbali na Mramba, washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Daniel Yona na Katibu Mkuu Mstaafu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Gray Mgonja.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumatano, Septemba 24, 2009

No comments:

Powered by Blogger.