Header Ads

SIASA KATIKA UTENDAJI HADI LINI?

Na Happiness Katabazi

UTAWALA wa awamu ya nne umefikia pahala unatisha.Raia wanyonge wananyang’anywa kile kidogo walichonacho kwa kutumia sheria za dola.
Hilo tumeliona kwa wingi wa matukio ya bomoa bomoa ,uchukuaji wa ardhi za kutolipwa fidia zinazostahili kwa waathirika wa matukio hayo.

Rasilimali za nchi zinaporwa na wageni wakishirikiana na kikundi kidogo cha mafisadi wenyeji kwa kisingizio cha uwekezaji.Hilo nalo limetungiwa sheria na kufadhiliwa na dola.

Watendaji wa serikali walio wengi wamekumbwa na utendaji utokanao na sheria zenye kulinda ufisadi na hivyo ama kwa kutodhamiria wanajikuta wamekuwa sehemu ya ukandamizaji wa uhujumu wa maslahi ya nchi.

Utawala wa kisiasa umejivisha joho la ‘siasa pendwa’ zisizozingatia haki ,hila zinajali majungu,fitna,kujikomba ,wivu,uonevu,ubaguzi,mifarakano na ushirikina.Vyombo vya utendani wa haki vimekaliwa na baadhi ya watendaji ambao wengi wao ni dhahifu kitaaluma na baadhi yao ni makuwadi wa wanasiasa na wengine ni mafisadi.Haki imewekwa njia ya panda, inanunulika ukiwa na fedha na nguvu kwenye mamlaka ya nchi katika awamu hii.

Raia wanapopiga mayowe kwa hamaki na uchungu kuusiana na haya yote , wanapewa lugha kwamba mamlaka ya nchi ipo vitani dhidi ya ufisadi na wataona matokeo yake kwa kesi nyingi zilizofunguliwa na zitakazofunguliwa mahakamani zinazohusu vigogo.

Wapo baadhi wanalolishangilia hili wakizani ni ufumbuzi kumbe wasijue kiini macho au usanii uliojengeka katika mfumo wa ‘siasa pendwa’ .Kesi hata zingekuwa elfu moja haziwezi kuwa ufumbuzi wa ufisadi kama Katiba na Sheria zetu hazikuumbwa kupambana na ufisadi.

Hao watuhumiwa watabezwa,kukashifiwa,kunyanyaswa lakini wanaweza kuachiwa na Mahakama mwisho wa siku.Hata kama kweli ni mafisadi tatizo ni ubora wa Katiba na sheria tulizonazo.

Lakini watuhumiwa waliopo mahakamani na watakaofikishwa wanaweza kuwa ni wahanga wa usanii wa ‘siasa pendwa’,wamekamatwa na kupelekwa mahakamani ili kutuliza hasira za umma wakati ukweli ni kwamba hawausiki wala hakuna ushahidi kwamba kweli walifanya ufisadi wanashitakiwa nazo.

Sasa hili ni jambo kubwa ambalo wananchi wengi hawajaliona na Idara ya Usalama wa Taifa chini ya Mkurugenzi shupavu,Rashid Othman walitupie macho na kulifanyia kazi haraka na kikamilifu.Kwani ni hatari watu wasiyo na hatia kutuhumiwa ,kunyanyaswa,kukashfiwa na hata kufunguliwa kesi za ufisadi au kesi zozote bila ushahidi.

Jambo kama hilo uzaa chuki binafsi ndani ya familia za watuhumiwa na kuligawa taifa katika makundi kwani tukumbuke kila binadamu ni mwanajamii ana ndugu,marafiki na ana jamii inayomzunguka ambayo inaweza kuungana naye na kumtetea kwa namna yoyote pale inapoonekana hakutendewa haki.

Taifa linaweza likajikuta linaingia kwenye machafuko na mauaji ya koo,makabila,dini na hata Kiitikadi kama itaadhiirika kwamba mtu fulani alituhumiwa na kufikishwa mahakamani bila ushahidi ili kumchafulia jina, chuki binafsi,kutokana na kunyang’anyana mabibi ,kutokana na magomvi ya kushindana kwenye zabuni,vyeo,kumkomesha mtu fulani kwasababu unadhani hakuheshimu au alikuwa akuungi mkono katika harakati zako za kupata cheo fulani.

Sote tunajua hao baadhi ya watuhumiwa wa kesi mbalimbali wengine wanaangukia katika makundi hayo niliyoyataja hapo juu.

Tutaona mmoja baada ya mwingine akiachiwa na mahakama na hilo lisijekutushangaza wala isije ikafikirika kwamba mahakama imenunuliwa kwa kuwa tunachokijua katika baadhi ya kesi hizo ni kwamba upelelezi ulifanyika harakara na ovyo ovyo kwa mashinikizo ya kisiasa yaliyogubikwa taaluma za kipelelezi na kisheria na chuki za wazi zimejidhiirisha na kuashiria maslahi binafsi katika kesi hizo badala ya maslahi ya taifa.

Watanzania na hayo ninayoyasema tumekuwa tukielezwa kwa siri na wahusika wa kuu wa kesi hizo wanaofanyakazi serikali na ndiyo sababu inayonisukuma kuandika makala hii kutoa taadhari hizo.Licha wananchi wengine ambao nao wamekuwa wakipata taarifa hizo toka kwa serikali wamekuwa wakizungumza katika mitaani.

Hukumu ya kesi ya mauji ya watu wanne iliyokuwa ikimkabili aliyekuwa Kamishna Msaidizi wa Polisi(ACP)Abdallah Zombe na wenzake iliyotolewa na Jaji Salum Massati Agosti 17 mwaka huu, iwe mfano endelevu wa haya tunayoyasema.Tunachokiona kesi hizi za ufisadi zinaweza zenyewe kuzaa ufisadi kwa maana mabilioni ya fedha yanaendelea kutumika kuzishughulikia wakati mavuno yatakuwa kiduchu.

Atakayebeba msalaba huu ni mlipa kodi hivyo tuna haki ten asana ya kutoa taadhari kwamba ofisi ya Mwendesha Mashitaka ,ofisi ya TAKUKURU zivunjwe na kuundwa upya kwa kuzingatia vigezo vya kitaaluma zaidi kuliko siasa.Kwani hivi sasa zinafanyakazi kama Idara ya Chama cha Mapinduzi(CCM).Hatuoni jinsi gani ofisi hizi ni za kitaaluma kwani sheria bado inaziweka mikononi mwa rais ambaye Mwenyekiti wa CCM.

Kwa hiyo ofisi hizo kupokea mashinikizo na maelekezo ya kisiasa sijambo la kubuni.Na ndiyo maana rais Jakaya Kikwete hivi karibuni, alikuwa na jeuri ya kuwaeleza wananchi kwamba kuna kesi tatu kubwa zitafunguliwa hivi karibuni.Sasa Mkurugenzi wa Mashitaka(DPP) ni rais Kikwete au Eliezer Mbuki Feleshi?

Katiba na Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002, inasema mwenye mamlaka ya kushitaki au kutoshitaki ni DPP ,sasa inakuwaje rais wa nchi kuingilia mamlaka ya DPP?.Na katika kutoa tamko hilo rais alitumia kofia ipi ya urais au mwenyekiti wa CCM?

Mungu Ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika.

0716 774494

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima Jumapili, Oktoba 11,2009

No comments:

Powered by Blogger.