Header Ads

WATANZANIA WATEGEMEE NINI KWENYE 'PH' YA LIYUMBA?


Na Happiness Katabazi

SEPTEMBA 25 mwaka huu, Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Dar es Salaam, imepanga kusikiliza maelezo ya awali yatakayosomwa na upande wa mashitaka katika kesi ya matumizi mabaya ya ofisi ya umma na kuisababishia serikali hasara ya sh bilioni 221 inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Utumishi na Utawala wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Amatus Liyumba.


Mei 28 mwaka huu, Wakili Kiongozi wa Serikali, Justus Mulokozi alidai mahakamani hapo kuwa Liyumba anakabiliwa na makosa mawili ya jinai katika kesi hiyo namba 105/2009 kwa matumuzi mabaya ya ofisi ya umma ambapo anadaiwa kuwa kati ya mwaka 2001-2006 akiwa mwajiriwa wa serikali, aliidhinisha ujenzi wa minara pacha, bila idhini ya Bodi ya Wakurugenzi wa Benki Kuu, uamuzi ambao ulisababisha serikali kupata hasara ya kiasi hicho cha fedha.

Kwa kuwa kesi hiyo imevuta hisia za wananchi wengi na kwa kuwa kesi hiyo ina masilahi ya umma ndani yake , ni vizuri wananchi wajue, kumbe kupangwa kwa ajili ya mshitakiwa kusomewa maelezo ya awali (PH), kuna maanisha kwamba upande wa mashitaka sasa umekamilisha upelelezi wake na upo tayari kuendesha kesi dhidi ya Liyumba.

Ni vizuri wananchi watambue kuwa hatua hiyo ya kisheria ni kama ifuatavyo:
Utaratibu wa kesi za jinai baada ya kukamilika kwa upelelezi wa kesi, mtuhumiwa anasomewa maelezo ya vitendo, vituko ambavyo vinaelezea mashitaka yanayomkabili.

Kisheria hatua hiyo inaitwa (Preliminary Hearing), ambapo inafanyika kwa mujibu wa Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Mwendesha mashitaka akishamaliza kumsomea maelezo hayo mshitakiwa au wakili wake watatakiwa kukubali kila kituko kilichoelezwa na akishamaliza anatia saini na hapo ndipo upande wa mashitaka unatakiwa kueleza mfumo wa uendeshaji wa mashitaka katika kesi husika utakavyokuwa, mfano kutaja idadi ya mashahidi na vielezo vitakavyotolewa mahakamani.

Na baada ya zoezi hilo mahakama ndiyo itapanga tarehe rasmi ya kuanza kusikiliza kesi husika. Huo ndiyo mfumo wa kawaida wa usomaji wa maelezo ya awali (PH).

Sasa ikiwa mahakama haina mamlaka ya kusikiliza kesi husika, zoezi la aina hiyo linapofanyika, mtuhumiwa hatakiwi kujibu kama anakubali maelezo hayo au ana yakata kwa kuwa zoezi hilo linafanyika ili tu kuweka rekodi kwamba upelelezi umekamilika na sasa jarada la kesi husika linafungwa kwa ajili ya kuhamishiwa mahakama yenye mamlaka ya kusikiliza kesi husika.

Zoezi hilo kisheria huitwa (Commital Proceedings). Ambapo pia utaraibu huu nao umeainishwa katika sheria hiyo hiyo ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai.

Kwa tafsiri hiyo, tujiulize wananchi wategemea nini kutoka kwenye maelezo ya awali katika kesi ya Liyumba? Je, mkoba wa upande wa mashitaka katika kesi hiyo unaobebwa na Wakili Kiongozi wa Serikali, Justus Mulokozi, umesheheni ushahidi gani unaofanya serikali iridhike kwamba sasa kesi ya Liyumba imeiva?

Nauliza maswali haya kwa vile bado nina kumbukumbu na kihoro kilichowakumba mawakili wa serikali Agosti 17, 2009 baada ya Mahakama Kuu ya Tanzania hukumu ya kesi ya mauaji iliyokuwa ikimkabili aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Dar es Salaam, ACP-Abdallah Zombe na wenzake tisa ilivyomalizika kusomwa na washitakiwa wote kuachiwa huru baada ya mahakama kuwaona hawana hatia.

Ni dhahiri kama alivyosema Jaji wa Mahakama ya Rufaa Salum Massati kwenye kesi ya Zombe kwamba wingi wa mashahidi si hoja, bali ubora wa mashahidi.

Pia tukumbuke tahadhari ambayo hukumu ile ya kesi ya Zombe imeweka kwamba kuleta ushahidi dhaifu kwenye kesi husika hautaisaidia serikali yetu.

Ikiwa mtenda kosa hakuletwa mahakamani, mahakama haina uwezo wa kuisaidia serikali kupambana na uhalifu unaohusika.

Kwa hiyo tunatazamia serikali imejifunza na haitaleta tena mchezo wa kuigiza katika kesi ya Liyumba kwani tungali tukikumbuka madudu yaliyofanywa na upande wa serikali katika kesi namba 27 ya mwaka huu, iliyokuwa ikimkabili Liyumba na Meneja Miradi wa Benki Kuu, Deogratius Kweka, Mei 27 mwaka huu, ambayo ilimlazimisha Hakimu Mkazi, Waliarwande Lema kuifuta kesi hiyo kwa sababu hati ya mashitaka ilikuwa na dosari za kisheria.

Nasema kama mkoba wa mwendesha mashitaka katika kesi ya Liyumba hauna kitu ni afadhali akubali yaishe, Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) Eliezer Feleshi, aondoe mashitaka mahakamani, ili kumuondolea kero mshitakiwa na asipoteze rasilimali za wananchi bure katika kesi hiyo.

Tukumbuke muda wa mahakama, rasilimali watu inavyotumika, kodi ya wananchi na matumaini ya wananchi, vyote ni gharama kubwa kwa mlipa kodi.

Lengo la Watanzania ni kupambana na ufisadi wala si kuona wingi wa watuhumiwa wakifikishwa mahakamani.

Kwa hakika inawezekana kwamba baada ya wimbi hili la maigizo la kupeleka watu mahakamani, serikali ikavuna machungu wakati washitakiwa watakapofungua kesi za madai ya kukashifiwa na serikali pale itakapoonekana kwamba lengo lilikuwa tu kuwapaka matope japo serikali ilikuwa haina ushahidi wa kutosha.

Tunajua sheria za nchi pia zinaruhusu kesi za madai ya kufunguliwa mashitaka ya kero, bugudha, yaani ‘malicious’ pale itakapoonekana serikali iliwafungulia watu kesi bila sababu wala ushahidi, basi wanaohusika wanaweza kurejea mahakamani kwa kuifungulia serikali kesi za fidia ya mabilioni ya fedha.

Sasa hiyo itakuwa ni hasara kwetu sisi walipa kodi kwa hiyo lazima Watanzania tukabili ufisadi kwa makini na weledi wa kutosha.
Ofisi ya DPP inasadikiwa kuwa imeajiri wanasheria wasomi, makini na wenye weledi wa hali ya juu.

Haya mambo ya mahakama kutuambia kuwa mtuhumiwa wa kosa husika hakuletwa mahakamani na badala yake ameletwa mtu ambaye hausiki na kosa hilo, hayaonyeshi usomi, umakini wala weledi wa kiwango chochote. Inaonekana wazi Ofisi ya DPP ina wanasheria ‘vihiyo’.

Hiyo ni aibu na si halali wananchi kutozwa kodi kuwalipa wanasheria wa seriakali mishahara na marupurupu kama ilivyo hivi sasa.

Kwa hiyo wananchi wenzangu tukae mkao wa kula kwa maana tuwe wasikivu siku ya Septemba 25 mwaka huu, ambayo ni Ijumaa ijayo, tufuatile mwenendo wa kesi hiyo na maelezo hayo ya awali ili mwisho wa yote tuweze kutoa tathmini kama haki imetendeka ama tupo kwenye mchezo mwingine wa kuigiza.

Nimalizie kwa kumwomba Mungu apishe mbali vituko vyote vinavyoweza kusababisha kesi ya Liyumba siku hiyo kuahirishwa.

Pia nawaombea jopo la mahakimu wakazi wanaosikiliza kesi hiyo likiongozwa na Edsons Mkasimwongo, Lameck Mlacha na Benedict Mwinga wawe na afya njema.

Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki afrika.

0716 774494
Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Jumapili, Septemba 20, 2009

No comments:

Powered by Blogger.