Header Ads

MANJI APINGA KUHAMISHWA QUALITY PLAZA

Na Happiness Katabazi

SIKU chache baada ya mmiliki wa Jengo la Quality Plaza Ltd, Image Properties and Estates Ltd, kuwataka wapangaji wake walipe malimbikizo ya kodi ya pango ndani ya siku 30 au wahame, miongoni mwa wapangaji akiwamo mmiliki wa Kampuni ya Quality Group Ltd, Yusuf Manji, na wenzake, wamekimbilia Mahakama Kuu Kitengo cha Ardhi kupinga uamuzi huo.

Mbali na Manji, wengine waliofungua kesi hiyo ni Kampuni ya Gaming Management Ltd, Q-Consuld Ltd, Quality Logistics Company Ltd, Internation Transit na Investment Ltd, dhidi ya Kampuni ya Image Properties, wamiliki wa jengo hilo lililopo Barabara ya Nyerere, Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa hati ya madai, Kampuni ya Quality Group Ltd iliwasilisha maombi hayo hivi karibuni na kesi hiyo imepewa namba 33 ya mwaka huu.

Kwa mujibu wa hati ya madai, kadhalika, walalamikaji hao wanaiomba mahakama itangaze taarifa iliyotolewa na mlalamikiwa (mmiliki wa jengo) si halali.

Pia walalamikaji wanaiomba mahakama itoe amri ya kumzuia mdaiwa kuwaingilia walalamikaji (wapangaji) kwenye jengo hilo wakati mkataba wao ukiwa unaendelea na pia kuiomba mahakama itoe amri ya mlalamikaji kulazimishwa kufuata masharti ya mkataba wa upangaji.

“Tunaomba mdaiwa aamriwe kumlipa mlalamikaji wa tatu dola 373,024.16 za Marekani kama ziada ya gharama za usimamizi wa jengo na pia kutulipa dola 135,300 kama madai ya walalamikaji kwa uharibifu uliosababishwa na mvua kutokana na uzembe wa mdaiwa,” walidai walalamikaji hao.

Aidha, wanaiomba mahakama itoe amri ya kumlazimisha mdaiwa aeleze dola 646,540 walizolipa walalamikaji kama kodi ya pango amezifanyia nini na kwamba amriwe kuwalipa gharama zisizozidi dola milioni moja.

Mapema mwaka 2005 walalamikaji waliingia mikataba mbalimbali ya kupanga ndani ya jengo hilo na mwaka huohuo mlalamikaji wa tatu alifanya makubaliano ya usimamizi wa jengo hilo na mdaiwa kwa ajili ya kuliangalia jengo hilo kwa mwaka mmoja ambapo baadaye aliongezewa muda hadi kufikia miaka miwili.

Hati hiyo ya madai inaeleza kwa sababu hiyo mlalamikaji wa tatu alikuwa analipa kodi ya kila mwezi na ilipofika mwaka 2006-2007, mdaiwa huyo alikuwa na uhalali wa kulipa dola 373,024.16 kama sehemu ya ada ya mwezi ya usimamizi wa jengo, fedha ambazo zilitumika na mlalamikiwa ameshindwa kuzirejesha.

Walidai kuwa kitendo cha mdaiwa kushindwa kurejesha kiasi hicho cha fedha ni kuvunja mkataba.

Mei 9 mwaka jana, mdaiwa alitoa siku 30 kwa wadai kuwa wawe wamemlipa dola 1,268,058.56 kama malimbikizo ya kodi na gharama nyingine ama sivyo wangeondolewa kwenye jengo; uamuzi walioupinga.Tayari kesi hiyo imeishapangwa kwa Jaji Atuganile Ngwala na itatajwa Machi 12 mwaka huu.

Chanzo:Gazeti la Tanzania Daima la Ijumaa, Machi 6 mwaka 2009

No comments:

Powered by Blogger.